Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Huenda Wimbo Tu Ukatosha”

“Huenda Wimbo Tu Ukatosha”

“Huenda Wimbo Tu Ukatosha”

Juliana alikuwa Mkristo mpendwa mkongwe nchini Filipino ambaye aliugua ugonjwa wa Alzheimer. Hata hangeweza kuwatambua watoto wake mwenyewe. Hata hivyo, kila mara nilipokuwa kwenye eneo hilo nilimtembelea Juliana.

Juliana hangeweza kutoka kitandani na angetazama tu nje ya dirisha. Ilikuwa vigumu kuwa pamoja naye kwani hakunikumbuka. Alinikodolea macho bila kuonyesha hisia wala kunitambua. “Je, bado wewe hufikiria kumhusu Yehova?” nilimuuliza. Nilimweleza kuhusu jambo moja lililoonwa katika utumishi wa shambani na nikamwuliza maswali zaidi, lakini bado ni kama hakuelewa lolote. Kisha nikaanza kuimba wimbo fulani. Kilichofuatia kilinigusa moyo sana!

Juliana aligeuza kichwa chake, akaniangalia, na kuanza kuimba pamoja nami! Baada ya muda niliacha kuimba kwa sababu sikukumbuka maneno yote katika Kitagalogi. Lakini Juliana aliendelea kuimba. Alikumbuka beti zote tatu. Nikamuuliza mwenzangu ikiwa angeomba kitabu cha nyimbo kutoka kwa Shahidi mmoja aliyeishi hapo karibu. Alirudi akiwa nacho mara moja. Ingawa sikujua namba ya wimbo huo nilifaulu kufungua ukurasa wenyewe. Basi tukaimba wimbo wote pamoja! Nilipomwuliza Juliana ikiwa alikumbuka nyimbo nyingine, alianza kuimba wimbo fulani wa mapenzi wa Kifilipino.

“Hapana Juliana, sio wimbo kutoka kwenye redio lakini wimbo unaoimbwa kwenye Jumba la Ufalme.” * Kisha nikaanza kuimba wimbo mwingine kwenye kitabu chetu cha nyimbo, naye akaanza kuimba pamoja nami. Macho yake yaling’aa kwa furaha. Yale macho makavu yalibadilika na alitabasamu kwa furaha.

Majirani walianza kutoka nje ili waone ni nani waliokuwa wakiimba. Walisimama dirishani wakitutazama na kutusikiliza. Ilipendeza sana kuona jinsi muziki ulivyougusa moyo wa Juliana! Ulimsaidia kukumbuka maneno ya wimbo.

Kisa hicho kilinifunza kwamba huwezi kujua nini kitakachomgusa mtu ambaye hawawezi kuelewa au kuwasiliana vizuri. Huenda wimbo tu ukatosha.

Muda mfupi tu baada ya kisa hicho, Juliana alikufa. Nilikumbuka kisa hicho nilipokuwa nikisikiliza muziki mpya wenye kusisimua uliorekodiwa na Mashahidi wa Yehova na kutolewa mwaka wa 2009. Unaweza kuwauliza jinsi unavyoweza kupata rekodi hizo maridadi na zenye kusisimua.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Jina la mahali ambapo Mashahidi wa Yehova hukutanika.