Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafuta Msaada

Tafuta Msaada

Tafuta Msaada

“Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake.”—Mhubiri 4:12.

TUNAPOTEGEMEZWA na wengine, tunaweza kumshinda adui, hata awe nani. Kwa hiyo, ukitaka kushinda zoea la kuvuta sigara, huenda likawa jambo la hekima kuwaomba msaada watu wa familia na marafiki—au mtu yeyote mwenye subira na anayeweza kukusaidia.

Watafute wale ambao wamefaulu kuacha zoea hilo kwa kuwa huenda zaidi ya kuelewa hisia zako, wanaweza kukusaidia. “Msaada wa watu wengine ulikuwa muhimu sana,” anasema Torben, Mkristo huko Denmark. Abraham, anayeishi India, anaandika hivi: “Upendo wa kweli nilioonyeshwa na familia yangu na Wakristo wenzangu ulinisaidia kuacha.” Lakini nyakati nyingine huenda hata msaada wa watu wa familia na marafiki usitoshe.

“Nilivuta sigara kwa miaka 27,” anasema mwanamume anayeitwa Bhagwandas, “lakini nilipojifunza kile ambacho Biblia inasema kuhusu mazoea machafu, niliamua kuacha. Kwa hiyo, nilijaribu kupunguza kiasi cha sigara nilichokuwa nikivuta. Nilibadili marafiki. Nilitafuta msaada wa wataalamu. Lakini sikufaulu. Usiku mmoja nilizungumza na Yehova Mungu katika sala na kumsihi anisaidie kuacha. Mwishowe, nilifaulu!”

Jambo lingine muhimu ni kujitayarisha kwa ajili ya magumu utakayokabili. Magumu hayo ni yapi? Habari inayofuata inaeleza.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

JE, UTUMIE DAWA?

Dawa zinazowasaidia watu waache kuvuta sigara, zinawaletea wafanyabiashara faida ya mabilioni ya dola. Kabla ya kuanza kutumia dawa hizo, fikiria maswali yafuatayo:

Zina faida gani? Inasemekana kuwa matibabu mengi yanamsaidia mtu aache kuvuta sigara kwa kupunguza athari zinazotokea baadaye. Hata hivyo, bado kuna mjadala kuhusu faida zake za kudumu.

Kuna hatari gani? Dawa fulani hutokeza matatizo mengine kama vile kichefuchefu, mshuko wa moyo, na kumfanya mtu awe na mawazo ya kujiua. Pia, kumbuka kwamba dawa zinazotumiwa badala ya nikotini huletea mtu matatizo ya afya. Kwa sababu hiyo, mtu anayetumia dawa hizo za badala anaendeleza uraibu huo.

Je, kuna njia nyingine? Katika uchunguzi mmoja, asilimia 88 ya watu waliofaulu kuacha kuvuta sigara walisema walifanya hivyo bila kutumia dawa zozote.