Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kutumiaje Pesa Zangu kwa Hekima?

Ninaweza Kutumiaje Pesa Zangu kwa Hekima?

Maoni ya Biblia

Ninaweza Kutumiaje Pesa Zangu kwa Hekima?

“Mshahara wangu unapozidi kupungua, madeni yanaongezeka. Mara nyingi siwezi kulala nikiwazia jinsi nitakavyolisha familia yangu.”—James.

“Mimi huhisi kana kwamba niko katika hali mbaya sana na siwezi kujiokoa.”—Sheri.

UCHUMI unapozorota, ni jambo la kawaida kusikia maneno kama hayo. Juan Somavia, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Kimataifa la Wafanyakazi alisema hivi kuhusu kuzorota kwa uchumi: “Hili si janga linalokumba Soko la Hisa la Marekani tu. Ni janga linaloathiri kila mtu.”

Mtu anaweza kuwa na wasiwasi mwingi na hata akate tamaa anapopoteza kazi bila kutazamia au kukosa pesa kwa ajili ya mahitaji ya msingi ya familia. Wakati fulani, mwandishi mmoja wa Biblia, Daudi, alihisi hivyo. Alisali hivi: “Taabu za moyo wangu zimeongezeka; uniondoe katika mikazo iliyo juu yangu.” (Zaburi 25:17) Biblia inasema nini kuhusu nyakati zetu, na je, hekima yake inayotoka kwa Mungu inaweza kututia moyo na kutufanya tuwe na amani?

Hekima kwa Ajili ya Nyakati Ngumu

Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho” za ulimwengu huu kungekuwa na “maumivu ya taabu” na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:8) Maneno hayo sasa yanatimia! Lakini bado tuna tumaini, kwa kuwa kupitia Biblia Takatifu, Mungu ametuandalia hekima tunayohitaji ili kukabiliana na hali ngumu kiuchumi.

Kwa mfano, Biblia inatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa. Andiko la Mhubiri 7:12 linasema hivi: “Hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi; lakini faida ya ujuzi ni kwamba hekima huwahifadhi hai waliyo nayo.” Ndiyo, pesa zinaweza kuandaa ulinzi wa kadiri fulani, lakini hekima inayopatikana katika Biblia inatoa ulinzi wa kweli kila wakati. Hebu fikiria mifano ifuatayo.

Kukabiliana na Hali Ngumu za Kiuchumi

Uwe na bidii. “Mvivu anajionyesha kutamani, lakini nafsi yake haina chochote. Hata hivyo, nafsi ya wenye bidii itanoneshwa.” (Methali 13:4) Somo ni nini? Uwe na sifa ya uaminifu na kufanya kazi kwa bidii. Wafanyakazi wazuri huthaminiwa sana na waajiri wao nao huwa wa kwanza kupata kazi na wa mwisho kufutwa.— Waefeso 4:28.

Fikiria gharama kabla ya kununua. Yesu alisema hivi: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28) Ingawa Yesu alikuwa anaonyesha umuhimu wa kuhesabu gharama ya kuwa mfuasi wake, maneno yake ni ya kweli katika maana halisi. Kwa hiyo, tayarisha bajeti, ukiorodhesha vitu unavyohitaji na gharama yake.

Usipoteze pesa kwa mazoea mabaya. Mazoea kama vile kucheza kamari, kuvuta sigara, kutumia kileo vibaya na dawa za kulevya ni mambo yanayomchukiza Mungu.—Methali 23:20, 21; Isaya 65:11; 2 Wakorintho 7:1.

Epuka ‘kupenda pesa.’ (Waebrania 13:5) Watu wanaopenda pesa, hukosa furaha na hutamaushwa, na hilo huwafanya ‘wajichome wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.’ (1 Timotheo 6:9, 10) Zaidi ya hilo, wanakuwa watumwa wa tamaa ambayo hawawezi kutosheleza, kwa kuwa hata wawe na pesa nyingi kadiri gani, bado hazitawatosha.—Mhubiri 5:10.

Jifunze kuridhika. “Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:7, 8) Uchumi unapozorota, si rahisi watu wanaoridhika na vitu vichache wapatwe na wasiwasi. Hivyo jaribu kuwa na uradhi na uishi kulingana na mapato yako.—Ona sanduku upande wa kulia.

Hakuna mtu anayejua kitakachotokea kesho. Andiko la Mhubiri 9:11 linasema hivi: ‘Wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’ Hivyo watu wenye hekima, ‘huweka tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu,’ ambaye amewaahidi waaminifu wake hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—1 Timotheo 6:17; Waebrania 13:5.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Biblia inasema nini kuhusu nyakati zetu?—2 Timotheo 3:1-5.

● Leo tunaweza kupata wapi mwongozo wenye kutegemeka?—Zaburi 19:7.

● Ninaweza kufanya nini ili familia yangu iwe na wakati ujao wenye usalama?—Mhubiri 7:12.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

JINSI YA KUWEKA PESA AKIBA

Kununua bidhaa: Andika orodha. Epuka kununua vitu ambavyo hukupangia. Tafuta mahali palipo na bei ya chini. Angalia vikaratasi vya matangazo unapotafuta bidhaa. Nunua bidhaa zinapouzwa kwa bei ya chini na wakati ambapo hakuna wanunuzi wengi. Ikiwezekana, usinunue bidhaa mojamoja.

Gharama za nyumbani: Lipa madeni kwa wakati ili uepuke kulipia ada za ziada. Tayarisha chakula na vinywaji nyumbani, na utumie chakula na kileo kwa kiasi. Zima taa na vifaa vingine ikiwa huvitumii. Ikiwezekana, tumia vifaa visivyotumia umeme mwingi. Hakikisha nyumba yako haipotezi joto upesi. Fikiria kuhamia kwenye nyumba ndogo.

Usafiri: Ikiwa unahitaji gari, nunua gari linalotegemeka, lisilotumia petroli nyingi. Si lazima liwe gari jipya. Ikiwezekana unganisha shughuli zako na mtumie gari moja na watu wengine. Au tumia usafiri wa umma, baiskeli, au utembee. Enda likizo wakati bei ziko chini na ufanye hivyo karibu na nyumbani.

Simu na burudani: Je, unahitaji simu ya nyumbani pamoja na simu ya mkononi? Ikiwa watoto wako wana simu za mkononi, je, wanaweza kuzitumia mara chache zaidi au hata kutozitumia? Ikiwa umejiandikisha ili kupokea vituo vya televisheni, je, unaweza kupunguza idadi ya vituo unavyopokea? * Kodisha vitabu na sinema badala ya kuvinunua.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 26 Ili upate mapendekezo zaidi, ona makala “Tumia Pesa Zako kwa Hekima,” kwenye gazeti Amkeni! la Machi (Mwezi wa 3) 2009 na “Vijana Huuliza . . . Naweza Kutumiaje Pesa Zangu Vizuri?” gazeti Amkeni! la Juni (Mwezi wa 6) 2006.