Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nafurahi Kuwa Mchungaji

Nafurahi Kuwa Mchungaji

Nafurahi Kuwa Mchungaji

Limesimuliwa na Alymbek Bekmanov

Nilianza kuchunga kondoo nilipokuwa na umri wa miaka mitatu na nilifurahia sana kazi hiyo. Nilipotimia umri wa miaka 17, tayari nilikuwa mchungaji mwenye uzoefu. Baadaye, nilijifunza kuhusu mchungaji wa aina nyingine, mchungaji wa kiroho. Acha nieleze jinsi kutumika nikiwa mchungaji wa aina hiyo kumeniletea shangwe kubwa hata zaidi.

NILIZALIWA mwaka wa 1972. Familia yetu kubwa ya Kikirghiz iliishi katika kijiji cha Chyrpykty, kilichokuwa kwenye fuo za ziwa maridadi sana la Issyk Kul. Eneo linalozunguka ziwa hilo ni kivutio kikubwa kwa watalii ambao hutembelea Kyrgyzstan, ambayo hapo awali ilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Sasa mimi na mke wangu Gulmira, tunaishi huko Bishkek, mji mkuu wa Kyrgyzstan, ulio umbali wa kilomita 200 hivi kutoka mahali nilikolelewa.

Mchungaji na Kondoo

Nilipokuwa mtoto, tuliwalisha kondoo kwenye maeneo ya juu ya milimani wakati wa majira ya kuchipua. Hilo lilitia ndani kukwea umbali wa zaidi ya mita 3,000, ambao ulituchukua siku kadhaa. Wachungaji fulani walitumia njia za mkato na hivyo walifika malishoni upesi zaidi. Lakini njia walizotumia zilipita karibu na korongo na mabonde, na ikiwa kondoo wangepotea njia nyakati nyingine waliumia—au hata wakafa.

Kwenye njia hizo, ilikuwa kawaida kwa mbwa-mwitu kuwatisha au hata kuwashambulia kondoo, wakiwatenganisha kutoka kwa kundi na kuwaua. Kwa hiyo, mjomba wangu alichagua njia ambayo ilikuwa rahisi zaidi na isiyo na hatari, hata ingawa ilituchukua siku moja au zaidi kufika malishoni. Nyakati nyingine nilitaka kutembea kwa kasi, lakini mjomba wangu alinikataza. Aliniambia hivi, “Alymbek wafikirie kondoo, usijifikirie mwenyewe.”

Katika malisho yaliyokuwa kwenye sehemu za juu za milima, mazizi ya muda yalijengwa ili kuwalinda kondoo wakati wa usiku. Wachungaji wengine hawakupenda kuamka mapema na hivyo waliwapeleka kondoo malishoni jua likiwa limechomoza. Kondoo walipoanza kulisha, tayari jua lilikuwa kali sana.

Baada ya muda mfupi, kondoo hao wangesimama pamoja wakiwa wameinamisha vichwa vyao, wakipumua kwa shida. Kwa sababu hiyo, wao wangeshindwa kula vya kutosha na hivyo walikonda na kuwa dhaifu. Tofauti na wachungaji hao, mjomba wangu alirauka saa kumi alfajiri na jua lilipochomoza, tayari alikuwa amepeleka kondoo wake kwenye malisho bora. Wakiwa huko walilisha wakifurahia hewa baridi ya asubuhi iliyowaburudisha. Kama vile watu walivyosema kwa ukawaida, “Hali ya kondoo itakusaidia kumwelewa mchungaji.”

Wakati mzuri wa kuwachunguza kondoo na kuwatibu ni wakati wanapopumzika baada ya kulisha. Tatizo moja kuu ambalo kondoo wetu walikuwa nalo ni kushambuliwa na nzi ambao walitaga mayai kwenye kitovu cha kondoo. Hilo hufanya kitovu kiwashe na kuvimba. Ikiwa tatizo hilo haligunduliwi upesi, huenda uchungu ukawa mwingi sana hivi kwamba kondoo anaweza kutanga-tanga na mwishowe kufa. Tuliwachunguza kondoo wetu karibu kila siku na kuwatibu. Ingawa kufanya hivyo kulichukua muda na jitihada nyingi, tulithawabishwa kwa kuwa na kondoo wenye afya na walioridhika.

Kila jioni baada ya kurudi kwenye zizi kutoka malishoni, tuliwahesabu kondoo. Waliingia zizini kupitia mlango mwembamba—nyakati nyingine wakiwa watatu au wanne kwa wakati mmoja. Kundi letu lilikuwa na mamia ya kondoo, lakini tulikuja kuwa stadi wa kuwahesabu hivi kwamba tungehesabu kondoo 800 hivi kwa dakika 15 au 20. Haikuwa rahisi kufanya hivyo, lakini tulifaulu baada ya kupata uzoefu!

Ikiwa kondoo mmoja angepotea, mjomba wangu alichukua bunduki na fimbo na kutoka nje kwenda kumtafuta—hata kama usiku ulikuwa umeingia na mvua ilikuwa inanyesha bado alienda kumtafuta hata mwana-kondoo mmoja. Angepaaza sauti na kumwita. Sauti yake ingewaogopesha wanyama wa mwituni. Kondoo aliposikia sauti hiyo, alijihisi akiwa salama.

Tulimpa jina kila kondoo, ikitegemea maumbile au tabia yake. Katika kila kundi kulikuwa na kondoo wasumbufu. Kwa sababu fulani hawakutaka kumtii mchungaji. Wakati mwingine, kondoo fulani walimfuata yule asiye mtiifu. Hivyo mchungaji alijaribu sana kuwafunza na kuwatia nidhamu kondoo watundu. Kwa mfano, angemwacha kondoo huyo mtundu zizini akiwa peke yake. Baada ya muda, baadhi yao walikubali kurekebishwa na kufuata mwongozo wa mchungaji. Wale ambao hawakubadili tabia yao tuliwachinja na kuwala.

Mchungaji wa Aina Tofauti

Katika mwaka wa 1989, nilijifunza tae kwon do na nikawa mzoefu sana. Mwaka uliofuata, niliandikishwa katika jeshi la Sovieti. Nilipokuwa nikitumika huko Urusi, wenzangu tulioshiriki pamoja katika tae kwon do waliunda genge lao la ujambazi. Niliporudi nyumbani huko Kyrgyzstan, walinieleza kwamba ikiwa ningekubali kujiunga nao, ningepata chochote nilichohitaji. Lakini wakati huohuo, nilikutana na Mashahidi wa Yehova.

Mashahidi walinijibu maswali ambayo yalikuwa yamenisumbua sana tangu nilipokuwa mtoto mdogo, kama vile Kwa nini watu hufa? Baada ya mazungumzo tuliyokuwa nayo, nilikuja kuona kwamba kifo kilitokezwa na dhambi kutoka kwa mtu wa kwanza, Adamu. (Waroma 5:12) Pia nilijifunza kutoka kwenye Biblia kwamba Yehova, yule Mungu wa kweli, alimtuma Mwana wake Yesu awe Mkombozi wetu na kwamba tukiwa na imani katika Yehova na Mwana wake, tunaweza kusamehewa dhambi zetu tulizorithi. Kwa kufanya hivyo tunaweza kuwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani, kulingana na kusudi la awali la Mungu kwa wanadamu.—Zaburi 37:11, 29; 83:18; Yohana 3:16, 36; 17:1-5; Ufunuo 21:3, 4.

Majibu ya Maandiko niliyopata kutoka kwa Mashahidi yalikuwa wazi kabisa na yenye kueleweka sana hivi kwamba nilichochewa kusema, “Kwa kweli mambo yanapaswa kuwa hivyo!” Sikutamani tena kamwe kuwa pamoja na rafiki zangu wa hapo awali. Mara kadhaa walijaribu kunishawishi nijiunge tena na genge lao. Lakini tamaa yangu ya kujifunza na kufuata kweli za Biblia ilikuwa yenye nguvu sana hivi kwamba ilinisaidia kupinga vishawishi hivyo na kuwa mchungaji wa kiroho.

Katika kipindi hicho, mponyaji mmoja mashuhuri wa kimuujiza katika eneo letu alikuwa akija kumtembelea mama yangu. Siku moja niliporudi nyumbani, mwanamke huyo alikuwa akiwasiliana na pepo. Aliniambia kuwa nilikuwa na kipawa cha pekee na akanitia moyo niende msikitini ili nipewe hirizi fulani, na akaniambia kwamba hirizi hiyo ingenisaidia. Karibu anisadikishe kwamba nikifanya hivyo nitapokea uwezo wa kuponya.

Siku iliyofuata, niliwaendea Mashahidi waliokuwa wakinifunza Biblia na kuwaeleza kuhusu ziara ya mwanamke huyo. Walinionyesha katika Biblia kwamba Yehova anachukizwa na aina zote za kuwasiliana na pepo, kwa kuwa chanzo chake ni roho waovu. (Kumbukumbu la Torati 18:9-13) Sikulala kwa siku kadhaa kwa sababu ya kusumbuliwa na roho waovu. Mashahidi waliponifundisha jinsi ya kusali kulingana na mapenzi ya Yehova, nililala bila usumbufu wowote. Nilisadikishwa kwamba nilikuwa nimempata Mchungaji wa kweli, Yehova.

Nilijifunza kwamba Daudi, aliyeandika zaburi nyingi katika Biblia, alikuwa pia mchungaji alipokuwa kijana. Alimwita Yehova “Mchungaji wangu” na niliguswa moyo sana na hisia zake kumwelekea Yehova. (Zaburi 23:1-6) Nilitaka kumwiga Mwana wa Yehova, Yesu, ambaye anaitwa ‘mchungaji wa kondoo.’ (Waebrania 13:20) Nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa katika kusanyiko lililofanyiwa huko Bishkek, mapema katika mwaka wa 1993.

Mkutano Muhimu

Watu wengi wa ukoo, pamoja na jirani zangu, walianza kukutanika pamoja ili kujifunza Biblia. Watu 70 hivi kutoka kijiji changu walikutanika karibu na Ziwa Issyk Kul. Mtu mmoja wa ukoo, aliyekuwa kiongozi wa baraza la kijiji chetu, alipendezwa sana. Alisema kuwa angepanga kuwe na mkutano mkubwa ambapo tungeweza kueleza kuhusu imani yetu mpya. Lakini viongozi wa kidini wa eneo hilo waliwachochea watu wapinge kazi yetu ya kuhubiri. Walipanga kisiri kuutumia mkutano huo kuwachochea watu watupinge.

Siku ilipofika, watu elfu moja hivi walikusanyika, kutia ndani watu kutoka vijiji vitatu vilivyokuwa karibu. Mashahidi kadhaa walifika, na mmoja wao alianza kueleza kuhusu imani yetu iliyotegemea Biblia. Baada ya muda usiozidi dakika tano, mtu mmoja alisimama na kuanza kuuliza maswali yenye kuudhi. Watu walianza kutushutumu na kututisha, na umati huo ukawa karibu kutushambulia.

Wakati huo, mmoja wa kaka zangu ambaye alikuwa ameanza kujifunza Biblia, alisimama na kututetea. Kila mtu alimwogopa na kumwepuka kwa sababu alikuwa mpiganaji stadi. Alisimama kwa ujasiri kati ya Mashahidi na umati huo na tukaondoka bila vita vyovyote kutokea. Miaka iliyofuata, wengi kati ya wale waliohudhuria mkutano huo walibatizwa na kuwa Mashahidi. Leo kijiji chetu kilicho na watu karibu 1,000 kina Mashahidi wa Yehova zaidi ya 50.

Binti ya Mchungaji

Miezi kadhaa kabla ya kusanyiko kubwa la Mashahidi wa Yehova lililofanyika huko Moscow, Urusi, mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1993, nilikutana na Gulmira, Shahidi kutoka kijiji cha Wakirghiz. Alilelewa pia katika familia ya wachungaji. Katika mwaka wa 1988, wakati kazi ya Mashahidi ilikuwa bado imepigwa marufuku katika Muungano wa Sovieti, mama ya Gulmira alianza kujifunza Biblia pamoja na Shahidi mmoja anayeitwa Aksamy. Katika miaka ya 1970, Aksamy alikuwa Mkirghiz wa kwanza kuwa Shahidi wa Yehova katika eneo hilo.

Punde baadaye Gulmira alijiunga na mama yake katika funzo la Biblia pamoja na Aksamy. Katika mwaka wa 1990 wote wawili walibatizwa na kuwa Mashahidi. Moyo wa Gulmira ulimchochea kuanza utumishi wa wakati wote kwa hiyo akawa painia.

Katika miaka miwili iliyofuata, nilimwona Gulmira mara chache tu kwa sababu niliishi umbali wa kilomita 160. Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 1995, niliamua kumjua vizuri zaidi, kwa hiyo, asubuhi moja nilifunga safari na kuelekea nyumbani kwao. Nilishtuka sana aliponiambia kwamba alikuwa akiondoka nyumbani siku inayofuata kwenda kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Urusi, iliyokuwa umbali wa kilomita 5,633!

Kufikia wakati huo nilikuwa nimeanza utumishi wa wakati wote na pia nilikuwa nimeanza kujifunza Kirusi, kwani bado hatukuwa na vichapo katika Kikirghiz. Katika kipindi cha miaka mitatu tuliwasiliana na Gulmira kupitia barua na pia tulipanga kupatanisha usomaji wetu wa Biblia ili tuweze kuelezana mambo ya kiroho yenye kujenga. Wakati huo, nilitumika katika kutaniko la kwanza la Kikirghiz, katika mji wa Balikchi.

Kumtumikia Yehova Nikiwa na Gulmira

Katika mwaka wa 1998, Gulmira alikuja Kyrgyzstan kwa ajili ya likizo, na tukaoana wakati huo. Nilialikwa kutumika katika ofisi ya tawi ya Urusi. Nilifurahi kama nini kwa sababu nilikuwa nimeanza kujifunza Kirusi! Baadaye, nilipata mgawo wa kufanya kazi ya kutafsiri vichapo vya Biblia pamoja na kikundi cha Kikirghiz. Nilisali kwa Yehova na kumwomba anipe hekima na subira. Na pia, Gulmira, mfanyakazi mwenzangu, alinisaidia sana.

Katika mwaka wa 2004 kikundi chetu cha kutafsiri kilihamishwa hadi Bishkek, ambapo niliwekwa rasmi kutumikia katika halmashauri inayosimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kyrgyzstan. Wakati huo kulikuwa na makutaniko saba ya Kikirghiz na zaidi ya makutaniko 30 ya Kirusi kote nchini. Kufikia sasa kuna zaidi ya makutaniko 20 ya Kikirghiz na vikundi vingi katika lugha hiyo, ambavyo vinafanyiza asilimia 40 hivi ya Mashahidi 4,800 nchini Kyrgyzstan.

Mimi na Gulmira tuliamua kujifunza Kiingereza, kwa sababu lugha hiyo ingetusaidia katika utumishi wetu. Kwa sababu hiyo tulialikwa kwenda kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Marekani, katika mwaka wa 2008. Tukiwa huko, nilihudhuria shule ya pekee kwa ajili ya wale wanaoongoza kazi ya kuhubiri katika nchi za kwao.

Kwa sasa mimi na Gulmira, tunahisi kwamba tuna uwezo kamili wa kuwasaidia watu nchini Kyrgyzstan wamjue Mungu. Mambo ambayo tumejionea maishani yametusaidia kuona kwamba kwa kweli Yehova ni mchungaji mwenye upendo. Mimi binafsi nimejionea utimizo wa zaburi moja ya Biblia inayosema: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha. Anaiburudisha nafsi yangu. Ananiongoza katika mapito ya uadilifu kwa ajili ya jina lake.”—Zaburi 23:1-3.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kondoo wetu wakiwa malishoni

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kila jioni tulihesabu kondoo ili kuhakikisha hakuna aliyepotea

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mimi na Gulmira leo