Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Nitunze Afya Yangu?

Kwa Nini Nitunze Afya Yangu?

Vijana Huuliza

Kwa Nini Nitunze Afya Yangu?

Weka alama ya ✔ kando ya jambo ambalo ungetaka kutimiza.

Kupunguza uzito

Kuboresha ngozi yangu

Kuwa na nguvu zaidi

Kukaza fikira zaidi

Kupunguza mahangaiko

Kudhibiti hasira

Kujiamini zaidi

UKIWA kijana kuna mambo ambayo huwezi kuchagua. Kwa mfano, huwezi kuchagua wazazi wako, ndugu na dada zako, mahali unapoishi, na kadhalika. Lakini, ubora wa afya yako unaweza kutegemea mambo uliyorithi na pia jinsi unavyoishi. *

Huenda ukasema, ‘Lakini mimi sijazeeka hivi kwamba nianze kuhangaikia afya yangu!’ Je, wewe una maoni kama hayo? Hebu tazama orodha ya mambo yaliyo hapo juu. Ulitia alama mambo gani? Amini usiamini, kuwa na afya nzuri ndiyo siri kuu ya kutimiza kila moja ya malengo hayo.

Kwa kweli, huenda una maoni kama ya Amber * mwenye umri wa miaka 17 aliyesema, “Sifurahii kula chakula kinachotokana na nafaka ambayo haijatolewa maganda, chakula kilicho na mafuta kidogo na kisicho na sukari kila siku!” Ikiwa unahisi hivyo, tulia, kuwa na afya nzuri hakumaanishi uwe kama watu wanaopenda kufanya mazoezi kupita kiasi, uache kula peremende, au ukimbie mbali sana kila juma. Kwa kweli, utahitaji tu kufanya mabadiliko machache ili uwe na afya nzuri, ujihisi vizuri, na utimize mengi. Acha tuchunguze jinsi vijana wenzako walivyofaulu.

Kula Vizuri—Uwe na Afya Nzuri!

Biblia inatuhimiza tuwe na kiasi katika mazoea yetu. Methali 23:20 inasema hivi: “Usiwe . . . kati ya watu wanaokula . . . kwa ulafi.” Si rahisi kufuata himizo hilo.

“Kama vijana wengi, mimi huhisi njaa kila wakati. Wazazi wangu wamefananisha tumbo langu na shimo lisilo na mwisho!”—Andrew, 15.

“Kwa sasa sioni ubaya wa kula chakula fulani kwa kuwa sihisi madhara yake.”—Danielle, 19.

Je, unahitaji kudhibiti jinsi unavyokula? Yafuatayo ni mambo yaliyowasaidia vijana wenzako.

Sikiliza tumbo lako. “Nilikuwa nikihesabu kalori, lakini sasa mimi huacha kula ninapohisi nimeshiba,” anasema Julia, mwenye umri wa miaka 19.

Epuka chakula kisicho na lishe bora. “Nilipoacha kunywa soda, nilipunguza kilo tano baada ya mwezi mmoja,” anasema Peter, mwenye umri wa miaka 21.

Badili mazoea yako ya kula. “Mimi hujaribu sana nisiongeze chakula,” anasema Erin, mwenye umri wa miaka 19.

Siri ya Kufanikiwa: Usikose kula hata mlo mmoja! Ukikosa utahisi njaa na huenda ukashawishika kula chakula kingi.

Fanya Mazoezi—Uhisi Vizuri!

Biblia inasema hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Lakini vijana wengi hawapendi kufanya mazoezi.

“Nilipokuwa shule ya sekondari vijana wengi walishindwa na somo la mazoezi. Lilikuwa somo rahisi kama tu kula!”—Richard, 21.

“Vijana wengine hujiambia, ‘Kwa nini nikimbie-kimbie jua likiwa linawaka hadi nitoe jasho na nichoke ilhali ninaweza kucheza mchezo wa video?’”—Ruth, 22.

Je, wewe huhisi umechoka unaposikia neno “mazoezi”? Ikiwa ndivyo, zifuatazo ni faida za kuwa na mazoea mazuri ya kufanya mazoezi.

Faida ya 1. Mazoezi huongeza uwezo wa mfumo wa kinga wa mwili wako. “Baba yangu alikuwa akiniambia hivi, ‘Ikiwa huwezi kutafuta wakati wa kufanya mazoezi, basi tafuta wakati wa kuwa mgonjwa,’” anasema Rachel, mwenye umri wa miaka 19.

Faida ya 2. Mazoezi hufanya ubongo wako utokeze kemikali zenye kutuliza. “Kukimbia hunituliza, hasa wakati nina mawazo mengi,” anasema Emily, mwenye umri wa miaka 16. “Mimi huhisi mwili umepumzishwa, na hisia zimetulia.”

Faida ya 3. Mazoezi yanaweza kukufurahisha. “Mimi hufurahia kucheza nje ya nyumba,” anasema Ruth, mwenye umri wa miaka 22, “hivyo mazoezi yangu hutia ndani kutembea, kuogelea, kuteleza juu ya theluji, na kuendesha baiskeli.”

Siri ya Kufanikiwa: Tenga angalau dakika 20 mara tatu kila juma ili ufanye mazoezi unayofurahia na yatakayokufanya utumie nguvu nyingi.

Lala Vizuri—Utimize Mengi!

Biblia inasema hivi: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Ikiwa hutaweza kulala vizuri pia hutaweza kutimiza mengi!

“Nisipolala vya kutosha, siwezi kufanya mambo kwa njia nzuri! Mimi hushindwa kukazia fikira jambo lolote!”—Rachel, 19.

“Inapofika saa nane mchana, mimi huwa nimechoka hivi kwamba ninaweza kulala nikiwa ninazungumza na mtu!”—Kristine, 19.

Je, unahitaji kulala zaidi? Yafuatayo ni mambo ambayo vijana wenzako wameamua kufanya.

Epuka kulala ukiwa umechelewa. “Nimekuwa nikijaribu kulala mapema,” anasema Catherine, mwenye umri wa miaka 18.

Katiza mazungumzo. “Wakati fulani marafiki hunipigia simu au kunitumia ujumbe kwenye simu usiku sana,” anasema Richard, mwenye umri wa miaka 21, “lakini sasa nimejifunza kukatiza mazungumzo ili nilale.”

Lala na uamke saa zilezile kila siku. “Siku hizi mimi hujaribu kulala na kuamka saa zilezile kila siku,” anasema Jennifer, mwenye umri wa miaka 20.

Siri ya Kufanikiwa: Jaribu kulala kwa muda wa saa nane hadi kumi kila siku.

Ni mambo gani kati ya mambo matatu yaliyozungumziwa unayohitaji kufanyia kazi maishani mwako?

kula mazoezi kulala

Andika hapa chini mradi unaoweza kukusaidia utimize lengo lako.

․․․․․

Utapata faida nyingi ikiwa utafanya mambo machache ili kutunza afya yako. Kumbuka kuwa ukiwa na afya nzuri utaonekana vizuri, utahisi vizuri, na utatimiza mengi zaidi. Tofauti na mambo mengine maishani, una uwezo wa kuboresha hali yako ya kimwili. “Mwishowe,” anasema Erin mwenye umri wa miaka 19, “ubora wa afya yako unakutegemea wewe tu.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Tunafahamu kuwa watu wengi wanakabili matatizo ya kiafya au ulemavu ambao hawawezi kubadili. Habari hii inaweza kuwasaidia watu hao kuwa na afya nzuri wakiendelea kukabiliana na matatizo yao.

^ fu. 13 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Kutunza afya yako kutakusaidia jinsi gani ujiamini zaidi?

● Utaonyesha jinsi gani kuwa una usawaziko kuhusu afya yako?—Wafilipi 4:5.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Mwili wa mwanadamu ni kama gari—ni jukumu la mwenye gari kulitunza. Hiyo ni sababu moja inayonichochea nifanye mazoezi.”

“Kufanya mazoezi mkiwa wawili kutakufanya ujitahidi sana kwa kuwa hutaki kumvunja moyo mwenzako.”

“Mimi hufurahia sana jinsi ninavyohisi ninapofanya mazoezi. Mwili wangu unapoanza kuonekana vizuri kwa sababu ya mazoezi, mimi hutiwa moyo sana!”

[Picha]

Ethan

Briana

Emily

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

“NILIBADILI MAISHA YANGU”

“Nilipokuwa na umri wa miaka sita, nilikuwa mzito kidogo ikilinganishwa na umri wangu. Kisha, polepole niliacha kuonjaonja chakula mara kwa mara na nikaanza kula wakati wote hasa vyakula visivyo na lishe bora! Kwa kuwa sikupenda kutumia nguvu, sikufanya kazi yoyote ngumu. Bila kutambua nikawa mnene kupita kiasi, jambo ambalo sikutaka. Nilihuzunishwa sana na jinsi nilivyoonekana na kuhisi! Mara kadhaa nilijaribu kupunguza uzito kwa kula chakula maalumu lakini baada ya muda nilinenepa tena. Mwishowe nilipokuwa na umri wa miaka 15 niliamua kubadili maisha yangu. Nilitaka kupunguza uzito kwa njia inayofaa—njia ambayo ningeweza kudumisha katika maisha yangu yote. Nilinunua kitabu kilichozungumzia kanuni za msingi za lishe na kufanya mazoezi, na nikaanza kufanyia kazi kile nilichosoma. Niliazimia kuendelea hata ikiwa nitashindwa kula chakula kinachofaa na kufanya mazoezi au hata kama ningevunjika moyo. Matokeo? Nilifaulu! Baada ya mwaka mmoja nilipunguza kilo 25. Nimedumisha uzito huo kwa miaka miwili. Sikufikiri ningefaulu! Nafikiri nilifaulu kwa kuwa sikula tu chakula fulani maalumu bali pia nilibadili maisha yangu. Nilipoelewa kuwa hali hiyo ingeathiri kila sehemu ya maishani yangu, nilikuwa tayari kufanya mabadiliko yaliyohitajika.”—Catherine, 18.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Afya yako ni kama gari—usipolitunza vizuri, litaharibika