Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kujiumiza Kunaweza Kukusaidia Umkaribie Mungu?

Je, Kujiumiza Kunaweza Kukusaidia Umkaribie Mungu?

Maoni ya Biblia

Je, Kujiumiza Kunaweza Kukusaidia Umkaribie Mungu?

WATU wengi huogopa kujiumiza. Hata hivyo, waabudu wengi ambao hujitesa kupitia mazoea kama vile kujipiga mijeledi, kujinyima chakula kwa muda mrefu kupita kiasi, na kuvalia shati za manyoya ambazo hukwaruza ngozi zao na kuwafanya wahisi uchungu wamesifiwa sana kuwa mifano mizuri ya watu wanaomhofu Mungu. Mazoea hayo si mambo ya zamani tu. Kulingana na ripoti za hivi karibuni, hata viongozi mashuhuri wa kidini wamejiumiza kwa kujipiga mijeledi.

Ni nini huwachochea watu kujihusisha katika ibada za aina hiyo? Msemaji mmoja wa shirika linalodai kuwa la Kikristo alisema kwamba “unapojitolea kuteseka kwa njia inayokubalika, unaonyesha kwamba umejiunga na Yesu Kristo pamoja na kuteseka ambako alikubali kwa hiari ili kutuokoa kutokana na dhambi.” Licha ya madai ya viongozi wa kidini, Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo?

Tunza Mwili Wako

Biblia haipendekezi wala haiungi mkono kwamba tumwabudu Mungu kwa kujiumiza. Kwa kweli, Biblia inawatia moyo watu wanaomhofu Mungu watunze miili yao. Hebu ona jinsi Biblia inavyoeleza kuhusu upendo kati ya mume na mke. Ikizungumzia jinsi mtu huutendea mwili wake, Biblia inahimiza hivi: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe . . . Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko.”—Waefeso 5:28, 29.

Je, kweli amri ya mtu kumpenda mkewe kama mwili wake mwenyewe ingekuwa na maana ikiwa waabudu wangetazamiwa kuumiza miili yao wakati wa ibada? Ni wazi kwamba mtu yeyote anayependa kanuni za Kimaandiko anatazamiwa kutunza na hata kuupenda mwili wake, na anapaswa kumpenda mwenzi wake wa ndoa kwa njia hiyo.

Kwa kufaa, Biblia ina kanuni nyingi ambazo husaidia watu wajue jinsi ya kutunza miili yao. Kwa mfano, Biblia inazungumza kuhusu faida za kufanya mazoezi kwa kiasi. (1 Timotheo 4:8) Inaonyesha faida za kitiba zinazopatikana katika vyakula fulani na pia inataja athari za kukosa kula chakula chenye lishe. (Methali 23:20, 21; 1 Timotheo 5:23) Maandiko yanawatia watu moyo wadumishe afya njema kwa sababu kufanya hivyo kutawapa nguvu. (Mhubiri 9:4) Ikiwa wasomaji wa Biblia wanatazamiwa watunze afya yao katika njia hizo, basi kwa kweli wanaweza kutazamiwa pia waumize miili yao?—2 Wakorintho 7:1.

Je, Wakristo Wanapaswa Kuigiza Mateso ya Yesu?

Mashirika fulani bado hukazia fikira kimakosa mateso ambayo Yesu na wafuasi wake wa karne ya kwanza walipitia ili kuwachochea watu wajitese leo. Lakini Biblia haionyeshi kwamba watumishi wa Mungu walijiletea mateso yaliyowapata. Waandikaji wa Biblia waliokuwa Wakristo walipotaja kuhusu mateso ya Kristo, walikuwa wakiwatia moyo Wakristo waendelee kuvumilia mateso, si eti wajiletee mateso. Hivyo, wale ambao wanaumiza miili yao hawamwigi Yesu Kristo.

Kwa mfano: Hebu wazia kwamba unamtazama rafiki yako mpendwa akitukanwa na kuchapwa na umati wa watu wenye hasira. Unaona jinsi anavyovumilia mateso hayo akiwa mtulivu, bila kulipiza kisasi au hata kurudisha matusi. Ikiwa ungependa kumwiga rafiki yako, je, ungeanza kujichapa mwenyewe na kujitusi? La hasha! Kufanya hivyo kungeonyesha kwamba unaiga matendo ya umati ule uliokuwa ukimchapa. Ungeepuka tu kulipiza kisasi unaposhambuliwa.

Basi, ni wazi kwamba wafuasi wa Kristo hawapaswi kujiumiza kama kwamba wanaiga umati wenye hasira kali ambao ulimtesa na hata ukataka kumuua Yesu. (Yohana 5:18; 7:1, 25; 8:40; 11:53) Badala yake, wanapoteswa wanapaswa kuiga jinsi Yesu alivyovumilia mateso kwa njia tulivu na kwa amani.—Yohana 15:20.

Zoea Linalopotosha Maandiko

Hata kabla ya Ukristo, Maandiko ambayo yaliongoza maisha ya Wayahudi pamoja na ibada yao hayakuwaruhusu kuumiza miili yao. Kwa mfano, Sheria iliwakataza kabisa Wayahudi kuikatakata miili yao, zoea ambalo lilikuwa la kawaida katika mataifa ya kale yasiyo ya Kiyahudi. (Mambo ya Walawi 19:28; Kumbukumbu la Torati 14:1) Ikiwa Mungu hakutaka mwili ukatwekatwe, ni wazi kwamba hakutaka pia utiwe makovu kwa mijeledi. Msimamo wa Biblia ni wazi kabisa—kuumiza mwili wako kimakusudi kwa njia yoyote ile hakumpendezi Mungu.

Kama vile tu msanii angependa kazi yake iheshimiwe, Yehova Mungu, ambaye ni Muumba, angependa mwili wa mwanadamu ambao ni uumbaji wake utunzwe. (Zaburi 139:14-16) Kwa kweli, kujiumiza hakuimarishi uhusiano wa mtu pamoja na Mungu. Badala yake, kunazuia uhusiano huo na kupotosha mafundisho ya Injili.

Mtume Paulo, aliyeongozwa na roho, aliandika hivi kuhusu mapokeo kama hayo ya wanadamu yenye kukandamiza: “Kwa kweli, mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima katika namna ya ibada ya kujitwika mwenyewe na unyenyekevu wa kujifanya, kuutendea mwili kwa ukali; lakini hayana thamani yoyote katika kuzuia kuutosheleza mwili.” (Wakolosai 2:20-23) Kwa kweli, zoea la mtu kuumiza mwili wake haliwezi kwa vyovyote vile kumsaidia amkaribie Mungu. Badala yake, matakwa ya kumwabudu Mungu katika njia ya kweli ni yenye kuburudisha, laini, na mepesi.—Mathayo 11:28-30.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Mungu ana maoni gani kuhusu mwili wa mwanadamu?—Zaburi 139:13-16.

● Je, kuutesa mwili wako kunaweza kukusaidia kushinda tamaa zisizofaa?—Wakolosai 2:20-23.

● Je, ibada ya kweli inapaswa kuwa ngumu na yenye kulemea?—Mathayo 11:28-30.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Msimamo wa Biblia ni wazi kabisa—kuumiza mwili wako kimakusudi kwa njia yoyote ile hakumpendezi Mungu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mtu akitembea kwa magoti ili ajitie maumivu anapoelekea kanisani

[Hisani]

© 2010 photolibrary.com