Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninasubiri Wakati Nitakapowaambia, “Sote Tupo Hapa!”

Ninasubiri Wakati Nitakapowaambia, “Sote Tupo Hapa!”

Ninasubiri Wakati Nitakapowaambia, “Sote Tupo Hapa!”

Limesimuliwa na Abigail Austin

Nilikuwa na umri wa miaka tisa. Siku moja mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1995, tuliamua kwenda tafrija maeneo ya vijijini pamoja na wengine katika kutaniko letu la Mashahidi wa Yehova. Tulianza safari tukiwa katika magari kadhaa. Mimi nilikuwa katika gari la wazazi wetu pamoja na dada yangu mkubwa, Sarah, na rafiki wa familia yetu anayeitwa Deborah. Ghafula, gari likaja kwa kasi sana upande wetu wa barabara na kuligonga gari letu. Ni mimi tu niliyepona.

N ILIAMKA majuma mawili baadaye nikiwa hospitalini. Fuvu la kichwa changu lilikuwa limevunjika na madaktari walikuwa wameingiza vipande kadhaa vya chuma ili kulishikilia. Hata hivyo, nilipona upesi. Watu wa ukoo waliniambia kilichotukia nami sikuwaamini. Kila wakati nilijiambia kwamba wazazi wangu na dada yangu walikuwa wamenitembelea nilipokuwa nimelala kwa hiyo sikuwaona. Lakini niliporudi nyumbani, ndipo nilipotambua ukweli wa mambo. Nilifadhaika sana.

Ni nini kilichonisaidia kukabiliana na msiba huo mbaya?

Urithi Wangu wa Kiroho

Mimi ndiye kitinda-mimba katika familia ya watoto watano. Wakati wa aksidenti, Sarah alikuwa na umri wa miaka 22, Shane alikuwa na miaka 20, Jessica alikuwa na miaka 17, na Luke alikuwa na miaka 15. Tulikuwa na wazazi wazuri waliotujali sana. Baba yangu, Steve, alitumika akiwa mzee katika Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la West Yorkshire huko Shipley naye alipendwa na wote kwa sababu aliwasikiliza kwa subira na kuwasaidia wengine. Mama yangu, Carol, pia alipendwa na wengi kwa kuwa aliwatunza wenye umri mkubwa kutanikoni kama binti yao. Alipanga tafrija kwa ajili ya vijana na akatusaidia kupata marafiki wazuri. Watu wote walikaribishwa kwetu. Wazazi walitufundisha kuwa na fadhili na wenye ufikirio hata kwa majirani wetu.

Kila Jumatano (Siku ya 3) jioni tulijifunza Biblia pamoja tukiwa familia. Nyakati nyingine tuliigiza drama za Biblia na kuvalia kama watu wa nyakati za Biblia. Tangu tulipokuwa wachanga, Baba na Mama walitufundisha jinsi ya kutayarisha mikutano na kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia nyumbani kwao. Ingawa walikuwa na mengi ya kufanya kwa sababu walikuwa na watoto watano, wazazi wetu walitumia wakati pamoja nasi na kutusaidia kuwa na nguvu kiroho.

Sarah, Shane, na Jessica, walipomaliza shule, walianza kuwa mapainia, yaani, Wakristo wanaohubiri wakati wote, pamoja na rafiki yetu Deborah. Mimi na Sarah tulikuwa na uhusiano wa karibu sana. Alikuwa kama mama kwangu, na tulipofunga shule, tulitumia wakati mwingi pamoja tukiwasaidia watu wajifunze Biblia. Nilifurahia sana pindi hizo. Niliona kwamba mapainia wote walikuwa na furaha sana, nami nilifurahi kuwa pamoja nao. Nilijiwekea mradi wa kufanya upainia pamoja na Sarah baada ya kumaliza shule.

Wakati wa sikukuu, familia yetu ilifanya mambo pamoja na wengine kutanikoni. Urafiki na upendo kati ya vijana na wazee ulizidi kukua. Sikutambua jinsi ambavyo marafiki hao wangenisaidia na kunifariji katika siku zijazo!

Baada ya Aksidenti

Nilipotoka hospitalini, nilirudi nyumbani. Shane na Jessica walijitahidi sana kutuandalia riziki na kututunza kwa kufanya kazi za muda huku wakiendelea kuhubiri wakati wote.

Mashahidi wengi katika kutaniko letu walitusaidia. Walitufanyia mambo mengi! Walituandalia milo, walitusafishia nyumba, wakatununulia vitu, na kutufulia nguo, hadi tulipoweza kujitunza. Tulishukuru sana. Tulipata zawadi na kadi nyingi sana za kututia moyo kutoka kwa Mashahidi wa mbali na wa karibu, hilo likionyesha kwamba kuna upendo mwingi sana ndani ya tengenezo la Yehova.

Baada ya mwaka mmoja hivi, ndugu zangu wawili na dada yangu waliamua kwamba nilihitaji kuwa katika familia imara. Familia kadhaa zenye fadhili kutanikoni zilikuwa tayari kusaidia, kwa hiyo ndugu zangu na dada yangu waliketi chini na kufikiria ni familia gani ambao Mama na Baba wangeona kuwa ingenitunza vizuri kiroho na kimwili. Familia moja ilikuwa ya pekee sana. Billy, ambaye ni mzee wa kutaniko, na mke wake, Dawn, walikuwa marafiki wa karibu sana wa familia yetu, na walikuwa na binti mwenye umri wa miaka mitano anayeitwa Lois. Walinipokea nyumbani mwao na tangu wakati huo wamenitunza kwa upendo kama binti yao mwenyewe. Ingawa Lois alilazimika kunigawia upendo wa wazazi wake, hawajawahi kuwa na wivu, na leo tuna uhusiano wa karibu kama tu dada halisi.

Jinsi Nilivyokabiliana na Msiba

Mwanzoni, nilijiuliza kwa nini msiba huo mbaya ulikuwa umeipata familia yetu, hasa kwa kuwa wazazi wangu, na vilevile Sarah na Deborah, walikuwa wameonyesha wazi kwamba wanampenda sana Yehova na watu wengine. Lakini nikakumbuka simulizi la Biblia kumhusu Ayubu, ambaye aliendelea kuwa na imani katika Mungu licha ya kuwapoteza watoto wake. (Ayubu 1:19, 22) Nilijiambia, ‘Naam, Shetani alisababisha kuteseka na kifo ulimwenguni, naye atafurahi sana ikiwa msiba huu utatuzuia tusimtumikie Mungu.’ (Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9) Nilikumbuka pia kwamba Yehova ametuandalia tumaini zuri ajabu la ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Tutaiona tena familia yetu pamoja na Deborah, katika dunia iliyo paradiso! Kwa kweli, upendo wangu kwa Yehova umeongezeka.

Ninapokutana na watu ambao pia wamepatwa na misiba, mimi huhuzunika sana iwapo hawajasikia ahadi yenye thamani ya Biblia kuhusu ufufuo. Ninahisi kwamba ninataka kuwaeleza kuhusu tumaini hilo, kwa kuwa nina hakika kwamba ni kwa msaada wa Yehova na tengenezo lake tu kwamba tumefaulu kukabiliana vema na kipindi hiki kigumu sana tukiwa na tumaini.

Huenda pia hali yetu imesaidia kwa njia nyingine, ikiwafanya wazazi fulani wajiulize, ‘Je, tumewawekea watoto wetu msingi imara wa kiroho hivi kwamba iwapo tutapatwa na chochote, wao wataendelea kumtumikia Yehova?’

Nimejaribu kuishi ni kana kwamba bado Mama na Baba wako hai. Ninajua kwamba wangetaka nijitahidi sana kuwasaidia wengine, kama vile wao walivyofanya. Nilianza upainia mara tu nilipomaliza shule, na sasa Lois pia anatumika pamoja nami akiwa painia. Ndugu zangu na dada yangu wamefunga ndoa na wanamtumikia Yehova kwa furaha katika makutaniko yao.

Ninatazamia kwa hamu ulimwengu mpya wa Mungu na ufufuo! Hakutakuwa na maumivu wala kifo tena. (Ufunuo 21:3, 4) Kujua kwamba tutakuwa tena pamoja kunanisaidia nivumilie hata kukiwa na matatizo. Ninasubiri kwa hamu kumkumbatia Mama, Baba, Sarah, na Deborah na kuwaambia, “Sote tupo hapa!”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Abigail (wa pili kushoto) akiwa na familia yake ya kambo leo