Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

Vijana Huuliza

Nifanye Nini ili Nielewane na Ndugu na Dada Zangu?

Una uhusiano wa aina gani na ndugu na dada zako?

․․․․․ Marafiki wazuri sana

․․․․․ Mara nyingi tunaelewana

․․․․․ Tunavumiliana

․․․․․ Tunagombana kila wakati

NDUGU na dada fulani huwa na uhusiano wa karibu sana. Kwa mfano, Felicia, mwenye umri wa miaka 19, anasema, “Dada yangu, Irena, mwenye umri wa miaka 16, ni mmoja wa marafiki wangu wa karibu zaidi.” * Carly, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi kuhusu Eric, ndugu yake aliye na umri wa miaka 20: “Tunaelewana kabisa. Hatugombani hata kidogo.”

Kwa upande ule mwingine, vijana wengi wana uhusiano kama ule wa Lauren na Marla. Lauren anasema, “Sisi hugombana kuhusu kila kitu, haidhuru ni jambo dogo kiasi gani.” Au labda hali yako ni sawa na ile ya Alice mwenye umri wa miaka 12, anayesema hivi kuhusu ndugu yake Dennis mwenye umri wa miaka 14: “Yeye huniudhi sana! Yeye huingia chumbani mwangu na kuchukua vitu bila ruhusa. Dennis ana utoto mwingi!”

Je, una ndugu au dada anayekuudhi sana? Ni kweli kwamba ni daraka la wazazi kudumisha amani katika familia. Hata hivyo, itakubidi ujifunze kupatana na watu wengine. Unaweza kujifunza jambo hilo ukiwa bado nyumbani.

Fikiria kuhusu mambo ambayo husababisha kutoelewana kati yako na ndugu au dada zako. Kwa kawaida nyinyi huzozana kuhusu nini? Hebu tazama orodha iliyo hapa chini, kisha utie alama hii ✔ kwenye kisanduku kinachofaa au uandike jambo ambalo linakuudhi sana!

Vitu ulivyo navyo. Ndugu au dada yangu huchukua vitu bila kupewa ruhusa.

Nyutu kutofautiana. Ndugu au dada yangu hutenda kwa ubinafsi au bila kunijali au hata hujaribu kunitawala.

Faragha. Ndugu au dada yangu huingia chumbani mwangu bila kubisha mlango au yeye husoma barua-pepe zangu au ujumbe kwenye simu yangu ya mkononi bila kuniomba ruhusa.

Sababu nyingine. ․․․․․

Ikiwa ndugu au dada yako hukuudhi kila mara kwa mfano, anakuambia kile unachopaswa kufanya kila wakati, au hakuruhusu uwe na faragha, inaweza kuwa vigumu kujidhibiti usiwe na chuki. Lakini methali moja ya Biblia inasema hivi: “Kufinya pua ndiko hutokeza damu, na kuchochea hasira ndiko hutokeza ugomvi.” (Methali 30:33) Unapoweka kinyongo, kinaweza kufanya ufoke kwa hasira, kama vile tu kufinya pua lako kunavyoweza kufanya damu itoke. Halafu tatizo hilo litakuwa baya hata zaidi. (Methali 26:21) Unaweza kujizuia jinsi gani unapokasirika ili usianzishe magombano makubwa? Hatua ya kwanza ni kutambua tatizo.

Je, Ndilo Chanzo cha Tatizo au Ni Tukio tu?

Matatizo kati ya ndugu na dada ni kama chunusi. Chunusi inapotokea, ngozi huwasha na huwa haivutii, lakini chanzo chake ni maambukizo. Vivyo hivyo, ndugu na dada katika familia wanapozozana vikali ni lazima tatizo hilo liwe na chanzo.

Unaweza kuamua kufinya chunusi. Hata hivyo, kufanya hivyo kutaondoa tu dalili, na kuacha makovu au kuzidisha tatizo hilo. Ni afadhali kushughulikia tatizo lenyewe na hivyo kuzuia lisitokee tena. Ni hali moja na kutatua matatizo kati yako na ndugu au dada yako. Jifunze kutambua chanzo cha tatizo lenyewe, na hivyo utaweza kulitatua kwa undani si kijuujuu tu. Pia, utatumia shauri la Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyesema: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.”—Methali 19:11.

Kwa mfano, Alice, aliyetajwa hapo mwanzo, alisema hivi kuhusu ndugu yake Dennis, “Yeye huingia chumbani mwangu na kuchukua vitu bila ruhusa.” Hilo ndilo tukio. Lakini unafikiri tatizo ni nini? Huenda linahusiana na ukosefu wa heshima. *

Huenda Alice angekabiliana na tatizo hilo kwa kumwambia Dennis asiingie chumbani mwake wala asitumie vitu vyake kamwe. Lakini kufanya hivyo ni kama kutibu tu dalili na huenda hilo likaanzisha mzozo mwingine. Hata hivyo, ikiwa Alice angemsadikisha Dennis aheshimu vitu vyake na pia faragha yake, bila shaka uhusiano wao ungeboreka.

Jifunze Kutatua au Kuepuka Mizozo

Kwa kweli, kutambua chanzo cha matatizo unayokabili kati yako na ndugu au dada yako ni sehemu tu ya suluhisho. Unaweza kufanya nini ili kutatua tatizo hilo na kuepuka kuzozana tena wakati ujao? Jaribu kufuata hatua sita zifuatazo.

1. Wekeni sheria fulani za msingi. “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri,” akaandika Mfalme Sulemani. (Methali 15:22) Ili usikate tamaa, hebu angalia kile ulichotaja kuwa ndicho chanzo cha mzozo kati yako na ndugu au dada yako. Ona ikiwa mnaweza kuweka sheria fulani ambazo nyote wawili mtakubali ziwaongoze na ambazo zitasaidia kutatua tatizo lenu. Kwa mfano, ikiwa mnagombana kuhusu vitu, Sheria ya 1 inaweza kuwa: “Kabla ya kuchukua kitu cha mwenzako mwombe ruhusa.” Sheria ya 2 inaweza kusema hivi: “Heshimu uamuzi wa ndugu au dada yako anaposema, ‘Hapana, usitumie kitu hicho.’” Mnapoweka sheria hizo, kumbukeni amri ya Yesu: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Mkifanya hivyo mtaweka sheria ambazo wewe na ndugu au dada yako mnaweza kufuata. Halafu waelezeni wazazi wenu sheria hizo kuhakikisha kwamba wanakubaliana nazo.—Waefeso 6:1.

2. Fuata sheria hizo wewe mwenyewe. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba?” (Waroma 2:21) Unaweza kutumia kanuni hiyo jinsi gani? Kwa mfano, ikiwa ungetaka ndugu au dada yako aheshimu faragha yako, wewe pia unapaswa kubisha mlango wa chumba chake kabla ya kuingia au kuomba ruhusa kabla ya kusoma barua-pepe zake au ujumbe katika simu yake.

3. Usikasirike upesi. Kwa nini shauri hilo linafaa? Kwa sababu kama methali moja ya Biblia inavyosema, “wajinga ndio hukasirika upesi na kuweka kinyongo.” (Mhubiri 7:9, Contemporary English Version) Kwa hiyo, ikiwa kila wakati unakasirika upesi, utakosa furaha. Kwa kweli, ndugu au dada yako atafanya au kusema mambo yatakayokuudhi. Lakini hebu jiulize, ‘Je, nimemwudhi kwa njia kama hiyo wakati fulani uliopita?’ (Mathayo 7:1-5) Jenny anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 13, nilifikiri kwamba maoni yangu ndiyo yaliyokuwa sawa kabisa na lazima yafuatwe. Sasa dada yangu mdogo anapitia hali kama hiyo. Kwa hiyo, mimi hujitahidi sana nisiudhike anaposema mambo yenye kuudhi.”

4. Samehe na usahau. Matatizo mazito yanahitaji kuzungumziwa na kutatuliwa. Lakini je, ni lazima uzingatie kila kosa ambalo ndugu au dada yako anafanya? Yehova Mungu anathamini sana ‘unapopita kosa.’ (Methali 19:11) Alison, mwenye umri wa miaka 19, anasema hivi: “Kwa kawaida mimi na dada yangu Rachel husuluhisha matatizo kati yetu vizuri. Sote huwa tayari kuomba msamaha kwanza halafu tunaeleza sababu iliyofanya tugombane. Wakati mwingine mimi hungoja kwa muda kabla ya kuzungumzia tatizo fulani. Mara nyingi, baada ya wakati kupita inakuwa rahisi kusamehe na kusahau.”

5. Waombe wazazi wako wawe wapatanishi. Ikiwa wewe na ndugu au dada yako hamwezi kusuluhisha tatizo fulani, wazazi wako wanaweza kuwasaidia mfanye amani. (Waroma 14:19) Hata hivyo, kumbuka kwamba uwezo wa kutatua tatizo bila kuhusisha wazazi husaidia kuonyesha kwamba umekomaa kwa kadiri fulani.

6. Thamini sifa nzuri za ndugu au dada yako. Huenda ndugu au dada yako ana sifa ambazo unapendezwa nazo. Andika chini jambo moja ambalo unathamini kuhusu kila mmoja wa ndugu na dada zako.

Jina Sifa inayonipendeza

․․․․․ ․․․․․

Badala ya kufikiria sana kuhusu makosa ya ndugu au dada yako, ni vizuri utafute nafasi ya kumweleza kuhusu sifa zake zinazokuvutia.—Zaburi 130:3; Methali 15:23.

Ukweli kuhusu maisha: Utakapotoka nyumbani, huenda utachangamana na watu watakaokuudhi, kama vile wafanyakazi wenzako na wengine ambao hawana adabu, wasiojali hisia za wengine, na wenye kujipenda. Ukiwa bado nyumbani, una nafasi nzuri ya kujifunza jinsi ya kukabiliana na magumu kama hayo. Ikiwa una ndugu au dada ambaye hampatani kwa urahisi, uwe na maoni yanayofaa kwa sababu anakusaidia usitawishe sifa muhimu utakazotumia maishani!

Biblia inasema wazi kwamba si lazima ndugu au dada yako wa kimwili awe rafiki yako wa karibu zaidi. (Methali 18:24) Lakini unaweza kuimarisha urafiki pamoja na ndugu au dada zako ‘mkiendelea kuvumiliana,’ hata ikiwa watakupa “sababu ya kulalamika.” (Wakolosai 3:13) Ukifanya hivyo, huenda usiudhike sana na mambo ambayo ndugu au dada zako watafanya. Na hata wewe pia hutawaudhi sana!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 20 Kwa habari zaidi, ona  sanduku lililo hapa chini.

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Kwa nini ni muhimu kutambua tofauti kati ya tukio na chanzo cha tatizo lenyewe?

● Ni jambo gani kati ya mambo sita yaliyotajwa hapo juu unayopaswa kufanyia kazi zaidi?

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

TAMBUA CHANZO CHA TATIZO

  Je, ungependa kuboresha ujuzi wako wa kutambua matatizo kati yako na ndugu au dada zako? Ikiwa ndivyo, soma mfano wa Yesu kuhusu kijana fulani aliyehama nyumbani na kutumia vibaya urithi wake.—Luka 15:11-32.

Ona jinsi yule ndugu mkubwa alivyotenda wakati ndugu yake mdogo aliporudi nyumbani. Kisha ujibu maswali yafuatayo.

Ni tukio gani lililomfanya yule ndugu mkubwa atende kwa njia hiyo?

Unafikiri chanzo cha tatizo hilo lilikuwa nini?

Baba yao alijaribu kutatua tatizo hilo jinsi gani?

Yule ndugu mkubwa alihitaji kufanya nini ili kutatua tatizo hilo?

Sasa fikiria ugomvi ambao umetokea kati yako na ndugu au dada yako hivi karibuni. Halafu andika majibu kando ya maswali yafuatayo.

Ni nini kilichosababisha ugomvi huo?

Unafikiri chanzo cha tatizo hilo ni nini?

Ni sheria gani za msingi mnazoweza kuweka ili kutatua tatizo hilo na kuzuia ugomvi wakati ujao?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28, 29]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Ninataka tuwe marafiki wa karibu na dada zangu maisha yangu yote, kwa hiyo afadhali nianze urafiki huo sasa.”

“Sisi hufanya mambo pamoja tukiwa familia, na hilo hutuunganisha pamoja. Siku hizi hatugombani sana kama zamani.”

“Kwa njia fulani sisi ni tofauti sana kama vile giza na nuru. Hata hivyo, dada yangu ni wa pekee sana. Ninampenda sana!”

“Kama singekuwa na ndugu au dada zangu, singekuwa na kumbukumbu yoyote yenye kupendeza. Kwa wale wote walio na ndugu na dada wa kimwili, ningependa kuwaambia, ‘Waonyesheni kwamba mnawathamini!’”

[Picha]

Tia

Bianca

Samantha

Marilyn

[Picha katika ukurasa wa 27]

Matatizo kati ya ndugu na dada ni kama chunusi—ili kuzitibu vizuri unahitaji kushughulikia chanzo si dalili tu