Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suluhisho la Upweke

Suluhisho la Upweke

Suluhisho la Upweke

IKIWA wewe ni mpweke, ingefaa ujiulize: ‘Je, kuna mambo ninayoweza kufanya ili kuboresha hali yangu? Je, huenda ninahitaji kufanya mabadiliko fulani maishani? Ikiwa ndivyo, nifanye mabadiliko gani?’ Maswali yafuatayo yanaweza kukusaidia kujichunguza na kupata suluhisho linalofaa.

Je, Ninahitaji Kubadili Mtazamo Wangu?

Mtu yeyote anaweza kuwa mpweke. Lakini hali hiyo inaleta matatizo inapoendelea kwa muda mrefu. Inapoendelea kwa muda mrefu, huenda hilo likaonyesha kwamba una mtazamo usiofaa. Huenda tatizo likawa jinsi unavyotenda unapokuwa na watu wengine. Huenda mtu akajiwekea ua wa seng’enge bila kutaka na kuwafanya wengine wasitake kuwa marafiki wake. Nyakati nyingine mtu anahitaji tu kubadili mtazamo wake.

Sabine, aliyehamia Uingereza anasema hivi: “Inachukua muda kwa marafiki wapya kuaminiana na kuzoeana. Mbona usiwaulize wengine kuhusu malezi yao? Niliambiwa hivi: ‘Huwezi kusema kwamba tamaduni fulani ndiyo bora. Jifaidi na mambo mazuri kutoka katika tamaduni zote.’” Kama Sabine alivyotiwa moyo kufanya, unaweza kutafuta sifa nzuri katika tamaduni za wengine ambazo zitakufaidi ukiziiga.

Je, Mimi Hupenda Kuwaepuka Wengine?

Huenda ukajiuliza: ‘Je, mimi hupenda kuwaepuka watu? Je, wanaweza kuwa wenye urafiki zaidi ikiwa nitakuwa mwenye urafiki zaidi?’ Ikiwa unahisi hilo ndilo tatizo, jitahidi kuwa mwenye urafiki zaidi. Roselise, mwenye umri wa miaka 30, kutoka Guadeloupe ambaye alihamia Uingereza alisema, “Watu wanaohisi upweke wana mwelekeo wa kujitenga na wengine.” Hivyo anashauri hivi: “Tafuta watu ambao pia wanaonekana kuwa wapweke. Chukua hatua ya kwanza ya kuzungumza nao. Nyakati nyingine, swali moja tu hutokeza urafiki wenye kudumu.”

Hata hivyo, wakati na jitihada zinahitajika ili kusitawisha urafiki wa karibu. Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwa msikilizaji mzuri. Ukisikiliza kwa makini, utajua mambo yanayompendeza mwenzako. Kumbuka, kuwa na hisia-mwenzi huchangia urafiki!

Je, Nina Maoni Yasiyofaa?

Kujidharau kunaweza kumzuia mtu kuanzisha urafiki. Jiulize, ‘Je, nina mwelekeo wa kuwa na maoni yasiyofaa kujihusu?’ Abigaïl, mwenye umri wa miaka 15 anayeishi Ghana, anasema hivi: “Nyakati nyingine nilikuwa na maoni yasiyofaa ambayo yalinifanya niwe mpweke. Nilijihisi kuwa sifai na hakuna mtu anayenipenda.” Uwe na hakika kwamba ukichukua hatua ya kwanza kuwafikia na kuwasaidia wengine kwa njia fulani, hawatakudharau. Huenda hata wakataka kuwa rafiki zako. Kwa hiyo, mbona usichukue hatua hiyo ya kwanza?

Kuwa na maoni yanayofaa pia kutakusaidia kuanzisha urafiki na watu ambao si wa rika lako. Kuwa na marafiki ambao wamekuzidi umri au wale uliowazidi umri kunathawabisha. Abigaïl alishinda upweke hasa kwa kuwa na marafiki waliomzidi umri. Anaeleza, “Nilifaidika sana kutokana na uzoefu wao.”

Je, Mimi Hujitenga na Wengine?

Watu wengi walio wapweke hujituliza kwa kutazama televisheni au kucheza michezo ya video kwa vipindi virefu, au kutumia kompyuta zao. Lakini wanapozima vifaa hivyo, upweke hurudi. Elsa, mwenye umri wa miaka 21, anayeishi Paris anakubaliana na hilo, anasema, “Televisheni na michezo ya video inaweza kuwa kama dawa ya kulevya ambayo humwathiri mtu hadi afikie hatua ya kutotaka kuwa na marafiki.”

Madhara ya kutazama televisheni ni kwamba watu hawazungumzi, kubadilishana mawazo, au hawapati nafasi ya kusitawisha urafiki. Michezo ya video ina madhara hayohayo—inampeleka mtu kwenye ulimwengu wa kuwaziwa ambao hutoweka punde tu anapoacha kucheza. Kutembelea vituo mbalimbali vya Intaneti bila kusudi lolote kunaweza kumfanya mtu asahau matatizo yake, lakini pia vituo hivyo vinaweza kuonyesha mambo mapotovu kiadili na kufanya ukutane na watu wanaoficha utu wao. Intaneti si mahali pazuri pa kutafuta au kusitawisha urafiki wa kweli.

Je, Ninatafuta Mwenzi wa Ndoa?

Huenda waseja fulani wakataka kufunga ndoa ili tu waepuke kuwa wapweke. Ni kweli kwamba mwenzi mwenye fadhili na upendo anaweza kukufanya uwe na furaha sana maishani, lakini uwe mwangalifu usikimbilie ndoa.

Huenda ndoa isiwe suluhisho kwa tatizo la upweke. Inasemekana kwamba wenzi wa ndoa walio na tatizo la kuwasiliana ni “kati ya watu wapweke zaidi ulimwenguni.” Inasikitisha kwamba watu wengi sana wanakabili hali hiyo. Kwa hiyo, ikiwa ungependa kufunga ndoa siku moja, kwa nini usitatue tatizo hilo la upweke kwanza kabla ya kuanza uchumba? Ukibadili mtazamo wako na mazoea na kuchukua hatua ya kwanza ya kuwa na marafiki ukiwa bado mseja, huenda ukawa unajenga msingi imara wa ndoa yenye furaha.

Unaweza Kukabiliana na Upweke

Huenda tatizo lako la upweke lisitatuliwe mara moja. Lakini unaweza kukabiliana nalo kwa kufuata ile Kanuni Bora ambayo Yesu alitaja. Alisema: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Hivyo, ikiwa unataka wengine wawe wenye urafiki, basi wewe pia unapaswa kuwa mwenye urafiki. Ukitaka wengine wakufunulie yaliyo moyoni, lazima wewe uwafunulie yaliyo moyoni mwako. Huenda wengine wasiitikie mara moja, lakini baada ya muda, wataitikia. Hata wasipoitikia, utakuwa mwenye furaha kwa kuwa ulijitahidi.

Yesu alitaja kweli nyingine ambayo huenda ikakusaidia kukabiliana na upweke: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ukitumia wakati wako kuwasaidia wengine, iwe ni kumsaidia mtoto kufanya kazi za shuleni au kumnunulia mzee vitu dukani au kumfanyia kazi za nyumbani au kumtunzia bustani, utakuwa na furaha zaidi na huenda ukapata rafiki wa kweli.

Jinsi ya Kupata Rafiki Bora

Kuna njia nyingine za kukabiliana na upweke. Usijifungie tu nyumbani. Ikiwezekana, tembea kwenye bustani au sehemu za mashambani. Ukiwa peke yako nyumbani tumia wakati huo kufanya mambo mbalimbali kama vile, kushona, kufanya kazi za nyumbani, kurekebisha vitu, au kusoma. Mtu mmoja aliandika, “Hakuna mfadhaiko ninaopata ambao hauwezi kutulizwa ninaposoma kwa saa moja.” Wengi wamepata kitulizo hasa kwa kusoma zaburi za Biblia.

Wataalamu wanasema kwamba kushirikiana na watu walio na imani moja ya kidini kunaweza kumsaidia mtu kushinda upweke na pia kuna manufaa ya afya. Unaweza kupata wapi watu wanaojitahidi kufuata ile Kanuni Bora? Katika kitabu kuhusu dini mbalimbali, mtazamaji mmoja asiyeunga mkono dini yeyote aliandika hivi: “Katika makutaniko yao, Mashahidi [wa Yehova] wanafanyiza jamii ya watu wenye kutumainiana na kuvumiliana kikweli.”

Yesu alionyesha jambo ambalo lingewatambulisha Wakristo wa kweli alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo huo—kwanza kumwelekea Mungu kisha kuwaelekea waabudu wenzao—ndio huwatambulisha wale wanaofuata dini ya kweli.—Mathayo 22:37-39.

Kusitawisha urafiki pamoja na Mungu ndio njia bora zaidi ya kukabiliana na upweke. Akiwa rafiki yako, huwezi kujihisi mpweke kamwe!—Waroma 8:38, 39; Waebrania 13:5, 6.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

JINSI NINAVYOKABILIANA NA UPWEKE

Anny, mjane: “Mimi hujaribu kudhibiti mawazo yangu na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yangu.”

Carmen, mseja: “Nimejifunza kutokazia fikira mambo yaliyopita bali kusonga mbele na kuanzisha marafiki wapya.”

Fernande, mjane: “Ukijitahidi kuwasaidia wengine, unasahau matatizo yako.”

Jean-Pierre, mseja: “Kwa kawaida mimi hutembea kwa muda mrefu, na wakati huo ninamfungulia Mungu moyo wangu katika sala.”

Bernard, mjane: “Mimi huwasiliana kwa ukawaida na marafiki wangu kwa kuwapigia simu, si ili tukumbuke mambo yenye kuhuzunisha bali nifurahie kuwajulia hali.”

David, mseja: “Ingawa mimi hupenda faragha yangu, nimejitahidi sana kushirikiana na wengine.”

Lorenna, mseja: “Mimi huchukua hatua ya kwanza kuwafikia watu na kuanzisha urafiki.”

Abigaïl, miaka 15: “Mimi hutumia wakati mwingi pamoja na marafiki wanaonizidi umri na ninanufaika sana kutokana na uzoefu wao.”

Cherry, mseja: “Niligundua kwamba ukiwaambia watu kwamba wewe ni mpweke, wanajitahidi sana kuwa marafiki wako.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

NJIA ZA KUSHINDA UPWEKE

Uwe na mtazamo unaofaa

Punguza burudani zinazokutenga na wengine, kama vile kutazama televisheni

Tafuta marafiki walio na viwango kama vyako kutia ndani wale ambao si wa rika lako

Zaidi ya yote, sitawisha urafiki pamoja na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Anzisha urafiki na watu ambao si wa rika lako