Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Yeyote Anayeweza Kuaminiwa?

Je, Kuna Yeyote Anayeweza Kuaminiwa?

Je, Kuna Yeyote Anayeweza Kuaminiwa?

Daktari mmoja alionwa kuwa mwanzilishi wa tiba ya kupunguza maumivu. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka kumi, kuanzia mwaka wa 1996, daktari huyo wa unusukaputi anayeheshimiwa sana alikuwa amejitungia matokeo ya utafiti uliochapishwa katika majarida ya kitiba yanayojulikana sana.

“SIELEWI ni kwa nini mtu anaweza kufanya jambo kama hilo,” anasema Dakt. Steven L. Shafer, katika jarida Anesthesiology News.

Ni nini kinachoweza kumfanya mtaalamu anayeheshimika kuwadanganya wanadamu wenzake? Huenda ikawa mojawapo ya sababu hizi nne.

Pupa. Dakt. Jerome Kassirer, aliyekuwa mhariri wa jarida The New England Journal of Medicine, alieleza hivi katika ripoti iliyochapishwa katika gazeti New York Times: “Watafiti wanapotegemea sana kampuni [za madawa] ili kupata riziki, kuna mwelekeo wa kutoa matokeo yanayopendelea kampuni hizo.”

Kutafuta mafanikio kwa njia yoyote ile. Nchini Ujerumani, inaaminiwa kwamba wanafunzi wa vyuo vikuu wanaojifunza sayansi wamewalipa walimu maelfu ya euro kama rushwa ili kupata cheti cha Doktor, cheo ambacho katika nchi hiyo kinaonyesha kuwa mtu amefanikiwa sana. Uchunguzi uliochapishwa katika gazeti The New York Times ulionyesha kwamba wanafunzi wengi waliochukua njia hiyo ya mkato walisema kwamba “wanakusudia kufuata sheria zilizowekwa” baada ya kupata mafanikio.

Hakuna mifano bora ya kuigwa. Gazeti The New York Times lilimnukuu profesa mmoja aliyesema hivi kuhusu wanafunzi wa shule za sekondari: “Huenda tukasema kwamba hawana viwango vya maadili . . . Lakini huenda ikafaa kusema kwamba walimu na washauri wao na jamii kwa ujumla haijawafundisha kusitawisha viwango vya maadili ambavyo wanapaswa kufuata.”

Matendo ambayo hayapatani na viwango. Katika uchunguzi uliofanyiwa wanafunzi 30,000 hivi wa sekondari, asilimia 98 walisema kwamba wanaamini ni muhimu kuwa wanyoofu katika mahusiano. Hata hivyo, wanafunzi 8 kati ya 10 walikiri kwamba waliwadanganya wazazi wao, na 64 walikiri kwamba waliiba mtihani mwaka uliopita.

Kanuni Bora za Maadili

Kama ilivyotajwa katika sanduku lililo kwenye ukurasa huu, inaonekana kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuaminiana. Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Unaweza kupinga namna gani mwelekeo huo na kukataa ukosefu wa unyoofu ambao umeenea sana leo? Kanuni za Biblia zinazofuata zitakusaidia:

“Usimtungie mwenzako jambo lolote baya, wakati anapokaa nawe na kujiona salama.”—Methali 3:29.

Kumpenda jirani yetu kutatuchochea tutangulize masilahi yake, na tusimtendee kwa hila kwa kuwa anatuamini. Kanuni hiyo inaweza kukomesha matendo mengi yanayochochewa na pupa kama vile kuuza madawa bandia, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa habari hizi.

“Ukweli hudumu milele, lakini uongo ni wa kitambo tu.”—Methali 12:19, “Biblia Habari Njema.”

Wengi leo wanaamini kwamba watu wanyoofu hawawezi kufanikiwa. Lakini hebu jiulize, ‘Ni jambo gani lililo la thamani zaidi—kupata thawabu sasa au kupata faida za muda mrefu, kutia ndani kujiheshimu?’ Mwanafunzi anaweza kuwadanganya wengine kuhusu ujuzi au ustadi wake kwa kuiba mtihani, lakini hali itakuwa namna gani anapoanza kufanya kazi?

“Mwadilifu anatembea kwa utimilifu wake. Wanawe watakuwa na furaha baada yake.”—Methali 20:7.

Ikiwa wewe ni mzazi, wawekee watoto wako mfano mzuri kwa ‘kutembea kwa utimilifu.’ Waeleze jinsi ambavyo umefaidika kwa kuwa mnyoofu. Watoto wanapomwona mzazi akitembea kwa utimilifu, inaelekea watajitahidi kuwa watu wanaoaminika.—Methali 22:6.

Je, kanuni za Biblia zilizotajwa hapo juu zinafanya kazi? Je, kweli leo kuna watu wanaoweza kuaminiwa?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Gazeti Le Figaro, lilisema kwamba Wafaransa wengi “wanaamini kwamba watu mashuhuri—katika siasa, biashara, jamii, na utamaduni—si wanyoofu, na hivyo hawaoni kwa nini wao wanapaswa kuwa wanyoofu.”

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

JE, TULIUMBWA TUAMINIANE?

Majaribio yaliyofanywa na Michael Kosfeld, profesa wa mambo ya biashara katika Chuo Kikuu cha Frankfurt, Ujerumani, yalimfanya akate kauli kwamba kuaminiana ni “sehemu ya utu wa mwanadamu.” Kosfeld aligundua kwamba watu wawili wanapowasiliana, ubongo wa mwanadamu hutokeza homoni inayoitwa oxytocin, ambayo huwachochea waaminiane. “Kwa kweli, hilo ni mojawapo ya mambo ya pekee katika wanadamu,” anasema Kosfeld. “Tunapoacha kuaminiana, tunapoteza sehemu muhimu ya utu wa mwanadamu.”