Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Msiwe na Wasiwasi Juu ya Kesho”

“Msiwe na Wasiwasi Juu ya Kesho”

“Msiwe na Wasiwasi Juu ya Kesho”

Renée alikuwa amekata tamaa. Mume wake Matthew, hakuwa ameajiriwa kwa zaidi ya miaka mitatu. “Nilikuwa nimefadhaika sana,” anasema Renée. “Nilivunjika moyo sana kwa kuwa sikujua ni nini ambacho kingetokea!” Matthew alijaribu kumtuliza mke wake kwa kumweleza kwamba hakuna wakati ambapo wamewahi kukosa kile walichohitaji. “Lakini bado huna kazi!” Renée akajibu. “Tunahitaji pesa!”

BILA shaka kupoteza kazi humfanya mtu ahangaike. Mtu asiye na kazi hujiuliza, ‘Nitakaa kwa muda gani bila kazi? Tunaweza kutosheleza mahitaji ya familia yetu kwa njia gani?’

Ingawa ni kawaida kuwa na mahangaiko kama hayo, Yesu Kristo alitoa mashauri haya mazuri yanayoweza kupunguza mahangaiko. Alisema hivi: “Msiwe na wasiwasi juu ya kesho . . . Matatizo ya siku moja yanawatosheni kwa siku hiyo.”—Mathayo 6:34, Biblia Habari Njema.

Tambua Mambo Yanayokutia Wasiwasi

Yesu hakuwa akisema kwamba tunapaswa kutenda kana kwamba hatuna matatizo. Hata hivyo, kuhangaikia mambo yanayoweza kutokea kesho kutakuongezea tu wasiwasi leo. Kwa kweli, hatuwezi kuzuia mambo yatakayotokea kesho, yawe mazuri au mabaya. Lakini tunaweza kuchukua hatua za kukabiliana na mahangaiko ya leo.

Bila shaka, si rahisi kufanya hivyo. Rebekah, ambaye mume wake alikuwa amepoteza kazi aliyokuwa ameifanya kwa miaka 12 anasema hivi: “Unapokabiliwa na hisia kali, ni vigumu kufikiria mambo kihalisi. Lakini tulilazimika kufanya hivyo. Kwa hiyo, nilijaribu kudhibiti hisia zangu. Mambo yaliyonitia wasiwasi yalipokosa kutokea, nilitambua kwamba kuhangaika hakuna faida yoyote. Tulipokazia fikira mambo ya sasa na matatizo yaliyokuwapo, tulipunguza mfadhaiko.”

Jiulize: ‘Ni nini kinachonitia wasiwasi? Kuna uwezekano gani kwamba jambo linalonitia wasiwasi litatukia? Mimi hutumia nguvu nyingi kadiri gani kuhangaika kuhusu jambo ambalo huenda likatokea au lisitokee?’

Jifunze Kuridhika

Mtazamo wetu unaweza kuathiri hisia zetu. Kwa hiyo, Biblia inatuhimiza tuwe na mtazamo huu wa akili: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Kuridhika kunamaanisha kupunguza mambo tunayotaka na kutosheka wakati mahitaji yetu ya kila siku yanapotimizwa. Kujitahidi kutosheleza tamaa zetu kutavuruga jitihada zetu za kupunguza gharama.—Marko 4:19.

Renée alifaulu kukuza sifa ya kuridhika baada ya kuona hali yake kihalisi. Anasema hivi: “Hatujawahi kukosa umeme au gesi, wala hatujakosa makao. Tatizo kuu ni kwamba hatukuwa tumezoea kuishi kwa njia hiyo, na tamaa yangu ya kudumisha maisha tuliyokuwa nayo iliongeza tu mfadhaiko wangu.”

Punde si punde, Renée alitambua kwamba si hali zake zilizofanya maisha yake yawe magumu bali ni mtazamo wake. Anasema hivi: “Nilihitaji kuona hali yetu kihalisi bila kukazia fikira jinsi nilivyotaka mambo yawe. Nilipoanza kuridhika na yale ambayo Mungu alituandalia kila siku, nilikuwa na furaha zaidi.”

Jiulize: ‘Je, mahitaji yangu ya leo yameshughulikiwa? Ikiwa ndivyo, je, ninaweza kukazia fikira mambo ya leo nikiwa na uhakika kwamba ya kesho yatashughulikiwa pia?’

Kuwa na mtazamo unaofaa ndiyo hatua ya kwanza ya kukabiliana na ugumu wa kupunguza gharama zetu. * Lakini unaweza kuchukua hatua gani zinazofaa ikiwa mapato yako yameathiriwa na kupoteza kazi?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ili upate habari zaidi kuhusu kutafuta na kudumisha kazi, ona Amkeni! la Julai 8, 2005 (8/7/2005), ukurasa wa 3-11.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Mvumilivu Hula Mbivu!

Baada ya kutafuta kazi kwa majuma kadhaa bila kufaulu, Fred alihisi kwamba juhudi zake zimegonga mwamba. Alisema hivi, “Ilikuwa kama kusubiri mtu akuchukue kwenye kituo cha basi lakini hakuna anayetokea.” Fred aliamua kufanya yote ambayo angeweza. Alituma maombi ya kazi kwenye kampuni yoyote ambayo ingehitaji ujuzi wake hata kama ni kwa kadiri ndogo sana. Alifuatilia majibu yote aliyopokea na kujitayarisha kwa ajili ya mahojiano yote, akiwa amesadiki kwamba “mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Methali 21:5) Fred anasema, “Kwenye kampuni moja, nilihojiwa mara mbili na meneja wakuu.” Lakini Fred alipata matokeo mazuri kwa sababu ya bidii yake. Anasema hivi, “Mwishowe niliajiriwa!”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Jambo Muhimu Kuliko Mshahara

Ni nini muhimu zaidi—utu wako au mshahara wako? Hebu ona methali mbili za Biblia.

“Afadhali maskini anayetembea katika utimilifu wake kuliko mtu yeyote aliyepotoka katika njia zake, ingawa ni tajiri.”—Methali 28:6.

“Afadhali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ng’ombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.”—Methali 15:17.

Sifa zako nzuri na thamani yako haipotei unapopoteza kazi. Hivyo, mume wa Renée alipoachishwa kazi, aliwaambia hivi watoto wake: “Akina baba wengi wameacha familia zao. Lakini baba yenu bado yuko. Mnajua kwamba anawapenda na amewasaidia mlipokuwa na matatizo. Hamwezi kupata baba mzuri kuliko yeye!”