Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko

Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko

Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko

Biblia inazungumza kuhusu “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Bila shaka, utakubali kwamba leo tunaishi katika nyakati zilizo na mfadhaiko mkubwa.—2 Timotheo 3:1.

KAMA unavyojua, ni rahisi kuzima moto mdogo kuliko moto mkubwa. Vivyo hivyo, ni rahisi kudhibiti mfadhaiko mdogo mara tu unapotokea kuliko kudhibiti mfadhaiko mkubwa ambao umekuwapo kwa muda mrefu. Daktari mmoja alisema kwamba “licha ya maisha yetu yenye shughuli nyingi, ni muhimu tuwe na zoea la kupunguza mfadhaiko kila siku.” *

Kuna faida mbili za kuwa na zoea la kupunguza mfadhaiko kila siku. Kwanza, hilo litasaidia kupunguza mambo yanayosababisha mfadhaiko maishani. Na pili, litasaidia kudhibiti jinsi tunavyotenda tunapopata mfadhaiko usioweza kuepukwa.

Je, Biblia inatoa mwongozo ambao unaweza kutusaidia kukabiliana na mfadhaiko?

Kweli za Biblia Ni Muhimu

Kwa kufyonza kweli zilizo katika Biblia, tunaweza kupata mawazo ya Muumba wetu yenye kuburudisha na kuridhisha. Neno la Mungu ni chanzo cha mwongozo wenye thamani. Kwa kweli, Biblia ina kweli nyingi za kiroho zinazoweza kutupa kitulizo kutokana na mfadhaiko! Kweli hizo zinaweza kutusaidia ‘tusitetemeke wala kuwa na hofu’ na tufanikiwe kukabiliana na mfadhaiko kila siku.—Yoshua 1:7-9.

Biblia inatusaidia kupunguza mfadhaiko kwa njia yenye kupendeza kwa kutuhakikishia kwamba Baba yetu wa kimbingu, Yehova, “ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) “Jambo moja ambalo limenisaidia sana,” anasema Patricia, aliyekuwa profesa katika chuo kikuu kimoja huko California, “ni kufikiria kuhusu mapenzi ya Mungu na mambo ya ajabu anayotimiza.”

Fikiria jinsi matendo na maneno ya Yesu Kristo yenye fadhili yalivyowaburudisha wasikilizaji wake waliokuwa wamekandamizwa na kufadhaika. Alisihi hivi: “Njoni kwangu nyinyi nyote mnaofanyishwa kazi kupita kiasi na kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha [yaani, nitawaburudisha kiroho].”—Mathayo 11:28-30, The New Testament—An Understandable Version; mabano ni yao.

Kwa kweli, Yesu hakuwa mkali. Badala yake, alifikiria mahitaji ya kihisia na ya kimwili ya wanafunzi wake, hata akafanya mipango ili waweze kupumzika kutokana na shughuli zao nyingi za kuhubiri. (Marko 6:30-32) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu, ambaye sasa ni Mfalme mbinguni anaelewa hisia zetu tunapopatwa na mfadhaiko wenye kulemea. Kwa rehema, yeye anatusaidia kwa kutupa “msaada kwa wakati unaofaa.”—Waebrania 2:17, 18; 4:16.

Umuhimu wa Mawasiliano Mazuri

Mawasiliano mazuri ni mojawapo ya njia zenye matokeo za kudhibiti mfadhaiko. Biblia inafundisha: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” (Methali 15:22) Kwa hiyo, watu wengi wamegundua kwamba kuzungumza na mwenzi wao wa ndoa, rafiki, au mfanyakazi mwenzao husaidia sana kupunguza mfadhaiko.

Njia muhimu sana na yenye kufaa ya kuwa na “mazungumzo ya siri” ni kusali kwa Mungu. Kusali kwa ukawaida kunaweza kukusaidia ‘usihangaike juu ya kitu chochote.’ Wengi wameona kwamba kutegemea sala kumewasaidia kupata “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” Na kulingana na ahadi ya Biblia, ‘mioyo na nguvu zao za kufikiri’ hulindwa.—Wafilipi 4:6, 7; Methali 14:30.

Kitabu kimoja kuhusu mfadhaiko kinasema kwamba “watu walio na marafiki wa kuwategemeza hukabiliana vizuri zaidi na mfadhaiko na wana afya nzuri ya akili kuliko wale wanaojaribu kufanya kila kitu bila kuhusisha wengine.” Marafiki bora zaidi wanaoweza kututegemeza ni wale wanaomwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Kwa kutii agizo la Biblia, wao hukutanika pamoja kwa ukawaida na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Mtu mmoja ambaye huhudhuria mikutano hiyo alisema hivi: “Nyakati nyingine mimi hufanya kazi kwa saa nyingi, na ninapatwa na mfadhaiko mkubwa. Hata hivyo, ninapoenda kwenye mikutano, kufikia wakati wa sala ya mwisho, mfadhaiko wangu huwa umekwisha nami huhisi nimeburudishwa.”

Jambo lingine muhimu ambalo halipaswi kupuuzwa tunapokabiliana na mfadhaiko ni ucheshi. Mhubiri 3:4 inasema kwamba kuna “wakati wa kulia na wakati wa kucheka.” Kucheka huburudisha na pia hutokeza manufaa za kiafya kwa kuwa kama daktari mmoja alivyoeleza, “tunapocheka, mwili hutokeza kemikali inayoitwa endorphin na kuzuia kutokezwa kwa adrenalini.” Mwanamke mmoja aliyeolewa alisema hivi: “Tukiwa chini ya hali yenye mfadhaiko sana, mume wangu husema au kufanya jambo lenye kuchekesha na hilo husaidia sana.”

Sifa Zinazopunguza Mfadhaiko

Biblia inatutia moyo tukuze sifa zinazopunguza mfadhaiko. Sifa hizo ambazo zinaitwa “matunda ya roho” ya Mungu zinatia ndani “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, [na] kujizuia.” Pia Biblia inatuhimiza tuepuke “uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.” Kisha inaongezea hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”—Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 4:31, 32.

Daktari mmoja alieleza manufaa ya kufuata mafundisho hayo ya Biblia, hasa katika ulimwengu wa leo. Alisema: “Kuwatendea watu kwa heshima husaidia kupunguza mfadhaiko.” Biblia inatusaidia pia kuwa na kiasi, yaani, kujua mipaka ya uwezo wetu.—Mika 6:8.

Mungu anatarajia tukubali kwa unyenyekevu mipaka ya uwezo wetu wa kimwili, kiakili, na kihisia na kwamba hatuwezi kufanya kila jambo tunalotaka kufanya. Huenda tukahitaji kujifunza wakati wa kukataa kufanya mambo yanayopita uwezo wetu hata ingawa ikawa vigumu kufanya hivyo.

Hilo halimaanishi kwamba tukifuata mashauri yote yanayotegemea Biblia yaliyotolewa katika habari hii, hatutapatwa na mfadhaiko wowote. Ukweli wa mambo ni kwamba Shetani Ibilisi anawalenga wale wanaomwabudu Mungu ili kuthibitisha kwamba wataacha ibada ya kweli wakipatwa na mfadhaiko mwingi. (Ufunuo 12:17) Lakini, kama vile tumeona, Mungu hutoa msaada kwa wakati wake katika njia mbalimbali ili kutusaidia kupunguza na kukabiliana na mfadhaiko. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Unapokabili mfadhaiko mkali au unaoendelea kwa muda mrefu, inapendekezwa umwone mtaalamu ili upate matibabu.

^ fu. 20 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko, tafadhali soma mfululizo wa makala “Kukabiliana na Mfadhaiko” katika toleo la Amkeni! la Februari 8, 2005 (8/2/2005), na “Kukabiliana na Hekaheka za Leo,” katika toleo la Februari 8, 2001.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

NJIA FULANI ZA KUPUNGUZA MFADHAIKO

● Usitarajie ukamilifu kutoka kwako au kwa wengine.—Mhubiri 7:16.

● Panga mambo yanayofaa kutangulizwa.—Wafilipi 1:10, 11.

● Fanya mazoezi kwa ukawaida.—1 Timotheo 4:8.

● Furahia uumbaji wa Yehova.—Zaburi 92:4, 5.

● Tenga wakati wa kuwa peke yako mahali patulivu.—Mathayo 14:23.

● Pumzika na upate usingizi wa kutosha.—Mhubiri 4:6.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuwasiliana ni muhimu ili kupunguza mfadhaiko

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kusitawisha sifa za kimungu husaidia kupunguza mfadhaiko