Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakili Awachunguza Mashahidi wa Yehova

Wakili Awachunguza Mashahidi wa Yehova

Wakili Awachunguza Mashahidi wa Yehova

“NILIFAHAMU mambo machache sana kuwahusu Mashahidi wa Yehova,” anasema wakili Les Civin ambaye pia ni msimamizi wa shirika fulani la sheria huko Afrika Kusini. Kwa nini alitaka kuchunguza mambo ambayo Mashahidi wanaamini? Alifikia mkataa gani? Yafuatayo ni mambo aliyomweleza mwandishi wa Amkeni!

Ulikuwa ukishirikiana na dini gani?

Nililelewa katika familia ya Kiyahudi, lakini katika miaka ya 1970, nilimwoa Carol, ambaye alikuwa Mwanglikana. Hakupendezwa sana na mambo ya kidini, na dini haikuwa jambo muhimu maishani mwetu wakati huo. Hata hivyo, mwana wetu Andrew alipokuwa na umri wa miaka minane, Carol alihisi kuwa tunahitaji kumpa msingi fulani wa kidini. Rabi mmoja aliniambia kwamba ikiwa Carol angegeuka na kuwa Myahudi, basi Andrew angekuwa Myahudi moja kwa moja na angefanyiwa sherehe inayoitwa Bar Mitzvah (sherehe ya Kiyahudi inayoonyesha mtu amekuwa mtu mzima) wakati ambapo angetimia umri wa miaka 13. Hivyo, tukaanza kuhudhuria masomo ya kugeuzwa imani yaliyokuwa yakifanywa kila juma katika sinagogi.

Ulikutana na Mashahidi wa Yehova jinsi gani?

Kila mara Mashahidi walipokuja mlangoni petu nilikatiza mazungumzo yao. Niliwaambia, “Mimi ni Myahudi na siamini Agano Jipya.” Kisha Carol akaniambia kuwa rafiki yake mmoja ni Shahidi na anajua Biblia vizuri. Kwa hiyo, Carol akapendekeza tujifunze mambo mengi zaidi kuhusu Biblia. Nilikubali shingo upande kujifunza Biblia na Mashahidi.

Ulikuwa na maoni gani kuhusu funzo hilo la Biblia?

Nilikuwa na kiburi. Nilikuwa tu nimeanza kujifunza tena kuhusu imani yangu ya Kiyahudi na hilo lilinifanya nihisi kuwa mimi ni wa jamii iliyochaguliwa. ‘Watu hawa watanifundisha nini?’ nilijiuliza. Mara ya kwanza kuzungumza na Shahidi aliyekuja nyumbani nilimweleza hivi: “Nilizaliwa nikiwa Myahudi. Hiyo ndiyo dini yangu na nitakufa nikiwa Myahudi. Hakuna kitu unachoweza kunieleza kitakachofanya nibadili imani yangu.” Kwa fadhili aliniambia kuwa anaheshimu msimamo wangu. Hivyo, kila Ijumaa (Siku ya 5) na Jumatatu (Siku ya 1) usiku, tulihudhuria masomo ya Kiyahudi na Jumapili (Siku ya Yenga) asubuhi tulijifunza na Mashahidi (ikiwa singeweza kuepuka). Lakini tofauti ni kwamba funzo lao lilikuwa bure, lakini tulilipia masomo ya sinagogi.

Nilitumia Biblia yangu ya Kiyahudi kwa kuwa nilidhani kuwa Mashahidi walitumia tafsiri iliyopendelea mafundisho yao. Hata hivyo, nilishangaa sana kugundua kuwa Biblia hizo mbili zilipatana sana. Hilo lilinifanya nitake sana kuwathibitishia Mashahidi kuwa hawakujua kile walichokuwa wakizungumzia.

Baada ya kuhudhuria masomo kadhaa ya rabi, Carol aliniambia kwamba anaona kuwa rabi haifahamu Biblia vizuri. Naye akanifahamisha kuwa ataacha kuhudhuria masomo hayo na hataacha kumfuata Kristo. Nikiwa nimekasirika, nilifikiria kuvunja ndoa yetu. Hata hivyo, nilipotulia niliamua kutumia mbinu nyingine. Niliamua kutumia uwezo wangu wa kisheria kumthibitishia Carol kuwa ‘madhehebu hiyo hatari’ haikuwa dini ya kweli.

Je, ulifaulu?

Rabi alinipa kitabu kilichoandikwa ili kuthibitisha kuwa Yesu hakutimiza unabii wowote wa Kimasihi. Tulijifunza kitabu hicho pamoja na Carol kwa miezi 18. Pia, tuliendelea kujifunza kila juma na Mashahidi. Hata hivyo, tulipochunguza kila unabii katika kitabu tulichopewa na rabi, wasiwasi wangu uliongezeka. Tofauti na maelezo ya kitabu hicho, unabii wa Kimasihi ulio ndani ya Biblia ulielekeza kwa mtu mmoja tu—Yesu Kristo. Mwishowe, tukajifunza kuhusu unabii unaopatikana katika Danieli 9:24-27, uliotabiri kuwa Masihi angetokea mwaka wa 29 W.K. * Shahidi huyo alitoa tafsiri ya Kiebrania iliyokuwa na neno la Kiingereza chini ya kila neno la Kiebrania. Niliangalia maandishi hayo, na nikapiga hesabu ya matukio, kisha nikasema: “Sawa, unabii unatuelekeza kwenye mwaka wa 29 W.K. Kwa hiyo, tarehe hiyo inamhusu Yesu jinsi gani?”

“Huo ndio mwaka ambao Yesu alibatizwa,” Shahidi huyo alijibu.

Jambo hilo lilinishangaza sana! Pia, nilishangaa kuona jinsi unabii wa Biblia ulivyokuwa sahihi na jinsi ulivyopatana kabisa.

Marafiki wako walitenda jinsi gani ulipobadili maoni?

Wengine walihisi kuwa tumepotea na wakaahidi kutuletea watu ambao wangetuthibitishia kuwa tulikuwa tukidanganywa. Lakini mambo tuliyokuwa tumejifunza yalitegemea utafiti na mambo yanayopatana na akili.

Ni nini kilichokufanya uamue kuwa Shahidi?

Mwanzoni, nilihudhuria mikutano michache katika Jumba la Ufalme na mke wangu ambaye wakati huo alikuwa Shahidi. * Nilishangazwa na urafiki wa Mashahidi na upendo walioonyeshana bila kujali rangi ya mtu. Sikuwahi kuona watu katika dini yangu wakifanya hivyo. Hivyo, nilijifunza kwa miaka mingine mitatu kisha nikabatizwa.

Unahisi jinsi gani kuhusu uamuzi wako wa kuwa Shahidi?

Ni pendeleo kubwa kusema, “Mimi ni Shahidi wa Yehova.” Lakini ninapofikiria jinsi nilivyoipinga kweli, mimi huhisi kuwa sistahili baraka ambazo Yehova amenipa. Sitawahi kujutia uamuzi niliofanya.

Umefurahia baraka gani?

Baraka nyingi. Kwanza, ninafurahia pendeleo la kutumikia nikiwa mzee, au mchungaji wa kiroho na mwalimu, katika kutaniko letu. Pia, nimesaidia katika Idara ya Sheria katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini. Lakini, bila shaka, baraka kubwa zaidi ni kumjua Yehova na Mwana wake na kuelewa umuhimu wa wakati huu tunamoishi na matukio ya maana yanayotokea ulimwenguni leo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 W.K. inamaanisha “Wakati wa Kawaida.” Ili upate habari zaidi kuhusu unabii wa Danieli kumhusu Masihi, ona ukurasa wa 197 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

^ fu. 18 Carol alikufa mwaka wa 1994, na Les Civin alioa tena.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Nilishangaa kuona jinsi unabii wa Biblia ulivyokuwa sahihi na jinsi ulivyopatana kabisa