Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nina Furaha Licha ya Ulemavu

Nina Furaha Licha ya Ulemavu

Nina Furaha Licha ya Ulemavu

Limesimuliwa na José Godofredo Várguez

Nilizaliwa nikiwa na afya nzuri na nikakua kama watoto wengine. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilianza kufanya kazi ya kuchomelea vyuma. Miaka miwili baadaye nilipokuwa nikichomelea vyuma fulani karibu na nyaya zinazopitisha umeme wenye nguvu nyingi, mvua ilianza kunyesha. Ghafula nilipigwa na umeme ambao uliniangusha chini mita 14, na kunifanya nipoteze fahamu. Sikurudiwa na fahamu kwa miezi mitatu. Nilipoamka ningeweza kusongeza kichwa tu. Nilipooza mikono na miguu na hilo lilinifanya niwe na majonzi!

MWANZONI nilimkasirikia Mungu na kumuuliza kwa nini aliniacha niendelee kuishi. Nilifikiria kujiua. Nilijaribu kutafuta msaada katika dini mbalimbali, lakini hakuna iliyotoa faraja ya kweli au hata kutosheleza uhitaji wangu wa kiroho. Kwa kweli, dini hizo hazikuwahimiza watu kuishi kulingana na mafundisho na kanuni za Biblia! Mama yangu alipokufa mnamo 1981, nilianza kunywa pombe na kucheza kamari. Nilifikiri kuwa kwa sababu ya hali yangu, Mungu angenihurumia na kunisamehe kwa sababu nilikuwa nikinywa pombe kupindukia. Pia, nikaanza kuishi maisha machafu kiadili kwa kuishi na mwanamke ambaye sikuwa nimefunga ndoa naye.

Badiliko Kubwa Katika Kufikiri Kwangu

Nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza nilipokuwa na umri wa miaka 37. Kwa kuwa mama yangu aliathiriwa na mambo ambayo watu walikuwa wakisema kuhusu Mashahidi wa Yehova, sikuzote alisema kwamba hiyo ndiyo dini mbaya kuliko zote. Hata hivyo, niliwaalika nyumbani kwangu nikiwa na kusudi la kuwapinga kwa sababu nilidhani kuwa ninajua mengi kuhusu Biblia. Lakini niligundua kuwa nilijua mambo machache tu! Isitoshe, wageni wangu walinishangaza kwa kuwa walijibu maswali yangu yote kwa kutumia Biblia. Niliamini kuwa nimeipata kweli.

Kwa kusikitisha mwanamke niliyekuwa nikiishi naye alikataa imani yangu mpya hivyo tukaachana. Niliendelea kubadilisha maisha yangu na pia mtazamo na fikira zangu ili zipatane na mafundisho ya Biblia. Pia, kwa msaada wa Mungu, nimebadilisha sana mtazamo na hisia zangu ili nikabiliane na madhara yaliyotokezwa na aksidenti niliyopata. Kwa sababu hiyo, nimepata uradhi kwa kutumikia nikiwa mweneza-injili wa wakati wote kwa miaka 20. Watu wengi hushangaa jinsi ninavyofaulu kwa sababu ya ulemavu wangu. Ninaishi na ndugu yangu mdogo, Ubaldo, naye ana ugonjwa unaoitwa Down. Ubaldo pia amekubali kweli za Biblia naye pia anamtumikia Yehova.

Sisi ni marafiki wakubwa nasi husaidiana. Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, Ubaldo husukuma kiti changu cha magurudumu na kubisha mlango, na ninapozungumza na mwenye nyumba yeye hunisaidia kufungua Biblia na kumwonyesha kichapo kinachofaa. Pia, yeye hunisaidia kufanya mambo mengine. Nami huuza vipodozi ili tujiruzuku. Kwa kuongezea, washiriki wa kutaniko letu la Mashahidi wa Yehova hutusaidia kutunza nyumba yetu, kupika, na kutupeleka hospitalini. Mimi na Ubaldo tunathamini hayo yote!

Ninatumikia nikiwa mzee katika kutaniko la Kikristo, na ndugu zangu wa kiroho hunisaidia kufanya utafiti katika Biblia. Pia, mimi hupiga mstari mambo makuu katika kitabu ninachojifunza nikitumia mdomo kushikilia penseli.

Watu wanaponiuliza ikiwa nina furaha, mimi hujibu ndiyo kwa moyo wote! Na hilo ni kweli. Nimepata kusudi halisi maishani na ninaendelea kutazamia tumaini jangavu ambalo Mungu amewawekea waabudu wake waaminifu, yaani, afya kamilifu katika Paradiso duniani.—Isaya 35:5, 6; Luka 23:43.

[Picha katika ukurasa wa 24]

José alipokuwa na umri wa miaka 18, mwaka mmoja kabla ya aksidenti

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mimi na ndugu yangu Ubaldo tunasaidiana sana tunapohubiri nchini Mexico

[Picha katika ukurasa wa 25]

Shahidi mwenzangu ananisaidia kufungua Biblia ninapotoa hotuba katika Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 25]

Washiriki wa kutaniko letu wanatusaidia kupika na kutunza nyumba yetu