Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zawadi za Ndani Zinazotufanya Tuwe wa Kipekee

Zawadi za Ndani Zinazotufanya Tuwe wa Kipekee

Zawadi za Ndani Zinazotufanya Tuwe wa Kipekee

MWANAMUME mwenye umri wa miaka 50 ambaye ni mjenzi alikuwa akisubiri treni kwenye kituo kimoja huko New York City. Kijana mmoja aliyekuwa hapo karibu akateguka na kuanguka kwenye reli wakati tu treni ilipokuwa ikija. Mara moja mjenzi huyo akaruka kwenye reli na kumshika kijana huyo na treni ikapita juu yao bila kuwaumiza.

Wakati wa utawala wa Wanazi, Mashahidi wa Yehova huko Ulaya walikataa kusema “Heil Hitler!” kwa sababu neno la Kijerumani heil linamaanisha “wokovu.” Walikuwa na imani yenye nguvu kwamba Yesu Kristo ndiye Mwokozi wao na kwamba “hakuna wokovu katika mwingine yeyote.” (Matendo 4:12) Kwa sababu walikataa kumwabudu Hitler, wengi walikamatwa na kupelekwa kwenye kambi za mateso, ambako waliendelea kushikilia kanuni zao za Kikristo.

Mifano hiyo inatuonyesha kwamba wanadamu wanaweza kutanguliza hali njema ya wengine—hata ya watu wasiowajua kabisa—badala ya kujifikiria na wanaweza kutanguliza kanuni badala ya uhuru wao wa kibinafsi. Je, tabia kama hiyo inaonyesha kwamba wanadamu ni wanyama tu waliotokea kupitia mageuzi? Au je, hilo linaonyesha kwamba sisi ni viumbe wa hali ya juu? Fikiria kuhusu jambo hilo unaposoma maswali yafuatayo:

● Kwa nini tuna dhamiri, tuna ufahamu wa mema na mabaya ndani yetu?

● Mbona tunastaajabu tunapofikiri kuhusu maajabu ya uumbaji?

● Mbona tunafurahia muziki, kuchora, mashairi, na usanii wa aina nyingine? Mambo hayo si ya lazima ili tuendelee kuishi.

● Mbona watu wa karibu kila tamaduni wanatamani kuwasiliana na mungu?

● Mbona tunajiuliza: ‘Kwa nini niko hapa?’ ‘Ni nini kusudi la uhai?’

● Mtu anapokufa, kwa nini tunafuata desturi fulani?

● Na kwa nini ulimwenguni pote kuna imani ya kwamba mtu anaendelea kuishi baada ya kifo? Je, tamaa tuliyozaliwa nayo ya kuishi milele ni kitu tu tulichorithi kupitia mageuzi?

Majibu Yanaweza Kupatikana Wapi?

Majibu yanayopatana na akili zaidi ya maswali hayo yanaweza kupatikana katika kitabu kitakatifu kilichoenezwa zaidi ulimwenguni—Biblia. Fikira kile ambacho Biblia inasema kuhusu mambo yafuatayo:

Utu wa mwanadamu. Mwanadamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu,” yaani, tuna uwezo wa kuonyesha sifa za Muumba wetu. (Mwanzo 1:27) Kwa sababu hiyo, mwanadamu wa kwanza alikuwa “mwana wa Mungu.”—Luka 3:38.

Uhitaji wetu wa kupenda na kupendwa. “Mungu ni upendo,” inasema 1 Yohana 4:8. Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tunahitaji upendo kuanzia tunapozaliwa hadi tunapokufa. Ikiwa “sina upendo, mimi si kitu,” akaandika Paulo mtume Mkristo. (1 Wakorintho 13:2) Alisema hivi pia: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.”—Waefeso 5:1.

Uhitaji wetu wa kiroho. “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Maneno ya Mungu yaliyorekodiwa katika Biblia yanatufunulia utu wake na kusudi lake kwa ajili yetu. Hatuwezi kuishi maisha yenye kusudi la kweli iwapo hatuna uhusiano na Mungu.

Kwa nini tunakufa? “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele.” (Waroma 6:23) Dhambi ni kukosa kuishi kupatana na viwango vya maadili na vya kiroho vya Mungu. Hata hivyo, Mungu amekusudia kuja kuondoa dhambi, kuwaponya wote wanaompenda na kumtii, na kuwapa uzima wa milele katika Paradiso duniani.—Zaburi 37:10, 11, 29; Luka 23:43.

Je, ungependa kufurahia maisha kabisa, labda hata ukisitawisha vipawa ambavyo hukuwahi kufikiri unavyo? Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu Muumba wako na kusudi lake la ajabu kwa ajili yako? Ikiwa ndivyo, tunakukaribisha uichunguze Biblia, chanzo cha kweli ya kiroho. Hakuna jambo lingine linaloweza kukupa furaha ya kweli sasa na wakati ujao.—Mathayo 5:3; Yohana 17:3.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 9]

TUNAHITAJI UPENDO TANGU TUNAPOZALIWA

“Ubongo mchanga unahitaji hasa kuchochewa na kuonyeshwa upendo,” anasema mwanasayansi Gerald L. Schroeder. Basi ni jambo la maana sana kwamba wazazi wafuate himizo la Biblia, ambalo hasa akina mama wanapewa, kwamba “wawapende watoto wao”!—Tito 2:4.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Tunafurahia mambo mengi mazuri na yenye kupendeza ambayo si muhimu ili uhai uwepo

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wanadamu wanahitaji mengi zaidi kuliko chakula na maji. Pia wanahitaji mwongozo wa Muumba wao