Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kupunguza Gharama

Jinsi ya Kupunguza Gharama

Jinsi ya Kupunguza Gharama

ILI upunguze gharama zako unahitaji kupanga mambo kwa uangalifu. Yesu alikazia umuhimu wa jambo hilo. Aliuliza hivi: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28, 29) Kwa kutumia kanuni hiyo, unaweza “kuhesabu gharama” ya kuishi kulingana na mapato yako ikiwa utapanga bajeti. Kwa njia gani? Hebu jaribu kufanya hivi:

Unapopata mshahara wako, tenga pesa hususa katika vikundi tofauti ili kushughulikia gharama za sasa au za wakati ujao. (Ona sanduku kwenye  ukurasa wa 8.) Unapopanga gharama zako, unaweza kuona mahali pesa zako zinaenda na unatumia kiasi gani kununua vitu visivyo vya lazima. Kufanya hivyo kutakusaidia kuamua jinsi unavyoweza kupunguza gharama zako.

Ili upange bajeti inayokufaa, jaribu kutumia mapendekezo yafuatayo.

Tumia Busara Unaponunua Vitu

Raúl alipoachishwa kazi, mke wake Bertha, alibadili mbinu yake ya kununua vitu. Anasema, “Niliangalia matangazo yaliyoonyesha mahali ambapo bidhaa zimepunguzwa bei na maduka ya mboga yaliyouza vitu viwili kwa bei ya kimoja.” Zifuatazo ni mbinu nyingine:

Pika vyakula vinavyopatikana kwa wingi.

● Jipikie chakula badala ya kununua kilichopikwa na kupakiwa.

● Nunua bidhaa za ziada zinapopatikana kwa wingi au kwa bei ya chini.

● Nunua vitu kwa jumla, lakini jihadhari usijaze vitu vinavyoweza kuharibika upesi.

● Punguza gharama kwa kununua mavazi mazuri yaliyotumika.

● Safiri hadi maeneo ambako bei ni za chini, ikiwa hutatumia pesa nyingi kwa ajili ya usafiri.

● Punguza safari za kwenda dukani. *

Andika

Fred anasema, “Tulilazimika kupanga bajeti, kwa hiyo, niliandika gharama ambazo tulihitaji kulipa mara moja na pesa za matumizi ya mwezi mzima.” Mke wake, Adele, anasema hivi: “Nilijua ni pesa ngapi nitakazotumia ninapoenda sokoni. Nyakati nyingine nilipohitaji kununua kitu cha nyumbani au kwa ajili ya watoto, niliitazama bajeti na kujiambia, ‘Sina pesa za kukinunua, kwa hiyo, tutasubiri hadi mwezi ujao.’ Kuandika kulinisaidia sana!”

Fikiria Kabla ya Kununua

Uwe na zoea la kujiuliza: ‘Je, kweli ninahitaji kitu hiki? Je, kweli kile cha zamani kimechakaa, au ninataka tu kitu kipya?’ Ikiwa hutumii kitu fulani kwa ukawaida, je, si afadhali tu kukodi kitu hicho? Au ikiwa unafikiri kwamba utakitumia mara nyingi, je, unaweza kununua kilichotumika?

Ingawa huenda ikaonekana kuwa jambo dogo kufanya mambo yaliyotajwa hapa juu, yanapofanywa yote yanaweza kusaidia sana! Jambo kuu ni, ukiwa na zoea la kuokoa pesa unazotumia kwa ajili ya vitu vidogovidogo, utafanya hivyo pia unaposhughulikia mambo makubwa.

Tafuta Njia za Kupunguza Gharama

Ili uokoe pesa unazotumia kununua vitu visivyo vya lazima, uwe mbunifu. Kwa mfano, Adele anasema hivi: “Tulikuwa na magari mawili lakini tukauza moja na kutumia hilo lingine. Ili tuokoe pesa tulizotumia kununua petroli, tulipanga kufanya shughuli nyingi kwa wakati mmoja. Tulitumia pesa kwa ajili tu ya vitu vya lazima.” Zifuatazo ni njia nyingine zinazoweza kukusaidia kupunguza gharama:

● Kuza mboga zako nyumbani.

● Fuata maagizo ya watengenezaji wa vifaa, ili vidumu kwa muda mrefu.

● Badili mavazi yako mazuri mara tu unapofika nyumbani kwani kufanya hivyo kutayafanya yadumu yakiwa mapya kwa muda mrefu zaidi.

Usijitenge!

Watu wengi ambao hupoteza kazi hujitenga na wengine. Lakini Fred hakujitenga! Alitegemezwa kwa fadhili na watu wa familia yake, kutia ndani watoto wake wakubwa. Anasema hivi: “Tulijifunza kushirikiana katika mambo mengi na hilo lilitufanya tuwe na uhusiano wa karibu. Sote tulijiambia hivi, ‘Hili ni tatizo letu sisi sote.’”

Pia, Fred aliimarishwa na Wakristo wenzake alipokutana nao kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Kila wakati baada ya mikutano yetu ya Kikristo, nilihisi nimetiwa moyo. Kila mtu alikuwa mwenye fadhili na ufikirio. Faraja na msaada wao ulitufanya tutambue kwamba hatuko peke yetu.”—Yohana 13:35.

Manufaa za Kuwa na Imani

Kuachishwa kazi kumewafanya mamilioni ya watu wahisi wakiwa wamechukizwa na kusalitiwa na waajiri wao. Raúl aliyetajwa hapo awali, alivunjwa moyo alipopoteza kazi mara mbili, kwanza katika nchi ya nyumbani ya Peru na kisha huko New York City. Baada ya kuachishwa kazi mara ya pili, Raúl alisema, “Katika ulimwengu wa leo, huwezi kutegemea kitu chochote.” Kwa miezi mingi, hakufanikiwa kupata kazi. Ni nini kilichomsaidia kukabiliana na hali hiyo? Raúl alisema, “Nilisitawisha urafiki wa karibu pamoja na Mungu na nikatambua kwamba ninaweza kumtegemea kikamili.”

Raúl ni Shahidi wa Yehova, na kujifunza Biblia kumemsaidia asitawishe imani yenye nguvu katika Baba wa mbinguni mwenye kujali ambaye anaahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Hali zilikuwa ngumu. Raúl anasema, “Sikuzote tulisali ili tupate mahitaji ya lazima, na tulijifunza kuridhika na kile ambacho Mungu alituandalia.” Bertha, mke wa Raúl, anasema hivi: “Nyakati nyingine nilikuwa na wasiwasi mwingi nikijiuliza ikiwa Raúl atapata kazi. Lakini tuliona kwamba Yehova alijibu sala zetu kwa kutuandalia mahitaji yetu kila siku. Hata ingawa hatukuwa na vitu vingi kama hapo awali, maisha yetu yalikuwa rahisi zaidi sasa.”

Kwa kuwa Fred ni Shahidi wa Yehova kujifunza Biblia kumemsaidia sana kukabiliana na hali yake. Anasema hivi: “Nyakati nyingine, tunategemea sana kazi, cheo, au pesa tulizo nazo kwenye benki. Lakini nilijifunza kwamba ni Yehova Mungu peke yake anayeweza kumtegemeza kikweli, na uhusiano wetu pamoja naye ndio unaoweza kutuletea utegemezo huo.” *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 60 hivi ya bidhaa zote zilizonunuliwa hazikuwa zimepangiwa.

^ fu. 30 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kutumia pesa vizuri, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2009 (1/8/2009) ukurasa wa 10-12.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Sikuzote tulisali ili tupate mahitaji ya lazima, na tulijifunza kuridhika na kile ambacho Mungu alituandalia”

[Sanduku/Ramani katika ukurasa wa 8]

 Jinsi ya Kupanga Bajeti

(1) Andika gharama za lazima za kila mwezi. Weka rekodi ya pesa zote unazotumia mwezi mzima kwa chakula, nyumba, malipo ya huduma mbalimbali, gharama za gari, na kadhalika. Kwa ajili ya gharama zinazolipiwa kila mwaka, gawa gharama hizo mara 12 ili uhifadhi pesa hizo kila mwezi.

(2) Orodhesha gharama katika vikundi mbalimbali. Chakula, nyumba, gari, usafiri, na kadhalika.

(3) Tambua ni pesa ngapi ulizohifadhi utakazotumia kila mwezi kulipia matumizi ya kila kikundi kwenye orodha yako. Kwa ajili ya gharama za kila mwaka, “piga hesabu” ni pesa ngapi unazopaswa kuhifadhi kila mwezi.

(4) Andika jumla ya mapato yote ya kila mtu nyumbani. Ondoa malipo kama vile kodi. Linganisha na gharama.

(5) Tenga kiasi unachohitaji kila mwezi ili kulipia kila kikundi. Ikiwa unatumia pesa taslimu, njia rahisi ni kuwa na bahasha iliyo na alama ya kila kikundi. Kisha, tia pesa zinazohitajika ili kugharimia mahitaji hayo ndani ya kila bahasha.

Tahadhari: Ikiwa unatumia kadi ya mkopo, fanya hivyo kwa hekima! Bajeti za watu wengi zimevurugwa na tamaa ya ‘kununua sasa, kulipia baadaye.’

[Chati]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mapato ya Mwezi

MSHAHARA WA MWEZI Sh.․․․․․ MAPATO MENGINE Sh.․․․․․

MSHAHARA WA WATU

WENGINE NYUMBANI Sh.․․․․․ JUMLA YA MAPATO HALISI

Sh.․․․․․

Gharama za Mwezi Pesa

Ulizopangia Ulizotumia

Sh.․․․․․ Kodi ya Nyumba Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Bima/Kodi Nyingine Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Gharama za Huduma Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Gharama za Gari Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Burudani/Usafiri Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Simu Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Chakula Sh.․․․․․

Sh.․․․․․ Gharama Nyingine Sh.․․․․․

JUMLA JUMLA

Sh.․․․․․ Sh.․․․․․

Linganisha na Matumizi

MAPATO YA MWEZI Sh.․․․․․

ONDOA− SALIO

MATUMIZI YA MWEZI Sh.․․․․․ Sh.․․․․․