Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ulipie Huduma za Kidini?

Je, Ulipie Huduma za Kidini?

Maoni ya Biblia

Je, Ulipie Huduma za Kidini?

KATIKA nchi nyingi, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo pamoja na zile zisizo za Kikristo, hutoza kwa ajili ya huduma zao za kidini. Huduma hizo zinaweza kutia ndani ubatizo, arusi, au mazishi. Malipo hayo yanaweza kuwa zaidi ya mamia au maelfu ya dola.

Makasisi fulani hulipwa na serikali wanapotoa huduma zao katika sherehe fulani na pia wanapofungua bunge kwa sala kila siku. Huenda watu wakafurahia na kuthamini huduma hizo na pia huenda makanisa yakawa na gharama zinazopaswa kulipiwa. Lakini je, Biblia inaunga mkono makanisa kutoza kwa ajili ya huduma za kidini, au kuwafanya watu wahisi kana kwamba ni lazima wazilipie?

“Nyumba ya Biashara”?

Yesu Kristo alipokuwa duniani, viongozi wa kidini Wayahudi na wengine walitumia sherehe za kidini kuwa pindi za kupata faida. Walifanya hivyo hasa wakati wa Pasaka. Je, Yesu alifurahishwa na matendo hayo? La! Biblia inatueleza kwamba ‘alimwaga sarafu za waliokuwa wakibadili pesa na kupindua meza zao.’ Kisha akasema: “Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!”—Yohana 2:14-16.

Jambo sawa na hilo lilitukia wakati wa nabii Mika, aliyeishi karne ya nane K.W.K. Biblia inaripoti kwamba viongozi wa kidini wa Israeli, ‘walichukia haki,’ na makuhani ‘walifundisha ili tu wapate malipo.’ Lakini, wakati uleule, walidai eti Mungu alikuwa akiwategemeza wakisema hivi: “Je, Yehova hayuko katikati yetu?” (Mika 3:9, 11) Lakini Yehova Mungu hakuunga mkono yale waliokuwa wakifanya. Alichukizwa sana na mwenendo wao na akawaeleza hivyo waziwazi kupitia nabii wake.

Leo viongozi wengi wa kidini hutumia mbinu hizohizo zenye pupa, na hivyo kufanya mahali pao pa ibada kuwa ‘nyumba za biashara.’ Mashirika ya kidini kwa ujumla hufanya biashara zenye kuleta faida kubwa sana kwa kuuza sanamu za kuchongwa, na bidhaa zingine. *1 Yohana 5:21.

“Mlipokea Bure, Toeni Bure”

Yesu alipowaagiza mitume wake wahubiri habari njema, waponye wagonjwa, na hata wafufue wafu, aliwaeleza hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:7, 8) Ndiyo, wafuasi wake wa kweli hawakupaswa kutoza huduma walizotoa. Zaidi ya hilo, Yesu mwenyewe aliweka mfano kwa kuwahudumia wengine bila malipo yoyote.

Akifuata mfano uliowekwa na Yesu, mtume Paulo alitimiza huduma yake “bila gharama.” (1 Wakorintho 9:18) Alipohitaji pesa, alifanya kazi ya kutengeneza hema. (Matendo 18:1-3) Kwa sababu hiyo, angeweza kusema hivi kujihusu na kuwahusu wamishonari wenzake: “Sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo.” (2 Wakorintho 2:17) Lakini namna gani kuhusu kukusanya pesa za kutumiwa na kutaniko, labda ili kununua au kukodi mahali pa ibada?

“Mungu Humpenda Mtoaji Mchangamfu”

Mashahidi wa Yehova hupata pesa wanazohitaji kupitia michango ya hiari. Wanatumia kanuni hii: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kwa sababu hiyo, Mashahidi hawatozi gharama yoyote kwa ajili ya vichapo au huduma za kidini, kama vile kubatiza, arusi, au mazishi. Wala hawadai fungu la kumi au kupitisha sahani kwenye mikutano yao. Mtu yeyote anayetaka kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya kimataifa anaweza kufanya hivyo kwenye masanduku ya michango katika mahali pao pa ibada.

Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hulipia Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, ofisi za tawi, viwanda vya kuchapishia, na pia kazi ya kutoa msaada kupitia michango ya hiari. Wengine, kama yule mjane mwenye uhitaji ambaye Yesu alimpongeza, wanaweza kutoa kiasi kidogo sana. (Luka 21:2) Wengine wanaweza kutoa kiasi kikubwa. Hata mtu atoe kiasi gani, maadamu anafuata kanuni zilizowekwa katika Biblia na kutoa kulingana na uwezo wake, anakuwa mwenye uradhi mwingi, anapata baraka nyingi kutoka kwa Mungu, na kupata furaha ya kweli.—Matendo 20:35; 2 Wakorintho 8:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia: Je, Tumwabudu Mungu Kupitia Sanamu?” katika Amkeni! la Agosti 2008.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Yesu aliwaambia nini watu waliokuwa wakifanya biashara hekaluni?—Yohana 2:14-16.

● Je, mtume Mkristo Paulo alikubali malipo kwa huduma za kidini alizotoa?—2 Wakorintho 2:17.

● Yehova hupendezwa na mtoaji wa aina gani?—2 Wakorintho 9:7.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

“Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!”—Yohana 2:14-16