Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanaoamini Hakuna Mungu Wanatafuta Wafuasi

Watu Wanaoamini Hakuna Mungu Wanatafuta Wafuasi

Watu Wanaoamini Hakuna Mungu Wanatafuta Wafuasi

KUNA kikundi kipya cha watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu. Watu hao wameamua kwamba hawatanyamaza tu. Badala yake, wameamua kufanya kampeni “kwa moyo wote na wakitumia njia yoyote ile kuwashawishi watu wa kidini wakubali maoni yao,” akaandika mwandishi Richard Bernstein. Kikundi hicho kipya hata kinajaribu kuwashawishi watu ambao wanaamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana. Kwa maoni yao, hakuwezi kuwa na Mungu.

Mshindi wa Tuzo la Nobeli, Steven Weinberg alisema hivi: “Ulimwengu unahitaji kuamshwa kutoka kwa jinamizi la mafundisho ya kidini. Sisi wanasayansi tunapaswa kufanya lolote tunaloweza ili kupunguza uvutano wa dini na huenda hilo likawa ndilo jambo bora zaidi ambalo tutakuwa tumetimiza katika jamii.” Mbinu moja ambayo imetumiwa kupunguza uvutano huo ni vitabu, na inaonekana kwamba watu wengi wanavutiwa sana na vitabu hivyo kwa kuwa baadhi ya vitabu vilivyoandikwa na watu wasioamini kuwako kwa Mungu vimeuzwa kwa wingi.

Dini imechangia harakati ya kikundi kipya cha watu wasioamini kwamba kuna Mungu kwa kuwa watu wengi wamechoshwa na dini zenye imani kali, ugaidi, na vita ambavyo vinaikumba ulimwengu. Mtu mmoja anayeunga mkono imani ya kwamba hakuna Mungu anasema: “Dini imetia sumu kila kitu.” Isitoshe, inasemekana kwamba ‘sumu’ hiyo imeingia katika mafundisho ya kawaida ya kidini na si tu katika dini zenye imani kali. Wafuasi wa kikundi hicho kipya wanasema kwamba mafundisho ya msingi ya kidini yanapaswa kufichuliwa, kutupiliwa mbali, na badala yake watu waanze kuamini mambo yanayopatana na akili na yenye uhakika. Watu hawapaswi kuogopa kuzungumza waziwazi kuhusu “upumbavu mwingi” unaopatikana katika Biblia na Kurani, anasema Sam Harris, anayeamini kwamba hakuna Mungu. “Hatuwezi tena kunyamaza ili tu tusiwaudhi wanadini.”

Huku wakishutumu dini, watu hao wanaoamini kwamba hakuna Mungu wanaabudu sayansi, wengine wao hata wakidai kwamba sayansi inathibitisha kwamba hakuna Mungu. Lakini je, kweli inathibitisha hilo? Je, inaweza kuthibitisha hilo? Harris anasema kwamba “baada ya muda kupita, upande mmoja utashinda mjadala huo, na ule mwingine utashindwa kabisa.”

Wewe unafikiri ni upande gani utakaoshinda? Unapofikiria jambo hilo, jiulize: ‘Je, kuna madhara yoyote kuamini kwamba kuna Muumba? Je, ulimwengu ungekuwa bora ikiwa kila mtu angeamini kwamba hakuna Mungu?’ Acheni tuchunguze maoni ya wanasayansi na wanafalsafa maarufu kuhusu dini, sayansi, na imani ya kwamba hakuna Mungu.