Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfadhaiko Hatari Kubwa kwa Afya

Mfadhaiko Hatari Kubwa kwa Afya

Mfadhaiko Hatari Kubwa kwa Afya

“Ninafanya kazi kwa muda mrefu, usiku na mchana. Mara nyingi ninapomaliza upasuaji katika hospitali moja, ninakuwa na dakika chache tu za kwenda kwenye hospitali nyingine kupitia barabara yenye msongamano mwingi ili nikashughulikie upasuaji mwingine.”—Dakt. Peter Stuart, Afrika Kusini.

HUENDA unaelewa hisia za Dakt. Stuart, hata ikiwa hali zinazokuletea mfadhaiko ni tofauti na zake. Hata mfadhaiko wako uwe unasababishwa na jambo gani—iwe ni kuendesha gari katika barabara zenye msongamano mkubwa, hali ya kutoelewana nyumbani au kazini, au iwe ni jambo tofauti—ni kawaida kwa wanadamu kukabiliana na mfadhaiko.

Zaidi ya karne 30 zilizopita, mwanajeshi mwenye uzoefu alikiri hivi waziwazi: “Kutetemeka kunaingia ndani yangu, na mtetemeko unanifunika.” (Zaburi 55:5) Mwanamume huyo alielewa mfadhaiko ni nini. Alipokuwa kijana mchungaji, alikabiliana na simba, dubu, na shujaa aliyekusudia kumwua.—1 Samweli 17:4-10, 23, 24, 34-36, 41-51.

Kwa kweli, si vibaya kupatwa na mkazo. Mkazo unaweza kutusaidia tukabiliane na kipingamizi. Watu wanapokabiliwa na hali zinazohatarisha maisha, mkazo umewawezesha kufanya mambo ambayo hawakufikiria wanaweza kufanya. Ulipokuwa na mgawo muhimu, huenda mkazo ulitokeza adrenalini ndani yako na hilo likakuchochea umalize mgawo huo kwa wakati. *

Hata hivyo, mkazo unapozidi sana mwili wetu hushindwa kutulia kisha tunafadhaika. Mtafiti mmoja anasema kwamba “mfadhaiko ndio unaotokeza hatari kubwa zaidi kwa afya yetu.” Ikiwa unahisi kwamba huwezi kuvumilia mfadhaiko wako au ikiwa ungependa kuepuka kupatwa na mfadhaiko mkali, huenda ukajiuliza, “Je, kuna jambo lolote ninaloweza kufanya ili nipunguze mfadhaiko?”

Ndiyo kunalo! Wote wanaweza kupata msaada ambao umewasaidia watu wengi kukabiliana na mfadhaiko. Msaada huo unatoka katika chanzo ambacho hungetazamia, yaani, Neno la Mungu, Biblia. Ingawa Biblia si kitabu cha kutoa msaada wa kitiba, kina hekima inayoweza kutusaidia. Kinaeleza kwa nini watu wanafadhaika sana leo na kinaonyesha mambo yanayosababisha au kuchangia mfadhaiko. Pia kina mapendekezo ya kutusaidia kupunguza na kukabiliana na mfadhaiko.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Adrenalini ni homoni inayotokezwa na tezi za adrenali na inakusaidia kukabiliana na hali za dharura.