Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu cha Wafia Imani cha Jean Crespin

Kitabu cha Wafia Imani cha Jean Crespin

Kitabu cha Wafia Imani cha Jean Crespin

KATIKA mwaka wa 1546, watu 14 huko Meaux, Ufaransa walipatikana na hatia ya uzushi wa kidini, na wakahukumiwa kuteketezwa wakiwa hai. Walikuwa wamefanya makosa gani? Walikuwa wakikutana katika nyumba za watu binafsi, wakisali, wakiimba nyimbo, wakiadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana, na wakitangaza waziwazi kwamba hawatakubali kamwe “kutumia sanamu ambazo mapapa waliingiza katika kanisa.”

Siku ambayo walipaswa kuteketezwa, mwalimu wa Kanisa Katoliki François Picard aliwauliza wanaume waliokuwa wamehukumiwa waeleze imani yao kuhusu Chakula cha Jioni cha Bwana. Walijibu kwa kumwomba aeleze kuhusu fundisho la Kikatoliki kwamba wakati wa mwadhimisho huo, mkate na divai hugeuka kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Yesu. Wanaume hao waliuliza, ‘Je, mkate huo una ladha ya nyama? Au divai hiyo ina ladha ya damu?’

Wanaume hao 14 hawakujibiwa ingawa walikuwa wametoa hoja yenye nguvu, nao walifungwa kwenye miti na kuteketezwa wakiwa hai. Wale ambao ndimi zao hazikuwa zimekatwa waliimba nyimbo. Makasisi waliokuwa wamezingira mahali pa mauaji hayo walijaribu kuzima sauti zao kwa kuimba nyimbo kwa sauti ya juu zaidi. Siku iliyofuata, Picard akiwa amesimama mahali palepale ambapo mauaji yalikuwa yamefanyika alitangaza kwamba watu hao 14 walikuwa wamehukumiwa kuteseka milele kwenye moto wa mateso.

Katika miaka ya 1500, Ulaya palikuwa mahali hatari sana kwa wapinzani wa kidini. Watu wengi ambao walitilia shaka mafundisho ya kanisa yaliyokuwa yamekubaliwa waliteswa kikatili na wapinzani wao wa kidini. Kitabu kimoja kinachotoa habari kuhusu mateso hayo ni Le Livre des martyrs (Kitabu cha Wafia Imani), kilichoandikwa na Jean Crespin, na kuchapishwa huko Geneva, Uswisi, katika mwaka wa 1554. Pia kinajulikana kama Histoire des martyrs. *

Wakili Ajiunga na Marekebisho Makubwa ya Kidini

Crespin alizaliwa karibu na mwaka wa 1520, katika jiji la Arras ambalo sasa liko kaskazini mwa Ufaransa, na kusomea sheria huko Louvain, Ubelgiji. Huenda ni wakati huo ambapo alipata mawazo kuhusu watu waliokuwa wakitaka kufanya Marekebisho katika Kanisa Katoliki. Katika mwaka wa 1541, Crespin alienda huko Paris kufanya kazi akiwa karani wa mwanasheria mmoja maarufu. Karibu wakati huohuo, alishuhudia Claude Le Painctre akiteketezwa kwa moto huko Place Maubert, Paris, baada ya kuhukumiwa kuwa mzushi. Crespin alipendezwa sana na imani ya kijana huyo aliyekuwa mfuaji wa dhahabu, ambaye aliuawa kwa kile ambacho Crespin alikiita “kuwatangazia ukweli wazazi na rafiki zake.”

Katika kipindi hicho, Crespin alianza kufanya kazi akiwa mwanasheria huko Arras. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, alishtakiwa kuwa mzushi kwa sababu ya imani yake mpya. Ili aepuke kufikishwa mahakamani, alikimbilia Strasbourg, Ufaransa, kisha baadaye akahamia Geneva, Uswisi. Akiwa huko, Crespin alishirikiana na watu waliounga mkono yale Marekebisho Makubwa ya Kidini. Aliacha kufanya kazi ya uanasheria na akaanza kazi ya uchapishaji.

Crespin alichapisha vitabu vya kidini kutoka kwa waandishi kama vile John Calvin, Martin Luther, John Knox, na Theodore Beza. Alichapisha maandishi ya Kigiriki ya sehemu ya Biblia inayojulikana kama Agano Jipya, na pia akachapisha Biblia—ikiwa nzima au sehemu—katika Kifaransa, Kihispania, Kiingereza, Kiitaliano, na Kilatini. Hata hivyo, Crespin alipata umaarufu kwa sababu kitabu chake Book of Martyrs. Ndani yake aliorodhesha watu wengi ambao walikuwa wameuawa kwa sababu ya uzushi kati ya mwaka wa 1415 na 1554.

Sababu ya Kuandika Kuhusu Wafia Imani

Vitabu vingi vilivyochapishwa na wanaharakati wa Marekebisho Makubwa vilishutumu ukatili wa Kanisa Katoliki. Viliwatia watu moyo kwa kuonyesha kuwa wafia imani Waprotestanti walikuwa wakiendeleza “ushujaa” wa kuvumilia mateso kama ule ulioonyeshwa na watumishi wa Mungu wa kale, kutia ndani Wakristo wa karne ya kwanza. Ili kuwe na kielelezo cha kufuatwa na Waprotestanti wengine, Crespin aliandika orodha ya watu ambao walikuwa wameuawa kwa sababu ya imani yao. *

Kitabu cha Crespin kimefanyizwa na rekodi za kesi, uendeshaji wa mashtaka, na masimulizi ya mashahidi, pamoja na ushahidi ulioandikwa na washtakiwa walipokuwa gerezani. Kinatia ndani barua zenye kutia moyo ambazo wafungwa walitumiwa, na baadhi yake zilikuwa na manukuu mengi ya Biblia. Crespin aliamini kwamba imani ya washtakiwa hao “ilihitaji kukumbukwa daima.”

Mafundisho mengi ambayo Crespin aliandika yanahusu mabishano yanayojulikana kati ya Wakatoliki na Waprotestanti. Kwa mfano, watesaji na waliokuwa wakiteswa, walibishana kuhusu mambo kama vile utumizi wa sanamu katika ibada, toharani, sala kwa ajili ya wafu, na vilevile ikiwa dhabihu ya Yesu ilirudiwa kila mara wakati wa Misa ya Katoliki na pia ikiwa papa alikuwa mwakilishi wa Mungu.

Kitabu Book of Martyrs kinaonyesha wazi mizozo na kutovumiliana ambako kulionekana katika nyakati hizo zenye jeuri. Ingawa Crespin alikazia hasa minyanyaso ya Wakatoliki kuelekea Waprotestanti, tunapaswa kukumbuka pia kwamba nyakati nyingine Waprotestanti waliwatesa Wakatoliki kwa ukatili huohuo.

Katika historia yote, dini ya uwongo imejitia unajisi kwa “damu ya manabii na ya watakatifu na ya wale wote ambao wameuawa juu ya dunia.” Ni wazi kwamba damu ya wale ambao Mungu anatambua kuwa wafia imani wake waaminifu inalia ikitaka alipize kisasi. (Ufunuo 6:9, 10; 18:24) Huenda baadhi ya wale ambao waliteseka na kufa kwa sababu ya imani yao katika siku za Jean Crespin walikuwa wakitafuta kweli ya kidini kwa unyoofu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Moja ya vitabu vya Crespin vilivyotafsiriwa ni Book of Martyrs, That Is, a Collection of Several Martyrs Who Endured Death in the Name of Our Lord Jesus Christ, From Jan Hus Until This Year, 1554. Baadhi ya chapa zilizosahihishwa na kuongezwa ukubwa zenye vichwa na habari tofauti-tofauti zilichapishwa Crespin alipokuwa hai; na nyingine baada ya kifo chake.

^ fu. 11 Vitabu vingine viwili kuhusu wafia imani vilichapishwa katika mwaka wa 1554—mwaka uleule ambao Crespin alichapisha kitabu chake Book of Martyrs (Kitabu cha Wafia Imani)—kimoja kilikuwa katika Kijerumani, na kiliandikwa na Ludwig Rabus, na kingine kiliandikwa na John Foxe katika Kilatini.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Jalada la kitabu “Book of Martyrs” cha Crespin (Toleo la 1564)

[Picha katika ukurasa wa 13]

Waprotestanti wauawa mbele ya Mfalme Henry wa Pili wa Ufaransa akiwa na watumishi wake

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

Images, both pages: © Société de l’Histoire du Protestantisme Français, Paris