Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Baraka Kubwa Zaidi Kuliko Utajiri (Machi 2009) Habari hiyo ilimnukuu Kostas, ambaye alisema hivi: “Mungu hataki tufuatilie sana mali.” Nilifikiri kwamba Yehova haweki mipaka ya mali ambazo watumishi wake wanaweza kuwa nazo mradi mtu anamweka Yehova kwanza. Je, ni vibaya kutafuta mali huku ukimtumikia Yehova kwa uaminifu?

J. D., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Biblia haishutumu utajiri. Kwa kweli, watumishi wengi wa Mungu wa zamani walikuwa matajiri. (Mwanzo 25:5; 26:12-16; Ayubu 1:1-3) Hata hivyo, wale ambao ni matajiri wanapaswa kukumbuka kwamba ‘kujionyesha mali yao maishani hakutokani na Baba, bali kunatokana na ulimwengu.’ (1 Yohana 2:16) Isitoshe, mtume Paulo alisema: “Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Alisema kwamba kudhabihu mambo ya kiroho kwa sababu ya kutamani utajiri, kumewafanya ‘wengine wapotoshwe kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.’ (1 Timotheo 6:10) Bila shaka, Neno la Mungu halionyeshi kwamba matajiri wanapaswa kujihisi wakiwa na hatia kwa sababu wana vitu vingi kuliko wengine. Wakristo wanatiwa moyo “wawe wakarimu, tayari kushiriki,” haidhuru wana vitu vichache au vingi.—1 Timotheo 6:18.

Sauti Isiyosikika Inayosema Mengi (Oktoba 2008) Nilitiwa moyo sana na habari hiyo kumhusu Hillary, ambaye ana ugonjwa wa Rett. Mjukuu wangu mwenye umri wa miaka mitano hawezi kuona, kusikia, kutembea, kuzungumza, au kuketi. Sasa ninatumaini kwamba ninapoimba, kusoma, kuzungumza, na kumkanda, ubongo wake unatambua hilo. Nililia niliposoma maneno haya ya mamake Hillary: “Ingawa siwezi kusikia anachosema, Yehova anaweza kusikia.” Yalinisaidia kutambua kwamba ingawa mjukuu wangu hawezi kusema chochote, Yehova anaweza kuisikia sauti inayotoka moyoni mwake.

M. A., Japani

Binti yangu ana umri wa miaka 43, hata hivyo, hiyo ndiyo iliyokuwa habari ya kwanza kunisaidia nielewe vizuri hali yake na sababu za ulemavu wake. Ninamsikitia Hillary, mama yake, na dada yake. Ingawa wanaishi maelfu ya kilomita mbali na mimi, ninaelewa hali yao, na ninathamini sana mfano wao wa imani, upendo, na uvumilivu.

T. Y., Ghana

Kutoa Mimba—Si Suluhisho Lisilo na Madhara (Juni 2009) Asanteni kwa mfululizo wa habari kuhusu kutoa mimba. Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, niliamua kutoa mimba, jambo ambalo nimejutia sana. Ikiwa singekuwa ninaijua kweli sasa, ningejihisi nikiwa sina tumaini. Ninashukuru sana kwamba nina tumaini na ninajua kwamba Yehova husamehe.

Jina limebanwa, Marekani

Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kukabilianaje na Kifo cha Mzazi? (Agosti 2009) Nina umri wa miaka 22 tu na kifo cha baba yangu kilikuja ghafula na bila kutazamiwa hivi kwamba nilihuzunika kabisa. Kama habari hiyo ilivyoonyesha, nitakosa kushiriki pamoja naye mambo muhimu zaidi maishani mwangu. Baada ya miaka mitatu, bado ni vigumu kwangu kuishi maisha ya kawaida. Licha ya hayo, habari hiyo ilinifariji sana. Mapendekezo yaliyotolewa ya kutusaidia kukabiliana na hali hiyo yamenisaidia sana, ingawa ni vigumu kuyafuata. Asanteni sana kwa kazi nzuri mnayofanya.

N. P., Ufaransa