Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anajali?

Je, Mungu Anajali?

Je, Mungu Anajali?

ASUBUHI ya Novemba 1, 1755 (1/11/1755), jiji la Lisbon, Ureno, lilikumbwa na tetemeko la nchi. Kisha kukawa na tsunami na moto ambao uliharibu sehemu kubwa ya jiji hilo na kuua maelfu.

Baada ya tetemeko la nchi lililotukia huko Haiti mnamo 2010, makala moja katika gazeti National Post la Kanada ilisema hivi: “Misiba yote mikubwa hujaribu sana imani ya wanadamu kwamba kuna mtu fulani mwenye nguvu zisizo za kibinadamu. Lakini misiba mingine, kama huu wa sasa [huko Haiti] unaofanana na [ule mkubwa uliotukia] Lisbon, hujaribu imani hata zaidi.” Makala hiyo ilimalizia kwa kusema: “Huenda Mungu ameiacha Haiti.”

Akiwa “Mweza-Yote,” Yehova Mungu ana nguvu zisizo na mipaka, kutia ndani uwezo wa kukomesha kuteseka. (Zaburi 91:1) Isitoshe, tunaweza kuwa na hakika kwamba anajali. Kwa nini?

Tunajua Nini Kumhusu Mungu?

Mungu anawahurumia wanadamu wanaoteseka. Waisraeli walipokuwa watumwa huko Misri na kutendewa vibaya na wale waliowashika mateka, Mungu alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” (Kutoka 3:7) Hilo linaonyesha nini? Kwamba Mungu hapuuzi kuteseka kwa wanadamu. Badala yake, nabii Isaya aliandika hivi karne nyingi baadaye kuhusu Waisraeli: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.”—Isaya 63:9.

“Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Mungu hutenda kwa haki katika kila jambo na habagui. “Atailinda njia ya washikamanifu wake,” lakini pia ‘atawalipa dhiki wale wanaowafanyia dhiki’ watu waadilifu. (Methali 2:8; 2 Wathesalonike 1:6, 7) Bila ubaguzi, “yeye hawapendelei wakuu, wala kuwajali matajiri kuliko maskini, maana wote ni kazi ya mikono yake.” (Ayubu 34:19, Biblia Habari Njema) Pia Mungu anajua njia bora ya kuponya kuteseka kwa wanadamu. Tofauti na hilo, tunaweza kulinganisha jitihada za wanadamu za kusuluhisha mambo na kutumia bendeji ndogo kufunga jeraha la risasi. Ingawa bendeji hiyo inaweza kufunika kidonda, haiwezi kumtibu mgonjwa na pia haiwezi kumwondolea maumivu yake.

Mungu ni “mwenye rehema na neema . . . naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo.” (Kutoka 34:6) Kulingana na Biblia, neno “rehema” linamaanisha kuwa na huruma na sikitiko, sifa ambayo humchochea mtu kumsaidia mwingine. Mzizi wa neno la Kiebrania “neema” unafafanuliwa kuwa “mtu anayesukumwa na moyo kumsaidia mtu mwenye uhitaji.” Kulingana na kamusi Theological Dictionary of the Old Testament, neno linalotafsiriwa “fadhili zenye upendo” linatia ndani “hatua inayochukuliwa kumsaidia mtu ambaye amepatwa na mabaya au taabu.” Kwa hiyo, Yehova Mungu hahuzuniki tu anapowaona wanadamu wakiteseka, bali akichochewa na rehema, neema, na fadhili zake zenye upendo, yeye hutoa msaada. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atakomesha kuteseka.

Habari iliyotangulia ilitaja mambo matatu ambayo huwafanya wanadamu wateseke sana leo, na hakuna lolote kati ya hayo linalosababishwa na Mungu. Sasa acheni tuchunguze ni nini chanzo cha mambo hayo.

Uamuzi wa Kibinafsi

Hapo mwanzoni, Adamu alitawaliwa na Mungu. Hata hivyo, alipoambiwa achague, aliamua kukataa utawala wa Mungu na kujaribu kujitegemea mwenyewe bila msaada wa Mungu. Alipuuza onyo la Yehova linalopatikana katika Mwanzo 2:17: “Utakufa hakika.” Kukataa kujitiisha chini ya utawala mkamilifu wa Mungu kulileta dhambi na kutokamilika. Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Lakini Mungu ataondoa matokeo ya dhambi.

Matukio Yasiyotazamiwa

Kama iliyotajwa hapo juu, mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikataa mwongozo wa Mungu—mwongozo ambao ungewalinda wanadamu. Uamuzi wake unaweza kufananishwa na mgonjwa ambaye anakataa kutunzwa na daktari stadi mwenye ujuzi. Ikiwa mgonjwa huyo hajui hatari na matatizo ya kiafya ambayo daktari huyo anajua, huenda akateseka kwa sababu ya kumpuuza daktari kimakusudi. Vivyo hivyo, kwa sababu mwanadamu ameitumia vibaya dunia—kutia ndani kutumia mbinu ujenzi zisizo salama na kupuuza nguvu za asili za dunia—jambo hilo mara nyingi husababisha misiba ya asili. Hata hivyo, Mungu hataachilia hali hiyo iendelee milele, kama habari inayofuata itakavyoonyesha.

“Mtawala wa Ulimwengu Huu”

Kwa nini Mungu alimruhusu Shetani atawale ulimwengu baada ya kuasi? Kulingana na kitabu kimoja, “serikali yoyote mpya inapoanza kutawala, kunakuwa na kipindi kifupi ambacho wale wanaotawala wanaweza kuilaumu serikali iliyopita kwa matatizo yaliyopo.” Ikiwa Yehova hangempa “mtawala wa ulimwengu huu” wakati wa kutosha kutawala, na Shetani ashindwe kutawala vyema, basi angemlaumu mtawala wa zamani, Mungu. (Yohana 12:31) Hata hivyo, kuruhusu wakati wa kutosha upite ili Shetani aonyeshe mamlaka yake ulimwenguni pote kumethibitisha kwamba ameshindwa kabisa kutawala. Lakini bado kuna swali, Tuna uhakika gani kwamba kuteseka kutakwisha?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, daktari anaweza kutumia bendeji ndogo kufunga jeraha kubwa linalovuja damu?