Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niliingia Kwenye Shindano Bora Zaidi Maishani

Niliingia Kwenye Shindano Bora Zaidi Maishani

Niliingia Kwenye Shindano Bora Zaidi Maishani

Limesimuliwa na Karl-erik Bergman

Nilihisi vizuri sana nilipokimbia kwa kasi. Kwa kuwa nilikuwa na kipawa cha kukimbia, niliamua kufanya mbio ziwe jambo muhimu zaidi maishani mwangu.

NILIJIUNGA na kilabu cha michezo katika mwaka wa 1972, nikiwa na umri wa miaka 17. Muda mfupi baadaye niligundua kwamba ili niweze kuwa mwanariadha mashuhuri nilipaswa kujitahidi sana. Haitoshi kuwa na kipawa tu ili kufaulu kuwa bingwa wa mbio fupi. Lakini niliazimia kujitahidi.

Nilipokuwa na umri wa miaka 22, nilijiunga na timu ya taifa ya Finland. Mwaka uliofuata niliweka wakati bora zaidi katika mbio fupi za mita 100 kuliko mwanariadha yeyote wa Finland. Hata hivyo, majeraha ya kano kwenye shavu langu la mguu na misuli iliyo nyuma ya paja, yalifanya nisiendelee. Lakini kwa sababu nilipenda sana riadha, niliamua kuwazoeza wanariadha wengine waliokuwa na vipawa. Mnamo 1982, nilifanya mipango kwenda kwenye chuo kikuu kimoja huko California, Marekani, na nikiwa katika eneo hilo lenye hali nzuri ya hewa, ningeweza pia kufuatia kazi ya michezo. Hata nilinunua tiketi ya ndege.

Kilichobadili Maisha Yangu

Jioni moja kabla ya kusafiri kuelekea California, nilisikia kengele ya mlango wangu. Nilipofungua mlango niliwaona wanawake wawili waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Walionekana wakiwa watulivu sana, sifa muhimu sana kwa mwanariadha. Niliwakaribisha ndani, na tuliketi na kuzungumza. Baada ya mazungumzo yenye kuelimisha, waliniachia kitabu kinachoitwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. * Nilianza kukisoma. Nilipofika katikati, nilitambua kwamba yale niliyosoma yalikuwa kweli. Wanawake hao waliporudi, niliwauliza kile nilichopaswa kufanya ili niwe Shahidi wa Yehova. Waliniambia kwamba nilipaswa kujifunza Biblia.

Nilikubali kujifunza Biblia na pia nikaanza kuhudhuria mikutano pamoja na Mashahidi katika Jumba la Ufalme huko Vantaa nilikoishi. Niligundua kwamba yale waliyokuwa wakifundisha yalitegemea Biblia. Hata kweli za Biblia nilizokuwa nikijifunza zilianza kubadili maoni yangu polepole kuhusu kile kilicho muhimu maishani. Kwa hiyo, nilienda kwenye ofisi ya kuuza tiketi za ndege na kuomba nirudishiwe pesa za ile tiketi yangu. Nilitumia kiasi fulani cha pesa hizo kununua suti ya kutumia mikutanoni na mfuko wa kubebea Biblia na vichapo vya Biblia. Mnamo 1983, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika kusanyiko huko Helsinki.

Wanariadha Wengine Wanajiunga Nami

Kadiri nilivyojifunza kweli za Biblia, ndivyo nilivyowaeleza rafiki zangu kuzihusu. Lakini walishangazwa kwamba nilipendezwa na Biblia. Hata fununu zilianza kusambaa kwamba nilikuwa nimerukwa na akili. Mmoja baada ya mwingine, rafiki zangu walianza kujitenga nami. Baada ya kubatizwa, nilikuwa nikikutana na wanariadha wenzangu kwenye uwanja wa mazoezi, kwa kuwa bado nilifanya mazoezi kwa ukawaida ili nidumishe afya nzuri. Mazungumzo yetu yaliwasaidia kuona kwamba ingawa nilikuwa nimebadili maisha yangu, sikuwa nimerukwa na akili.

Baada ya muda, baadhi ya wanariadha hao walielewa kwamba yale niliyokuwa nikiwaambia yalipatana na akili na walipaswa kuyafikiria. Pia, walitambua kwamba sikuwa mjeuri wala sikutumia lugha chafu. Wachache kati yao walikuwa tayari kujifunza Biblia. Nilifurahia kuwaonyesha kwamba Biblia ililinganisha maisha ya Mkristo na shindano la riadha. Tuko kwenye shindano la mbio za kupata zawadi ya uzima wa milele.2 Timotheo 2:5; 4:7, 8.

Ukweli wa mambo ni kwamba kusudi halisi na furaha maishani inapatikana, si kwa kushinda mashindano ya mbio, bali kwa kufanya mapenzi ya Muumba wetu. Mazungumzo hayo yaliwafanya wanariadha fulani wachunguze tena miradi yao, na baadhi yao wakakubali kweli za Biblia zilizokuwa zimebadili maisha yangu. Kwa furaha, wengi wao wamemtumikia Mungu kwa bidii ileile waliyokuwa nayo walipokuwa wanariadha.

Mmoja wao aliitwa Yvonne, aliyekuwa bingwa wa mbio za mita 800. Alikuwa ndiye mwanariadha wa kike mwenye kasi zaidi katika mbio za mita 800 katika nchi za Skandinavia na alishikilia rekodi ya kitaifa ya Finland. Alishinda mbio nyingi akiwakilisha Finland katika michezo ya riadha ya Ulaya. Baada ya kuzungumza naye, Yvonne alianza kuona ubatili wa kufuatia umaarufu katika ulimwengu huu. Alijifunza kile ambacho Biblia inafundisha, kwamba ulimwengu huu unapitilia mbali na mwingine mpya utakuja chini ya utawala wa Mungu.—1 Yohana 2:17.

Punde si punde, Yvonne alikubali kujifunza Biblia. Wakati huo, alikuwa akichumbiana na Jouko, aliyekuwa mwanariadha mwenye kipawa wa timu ya taifa ya Finland. Alikuwa tayari ameiwakilisha Finland kwenye mashindano ya riadha ya Ulaya na pia ya ulimwenguni. Baada ya muda, Yvonne na Jouko walihamia Marekani ili wajiendeleze katika riadha.

Walipokuwa huko, Yvonne aliendelea kujifunza Biblia, na Jouko pia alijiunga naye. Jouko alianza kujifunza akiwa na lengo la kutafuta jambo baya ili amfanye Yvonne aache kujifunza. Lakini pole kwa pole, kweli za Biblia zilizama katika moyo wa Jouko. Yvonne na Jouko walioana na baadaye wakajiweka wakfu kwa Mungu, na kubatizwa. Leo, wote wawili wanatumika wakiwa mapainia, yaani, wahubiri wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

Pia, nilianzisha funzo la Biblia na Barbro, aliyekuwa bingwa wa mbio za wanawake za mita 400. Alikuwa ametoka tu kuiwakilisha Finland katika mashindano ya riadha ya Ulaya. Baadaye, Barbro pamoja na mume wake, Jarmo, aliyekuwa akishiriki katika shindano la kuruka kwa kutumia ufito, walihamia Sweden. Wakiwa huko Barbro aliendelea na funzo lake la Biblia, na Jarmo pia akajiunga naye. Wote wawili walikuwa wakitafuta kusudi la maisha, na baada ya kujifunza kweli za Biblia, walibatizwa huko Sweden. Baadaye, Jarmo akawa mtaalamu wa kutibu viungo, na wote pamoja wamekuwa na bidii katika utumishi. Jarmo anatumika akiwa mzee katika kutaniko la Kikristo.

Kisha, kulikuwa na Heidi, mwanariadha kijana mwenye kipawa. Nilipokuwa nikimzoeza, nilitambua kwamba alipendezwa na mambo ya kiroho. Kwa hiyo, siku moja nilizungumza naye juu ya kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka zitakazoletwa na Ufalme huo hapa duniani. Nilimuuliza, “Je, unafikiri tunaweza kufurahia baraka hizi zilizoahidiwa?”—Zaburi 37:11, 29; Mathayo 6:9, 10.

“Ndiyo,” alijibu. Alitaka kujifunza Biblia. Kwa hiyo, nilipanga kwamba dada mmoja Mkristo ajifunze naye. Baada ya miaka michache, Heidi pia alijiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. Baadaye, alikomaa na kuwa mwanamke mrembo anayependa mambo ya kiroho na hivyo tukaoana. Heidi amekuwa mwandamani bora sana, amedumisha azimio lake la kumtumikia Mungu. Kama angeazimia kufuatia michezo angekuwa mwanariadha mashuhuri sana.

Ndugu yangu mdogo Peter, ambaye pia alijihusisha na michezo, hakufurahishwa kabisa nilipoanza kujifunza Biblia. Kisha nilimpa nakala ya kitabu Kuishi Milele. Baadaye alinieleza hivi: “Nimeanza kusoma kitabu hiki lakini sielewi kila kitu. Unaweza kunisaidia?” Nilipanga Shahidi mwingine ajifunze naye, na baada ya kujifunza kwa miezi minne, alibatizwa. Baadaye alifunga ndoa na sasa mke wake anatumika akiwa painia.

Shindano Bado Linaendelea

Hata kabla ya kubatizwa, nilikuwa nimejiwekea mradi wa kutumika nikiwa mmishonari. Muda mfupi baada ya kubatizwa, nilianza kutumika nikiwa painia. Nilifahamu kwamba unapokuwa kwenye shindano la uzima, lazima ujikaze kisabuni. Mimi na mke wangu, Heidi, tulituma maombi ya kuhudhuria Gileadi, ambayo ni shule ya umishonari ya Mashahidi wa Yehova huko New York, Marekani, na mwaka wa 1994 tulialikwa kuhudhuria. Baada ya kuhitimu tulipata mgawo wa kutumika huko Latvia, ambako watu wanazungumza sana Kirusi.

Muungano wa Sovieti ulipovunjika, watu walikatishwa tamaa. Biblia ilikuwa imedharauliwa na hata kupigwa marufuku, lakini tuligundua kwamba watu wengi walitamani sana kusikiliza ujumbe wake. Jambo gumu zaidi ambalo nimewahi kufanya ni kujifunza Kirusi. Lakini baada ya kutumika nikiwa mmishonari kwa miaka sita huko Latvia, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi anayesafiri ili niyatembelee na kuyatia moyo makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Bado ninaendelea kufanya kazi hiyo, nikiandamana na mke wangu mwaminifu.

Kwa miaka kadhaa sasa, nimewazoeza watu wengi katika shindano la kupata uzima, “uzima ulio wa kweli” katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Ili kuzoeza wanariadha wawe stadi kabisa, unahitaji kuwaelewa vizuri. Lazima mwalimu wao awasaidie kutokeza kabisa sifa zao nzuri na kushinda udhaifu wao. Anahitaji kuwachochea waendelee hadi wafikie uwezo wao kamili.

Nimeshangazwa sana kuona jinsi maisha ya Mkristo yanavyofanana sana na ya mwanariadha, kama mtume Paulo alivyokazia katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Mwanariadha mwenye mafanikio anakazia fikira kufanya mazoezi ya kimwili na hawazii tu ushindi. Yeye hujiwekea miradi halisi anayoweza kutimiza na huyafanyia kazi hadi anapoyatimiza. Anapoacha kukazia fikira lengo lake kuu na kuacha kulifanyia kazi, juhudi zake zote huambulia patupu. Vivyo hivyo, Mkristo wa kweli pia anapaswa kukaza fikira.

Pia mwanariadha mwenye mafanikio anahakikisha kwamba anakula chakula kilicho na lishe kwa ukawaida. Hali hiyo ni sawa na ile ya Mkristo wa kweli. Hali mafundisho yasiyo na maadili, chakula kutoka kwenye “meza ya roho waovu,” kama vile mtume Paulo alivyosema. Badala yake, yeye hula chakula bora zaidi cha kiroho kinachoandaliwa na Mungu kupitia Neno lake, Biblia. (1 Wakorintho 10:21) Zaidi ya hilo, matatizo yanapotokea, mwanariadha mwenye mafanikio hudumisha maoni yanayofaa. Yeye hukubali makosa yake na kufanya marekebisho. “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika,” Paulo aliandika. “Lakini naupigapiga mwili wangu,” akasema, ili asikataliwe.—1 Wakorintho 9:24-27.

Mimi pamoja na mke wangu hudumisha afya nzuri ya kimwili kwa kufanya mazoezi kwa ukawaida. Lakini, haturuhusu hilo lituzuie kumtumikia Yehova, aliyewaumba wanadamu kwa njia ya ajabu. (Zaburi 139:14) Pamoja tunakazia macho zawadi ya “uzima ulio wa kweli”—“ule utakaokuja” katika ulimwengu mpya wa Mungu.—1 Timotheo 4:8.

Baada ya kueleza kuhusu ‘wingu la mashahidi’ walioishi kabla ya nyakati za Ukristo, mtume Paulo alihimiza hivi: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 12:1) Hakuna jambo lingine lililo bora zaidi ya hilo, yaani, kukimbia shindano hilo kwa kuwa wote wanaoshiriki watapata baraka za milele.—2 Timotheo 4:7, 8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Katika miaka ya 1980, mimi na Heidi pamoja na Yvonne aliye nyuma na Jouko na binti yao mbele

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Heidi katika utumishi leo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la 2009 huko Helsinki. Yvonne na Jouko wakiwa upande wetu wa kushoto na Jarmo na Barbro wakiwa upande wetu wa kulia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 12]

Published in Aamulehti 8/21/1979