Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”

“Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”

“Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”

“SITASAHAU asubuhi hiyo ya Jumatatu (Siku ya 1) kwenye posta,” anasema Andre, mwanamume mzungu aliyezaliwa nchini Afrika Kusini lakini anayeishi Namibia. “Ofisi za posta zilikuwa zimejaa watu. Niliona mfuko uliokuwa umeachwa sakafuni. Nilichukua barua zangu na kuondoka. Baada ya kuendesha gari kwa dakika tatu hivi nilisikia mlipuko mkubwa. Baadaye, niligundua kwamba bomu lilikuwa limelipuka karibu sana na mahali nilipokuwa nimetoka kusimama.”

“Nilitaka tu kuchukua barua zangu,” anaeleza Andre. “Lakini nilishtuka sana kujua kwamba watu wasio na hatia, ambao baadhi yao nilikuwa ninawafahamu walikuwa wamelipuliwa vipande-vipande. Bado mimi huingiwa na hofu ninapokumbuka tukio hilo, ingawa lilitukia zaidi ya miaka 25 iliyopita. Nyakati nyingine, mimi huwakumbuka watu niliowaona wakiwa wamekufa au kujeruhiwa na kujiambia kwamba niliponea chupuchupu.”

Tatizo la Ulimwenguni Pote

Ingawa huenda usipatwe moja kwa moja na shambulio kama hilo, huenda umesikia kwamba matukio kama hayo yanatendeka mara nyingi ulimwenguni pote. Watu wengi zaidi wanatumia jeuri, matendo ambayo mara nyingi yanaitwa ya kigaidi ili kutimiza malengo yao.—Ona sanduku “Magaidi Ni Nani?” kwenye ukurasa unaofuata.

Mwandishi fulani wa habari anayechunguza mambo aligundua kwamba mnamo 1997 kulikuwa na “nchi nne tu ambako magaidi wa kujitoa mhanga walikuwa wakitenda kwa kuendelea.” Lakini katika mwaka wa 2008 mchunguzi huyohuyo aliandika kwamba “zaidi ya nchi 30 katika kila bara isipokuwa Australia na Antaktika zilikumbwa na mashambulizi mabaya ya ugaidi wa kujitoa mhanga.” Alimalizia kwa kusema kwamba mashambulizi hayo “yanatekelezwa na makundi mengi zaidi, na yanawaua watu wengi zaidi kila mwaka.”—The Globalization of Martyrdom.

Fikiria shambulizi lililotajwa mwanzoni mwa habari hii. Kikundi cha watu waliodai kwamba walilipua bomu hilo walijiita wapiganiaji uhuru. Walikuwa wakijaribu kujipatia uhuru kutoka kwa serikali iliyotawala nchi yao. Lakini ni nini ambacho huwachochea watu wafanye mambo kama hayo ili kutimiza malengo yao? Fikiria kisa cha Hafeni.

Hafeni alizaliwa nchini Zambia na kulelewa katika kambi za wakimbizi katika nchi jirani. “Nilikuwa na hasira,” akasema, “kwa sababu ya ukatili na ukosefu wa haki ambao familia yetu na nyingine zilikuwa zimetendewa.” Kwa hiyo, akajiunga na kikundi cha wanamgambo ambacho wazazi wake walishirikiana nacho.

Akifikiria kuhusu nyakati hizo, Hafeni anaendelea kusema: “Jambo lenye kusikitisha zaidi ni madhara ya kihisia unayopata kwa kuishi kama mkimbizi. Watoto walitenganishwa na mama, baba, na ndugu na dada zao. Wale wenye umri mkubwa walienda kupigana. Wengi wao hawakurudi. Sikuwahi kumwona baba yangu, hata katika picha. Ninachojua tu ni kwamba alikufa vitani. Bado ninakumbwa na maumivu makali ya kihisia hadi leo.”

Kwa kweli, mambo yanayohusika ni magumu. Kuelewa mambo hayo vizuri kutakuwezesha kuona kinachopaswa kufanywa ili wanadamu waishi bila jeuri ya aina hiyo.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 4]

MAGAIDI NI NANI?

Mtafiti Mark Juergensmeyer anaeleza: “Iwe mtu atatumia neno ‘gaidi’ kufafanua matendo ya jeuri au la, kunategemea ikiwa anafikiri matendo hayo ni ya haki. Kwa kiasi kikubwa utumizi wa neno hilo unategemea maoni ya mtu kuhusu ulimwengu: iwapo anaona ulimwengu kuwa wenye amani, basi matendo ya jeuri yanaonekana kuwa ugaidi. Iwapo anaona kuna vita ulimwenguni, basi huenda matendo ya jeuri yakaonekana kuwa halali.”

Kwa hiyo, mara nyingi kuna sababu za kisiasa wakati neno “gaidi” linatumika. Vikundi vingi hujiona kuwa vya wapiganiaji uhuru, si magaidi. Kupatana na mwandikaji mmoja, ugaidi unahusisha (1) matendo yaliyokusudiwa kuwaathiri raia na (2) utumizi wa jeuri ili kupitisha ujumbe, yaani, kuwaogopesha watu. Kwa hiyo, wapiganaji—wawe ni wanamgambo au ni wa serikali—mara nyingi wanaweza kutumia mbinu za kigaidi.