Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini ili Niache Kuhuzunika?

Ninaweza Kufanya Nini ili Niache Kuhuzunika?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kufanya Nini ili Niache Kuhuzunika?

“Kila wakati rafiki zangu wanapokuwa na matatizo, mimi huwasaidia kuyatatua na kuwafanya wajihisi vizuri. Lakini baada ya hapo—ingawa watu wengi hawafahamu hili—mimi hurudi nyumbani, na kuingia chumbani mwangu na kuanza kulia.”—Kellie. *

“Ninapokuwa na huzuni, mimi hujitenga na wengine. Ninapoalikwa mahali fulani, mimi hutafuta udhuru wa kutoenda. Mimi huficha huzuni yangu hivi kwamba hata watu wa familia yangu hawawezi kujua nimehuzunika. Wao hufikiri niko sawa kabisa.”—Rick.

JE, UMEWAHI kuwa na maoni kama hayo ya Kellie au Rick? Ikiwa ndivyo, usikate kauli mara moja kwamba una tatizo fulani. Ukweli ni kwamba kila mtu huhuzunika mara kwa mara. Hata wanaume na wanawake waaminifu katika Biblia walihuzunika pia.

Nyakati nyingine, huenda ukajua sababu inayokufanya uhuzunike lakini huenda nyakati nyingine usijue. Anna mwenye umri wa miaka 19 anasema: “Si lazima uwe katika hali mbaya ili uhuzunike. Unaweza kuwa na huzuni wakati wowote, hata ikiwa huna matatizo maishani. Hilo linashangaza, lakini hutukia!”

Hata sababu iwe nini—au hata ikiwa hakuna sababu yoyote—unaweza kufanya nini unapolemewa na huzuni?

Dokezo la 1: Zungumza kuhusu hali yako. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Kellie: “Baada ya kuongea na mtu kuhusu tatizo langu, mimi huhisi nimetulia sana. Hatimaye, kuna mtu anayeelewa kile ninachopitia. Ninajua kwamba anaweza kuniokoa—atanisaidia nikabiliane na huzuni yangu!”

Pendekezo: Andika hapa chini, jina la “rafiki wa kweli” unayeweza kuzungumza naye unapolemewa na huzuni.

․․․․․

Dokezo la 2: Andika kuhusu hisia zako. Unapokuwa na huzuni nyingi, huenda ikawa vizuri kuandika mawazo yako. Nyakati nyingine Daudi alieleza huzuni yake kubwa katika zaburi alizoandika kwa kuongozwa na roho ya Mungu. (Zaburi 6:6) Kuandika kuhusu hisia zako kutakusaidia ‘ulinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.’—Methali 3:21.

Heather: “Kuandika hunisaidia kupanga mawazo yangu mengi yanayosababishwa na huzuni. Unapofaulu kueleza hisia zako na kupanga mawazo yako, huzuni haitakulemea.”

Pendekezo: Watu fulani wameamua kuandika mambo wanayofanya kila siku. Ikiwa utafanya hivyo, unaweza kuandika mambo gani? Unapohuzunika, eleza jinsi unavyohisi na kile unachowazia kuwa kisababishi cha huzuni yako. Mwezi mmoja baadaye, soma yale uliyoandika. Je, hisia zako kuhusu jambo hilo zimebadilika? Ikiwa ndivyo, andika kile kilichokusaidia kukabiliana na hali hiyo.

Dokezo la 3: Sali kuhusu tatizo lako. Biblia inasema kwamba unaposali kuhusu mahangaiko yako, ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:7.

Esther: “Nilijaribu sana kuelewa sababu iliyonifanya nihuzunike, lakini sikufua dafu. Nilimwomba Yehova anisaidie niwe mwenye furaha. Kuhuzunika bila sababu yoyote kulinichosha sana. Hatimaye nilifaulu kukabiliana na tatizo hilo. Usifikiri kamwe kwamba sala haina nguvu!”

Pendekezo: Tumia Zaburi 139:23, 24 kama kielelezo cha sala yako mwenyewe kwa Yehova. Mweleze Yehova hisia zako zote za ndani kabisa, na umwombe akusaidie kutambua chanzo cha huzuni yako.

Mbali na mapendekezo yaliyotajwa hapo juu, Neno la Mungu ni chanzo kingine kilicho na thamani sana cha msaada. (Zaburi 119:105) Kujaza akili yako mawazo yenye kujenga yanayopatikana katika masimulizi ya Biblia kunaweza kuathiri mawazo, hisia, na matendo yako kwa njia inayofaa. (Zaburi 1:1-3) Masimulizi yenye kusisimua na kufurahisha yanapatikana katika kitabu cha Biblia cha Matendo. Mapendekezo zaidi ya usomaji wa Biblia wenye kujenga yanapatikana kwenye sehemu tisa zenye kichwa “Mfano wa Kuigwa” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kati ya masimulizi ya Biblia yanayozungumziwa katika kurasa hizo ni yale ya Yosefu, Hezekia, Lidia, na Daudi. Kwenye ukurasa wa 227, utaona jinsi mtume Paulo alivyokabiliana kwa mafanikio na hisia zisizofaa alizokuwa nazo kwa sababu ya kutokamilika kwake.

Lakini namna gani ikiwa bado unahuzunika licha ya jitihada zako?

Unapoendelea Kuwa na Huzuni

Ryan anasema, “Nyakati nyingine ninapoamka asubuhi, mimi huhisi ni afadhali nibaki kitandani tu badala ya kuamka na kushinda siku nzima nikiwa na huzuni.” Ryan anaugua ugonjwa wa kushuka moyo sana na kuna watu wengi kama yeye. Uchunguzi unaonyesha kwamba kijana 1 kati ya vijana 4 huugua aina fulani ya ugonjwa wa kushuka moyo sana kabla ya kuwa mtu mzima.

Unaweza kutambua jinsi gani ikiwa umeshuka moyo? Baadhi ya dalili zinatia ndani kubadilika sana kwa hisia na tabia, kujitenga na wengine, kutopendezwa na utendaji wa aina nyingi, badiliko katika mazoea ya kula na kulala, kujihisi kuwa hufai au kujihisi kuwa una hatia bila msingi wowote.

Kwa kweli, wakati mmoja au mwingine karibu kila mtu hupatwa na moja au zaidi ya dalili hizo. Lakini ikiwa dalili zitaendelea kwa zaidi ya majuma kadhaa, waombe wazazi ikiwa unaweza kumwona daktari. Daktari anaweza kukusaidia kujua ikiwa huzuni yako inasababishwa na tatizo fulani la afya. *

Hakuna sababu ya kuaibika ikiwa unaugua ugonjwa wa kushuka moyo sana. Baada ya kupata matibabu, wengi waliokuwa na tatizo hilo wamepata nafuu na kujihisi vizuri zaidi kuliko walivyohisi kwa muda mrefu! Hivyo, iwe huzuni yako imesababishwa na kushuka moyo au la, kumbuka maneno yenye kutia moyo ya Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 23 Huzuni inapoendelea kwa muda mrefu, vijana fulani hufikiria kujiua. Ikiwa umehisi hivyo, zungumza mara moja na mtu mzima unayemwamini.—Ona gazeti Amkeni! la Mei (Mwezi wa 5) 2008, ukurasa wa 26-28.

MAMBO YA KUFIKIRIA

Je, kuna faida za kulia?

“Si kawaida yangu kulia, lakini nimelazimika kufanya hivyo ninapohuzunika. Kulia hunifanya nirudie hali yangu ya kawaida tena. Kisha ninaanza kufikiri kwa njia inayofaa na ninaweza kuwa na tumaini la kuwa na furaha wakati ujao.”—Leanne.

Watu wengine wanaweza kukusaidia jinsi gani ukabiliane na huzuni?

“Ninapohuzunika, mimi huepuka kujitenga. Kwa kweli, huenda nikahitaji kuwa peke yangu ili nichanganue hisia zangu na hata labda niweze kulia. Lakini baada ya hapo, ninajua kwamba ninahitaji kuchangamana na watu ili niache kufikiri kuhusu jambo lililonihuzunisha.”—Christine.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Mara nyingi mimi huhuzunika ninapofikiria sana kujihusu. Ninapowasaidia wengine, mimi huacha kujifikiria na hivyo ninakuwa tena furaha.”

“Ninapodumisha ratiba nzuri ya kufanya mazoezi, sihuzuniki mara nyingi kwa sababu mazoezi hunifanya nijihisi vizuri. Baada ya kufanya mazoezi, ninakuwa nimechoka hivi kwamba sijishughulishi na huzuni!”

[Picha]

Drenelle

Rebekah

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ukipata msaada na unapotia bidii, unaweza kutoka kwenye shimo la huzuni