Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

What Others Have Said

What Others Have Said

Ufaransa “Mashahidi wa Yehova ni raia wanaoheshimu sheria za Jamhuri. . . . Wao si tisho kwa jamii. Wanafanya kazi, wanalipa ushuru, wanachangia kuboresha hali ya kiuchumi ya nchi yetu na kuwasaidia wenye uhitaji. Inavutia kuona watu wa rangi na malezi mbalimbali, wakikutana pamoja kwa amani. . . . Ikiwa kila mtu angekuwa Shahidi wa Yehova, sisi polisi hatungekuwa na kazi ya kufanya.”—Msemaji wa polisi wa Ufaransa.

Ukrainia “Mashahidi wa Yehova huwafunza watoto wao kanuni bora za maadili zilizo katika Biblia. Wanawafundisha watoto wao kuepuka tabia, matendo, na mitazamo ambayo leo imekubalika katika ulimwengu ingawa inaweza kuwadhuru wao au watu wengine. Kwa hiyo, wao huwaonya watoto wao kuhusu madhara ya kutumia dawa za kulevya, kuvuta sigara, na matumizi mabaya ya kileo. Wanatambua umuhimu wa kuwa waaminifu na kufanya kazi kwa bidii. . . . Mashahidi wa Yehova huwafunza watoto wao sifa nzuri za maadili, kuheshimu mamlaka, kuheshimu watu wengine na mali zao na kutii sheria za nchi.”—Kitabu The History of Religion in Ukraine, kilichohaririwa na Profesa Petro Yarotskyi.

Italia “Watu 30,000 wamekaa kimya katika Uwanja wa Michezo wa Olympic . . . Hakuna takataka zinazotupwa ovyoovyo, hakuna kelele. Hivyo ndivyo hali ilivyokuwa jana katika Uwanja wa Michezo wa Olympic . . . Hakuna mtu anayetoa ishara za matusi, hakuna sigara au hata mikebe [ya vinywaji] iliyotupwa ovyoovyo. Watu walikuwa wamefungua Biblia, wakinukuu mambo makuu, na watoto wakiwa wamekaa kimya.”—Gazeti L’Unità, likiripoti kuhusu kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Rome.

“Mashahidi wa Yehova huwafunza watoto wao sifa nzuri za maadili . . . na kutii sheria za nchi”

Uingereza “Shemasi Mkuu wa Cheltenham alisema kwamba [Kanisa Anglikana] linahitaji vikundi vya watu waliojitolea kwenda nyumba kwa nyumba kama vile Mashahidi wa Yehova wanavyofanya.”—The Gazette, Dayosisi ya Gloucester.

Uholanzi Majirani wanaoishi karibu na Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililo katika jiji la Leeuwarden waliwapa Mashahidi hao barua iliyosema hivi: “Tungependa kuwapongeza kwa sababu ya kuhakikisha kwamba [Barabara ya Noorder] Noorderweg inapendeza. Washiriki wenu huwa wamevalia vizuri sikuzote, nao huwa na tabia nzuri sana. Watoto wenu hujiendesha vizuri, nao watu wazima huegesha magari yao vizuri, hawatupi takataka ovyoovyo, na eneo la Jumba la Ufalme huwa safi kila wakati. Tunatumaini kuwa mtaendelea kuwa majirani wetu kwa muda mrefu, kwa sababu tunafurahi kuwa nanyi.”

Mexico Elio Masferrer, profesa na mtafiti katika Taasisi ya Kitaifa ya Elimu ya Wanadamu na Historia, alisema kuwa Mashahidi huwasaidia watu ambao “wamepatwa na matatizo makubwa ya familia kama vile kubakwa, kutendewa vibaya na familia, uraibu wa kileo na dawa za kulevya.” Pia, alisema kwamba mafunzo ambayo Mashahidi hutoa “huwafanya watu ambao hujihisi hawana thamani wajiheshimu” na kuwawezesha “kuishi bila matatizo makubwa kwa kufanya mambo ambayo yanampendeza Mungu.”—Gazeti Excélsior.

Brazili Gazeti moja liliripoti hivi: “Mashahidi wa Yehova hufanya mambo kwa njia inayopendeza sana. Mahali wanapokutania huwa safi kila mara. Kila kitu huwa kimepangwa vizuri . . . Wanapomaliza shughuli zao, wao huacha mahali hapo pakiwa safi kuliko palivyokuwa. Hotuba zinapoendelea mahali hapo huwa kimya. Hawasukumani wala kugongana. Wao huwa na tabia nzuri wakati wote. . . . Kwa kweli hii ni dini yenye utaratibu. Wanajua jinsi Mungu anavyopaswa kuabudiwa.”Gazeti Comércio da Franca.

Mashahidi wa Yehova wanaamini kuwa Muumba ndiye anayejua kanuni ambazo wanadamu wanapaswa kuishi kulingana nazo. (Isaya 48:17, 18) Kwa hiyo, wanaposifiwa na wengine kwa sababu ya mwenendo wao, wanamwelekezea yeye sifa yote. Yesu alisema hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:16.