Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kulea Watoto Wachanga Hadi Wanapobalehe

Kulea Watoto Wachanga Hadi Wanapobalehe

Kulea Watoto Wachanga Hadi Wanapobalehe

“Kabla ya watoto wako kufikia umri wa miaka mitano, wao huwa katika mazingira mazuri ya nyumbani na ni rahisi kuwafundisha sifa nzuri. Lakini mara tu wanapoanza kwenda shuleni, wanakumbana na njia tofauti za kufanya mambo na za kuzungumza.”—Valter, Italia.

WATOTO wanapozidi kukua, wao hujaribu kuelewa ulimwengu wao unaozidi kupanuka. Wao huchangamana na watu wengi zaidi—watoto wanaocheza nao, wanafunzi wenzao, na watu wa ukoo. Kama Valter aliyenukuliwa hapo juu anavyosema, si wewe tu uliye na uvutano juu ya mtoto wako tena, kama ulivyofanya alipokuwa mchanga. Hiyo ndiyo sababu unapaswa kutumia kipindi kati ya utoto na kubalehe kumfundisha mtoto wako umuhimu wa kutii na kuwa na adabu. Pia ni muhimu kumpa mwongozo kuhusu mambo yaliyo sawa na yaliyo makosa.

Si rahisi kumfundisha mambo hayo wala haichukui muda mfupi. Huenda ukahitaji ‘kumkaripia, kumkemea, kumhimiza, kwa ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha.’ (2 Timotheo 4:2) Wazazi Waisraeli waliamriwa hivi kuhusu sheria za Mungu: ‘Uzikazie kwa mwana wako na kuzisema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kama andiko hilo linavyoonyesha, ni muhimu sana kuwafundisha kwa kuendelea.

Kuna magumu fulani yanayohusika katika kutimiza daraka la kuwalea watoto. Acheni tufikirie baadhi yake.

Wakati wa Kusikiliza

Biblia inasema kwamba ingawa kuna “wakati wa kusema,” pia kuna wakati wa kusikiliza. (Mhubiri 3:7) Ni katika njia gani unaweza kumfundisha mtoto wako kusikiliza wakati wengine wanapozungumza—kutia ndani wewe unapozungumza? Njia moja ni kumwekea mfano. Je, wewe huwasikiliza wengine kwa makini, kutia ndani watoto wako?

Watoto wanaweza kukengeushwa kwa urahisi, na bila shaka ni rahisi kukosa subira unapojaribu kuwasiliana nao. Kila mtoto ni tofauti, kwa hiyo chunguza na utambue njia bora za kuwasiliana na mtoto wako. Kwa mfano, David, baba mmoja nchini Uingereza, anasema hivi: “Mimi humwomba binti yetu arudie jambo nililomwambia kwa kutumia maneno yake mwenyewe. Hilo linamsaidia ajifunze kusikiliza kadiri anavyokua.”

Yesu alipokuwa akiwafundisha wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:18) Ikiwa watu wazima wanapaswa kufanya hivyo, basi ni muhimu hata zaidi kwa watoto kuwasikiliza wengine kwa makini!

“Kusameheana kwa Hiari”

Biblia inasema: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Wakolosai 3:13) Watoto wanaweza kuzoezwa kusitawisha uwezo wa kusamehe. Jinsi gani?

Kama vile ambavyo tumetaja kuhusu ustadi wa kusikiliza vizuri, unahitaji kuweka mfano. Acha watoto wako wakuone ukisitawisha roho ya kusamehe unaposhughulika na wengine. Marina, mama mmoja nchini Urusi, hujitahidi kufanya hivyo. Anasema: “Tunajaribu kuwawekea watoto wetu mfano mzuri wa kuwasamehe wengine, kuachilia mambo tunapokosewa, na kutoudhika,” na anaongezea hivi: “Ninapowakosea watoto wangu, mimi huwaomba msamaha. Ninataka wajifunze kufanya vivyo hivyo wanaposhughulika na wengine.”

Uwezo wa kutatua ugomvi na kusamehe utakuwa muhimu wanapokuwa watu wazima. Wazoeze watoto wako sasa kuwafikiria wengine na kukubali makosa yao. Kwa kuwafundisha mambo hayo, utakuwa ukiwapa zawadi bora itakayowasaidia sana wanapokua.

“Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”

Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ watu wengi ‘wanajipenda wenyewe.’ (2 Timotheo 3:1, 2) Sasa, wakati ambapo watoto ni wachanga, ndio wakati wa kuwafundisha kuwa wenye shukrani. “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani,” akaandika mtume Paulo.—Wakolosai 3:15.

Hata watoto wanapokuwa wachanga, wanaweza kujifunza kuwa na adabu na kuwafikiria wengine. Jinsi gani? “Njia bora unayoweza kuwafundisha watoto kuwa na mtazamo wenye shukrani ni kuonyesha mtazamo huo kila wakati unapokuwa nyumbani,” ndivyo Dakt. Kyle Pruett alivyowaeleza waandishi wa gazeti Parents. Anaongezea hivi: “Hilo linamaanisha kwamba unapaswa kusema kwa ukawaida jinsi unavyothamini sana msaada unaopata na mambo mengine wanayofanya yanayoonyesha ufikirio . . . Unahitaji kufanya hivyo mara nyingi.”

Baba mmoja nchini Uingereza anayeitwa Richard, anajitahidi kufanya hivyo: “Mimi na mke wangu huwashukuru wale ambao wametuonyesha fadhili, kama vile walimu au babu na nyanya,” anasema. “Familia fulani inapotualika kwa ajili ya mlo, sisi huandika kadi ya kuwashukuru, na watoto wote hutia sahihi au wanachora picha fulani juu ya kadi hiyo.” Kuwatendea wengine fadhili na kuwa mwenye shukrani kutamsaidia mtoto wako kusitawisha urafiki wa kudumu na wa karibu baadaye maishani.

“Usimnyime Nidhamu”

Watoto wako wanapozidi kukua, ni muhimu wajifunze kwamba mambo wanayofanya yana madhara. Hata wanapokuwa wachanga, lazima watoto wajitiishe chini ya mamlaka, si nyumbani tu bali pia shuleni na katika jamii. Unaweza kuwasaidia watoto wako kujifunza kanuni inayosema kwamba utavuna unachopanda. (Wagalatia 6:7) Jinsi gani?

Biblia inasema: “Usimnyime . . . nidhamu.” (Methali 23:13) Ikiwa umesema wazi kwamba utamwadhibu mtoto kwa sababu ya tendo fulani baya, usiogope kufanya kama ulivyosema na kumtia nidhamu. “Ni muhimu kutobadili-badili msimamo,” anasema Norma, mama mmoja nchini Argentina. “Kubadili-badili msimamo humtia moyo mtoto kufanya anavyotaka.”

Wazazi wanaweza kuepuka ubishi mwingi baada ya mtoto kufanya jambo baya kwa kuhakikisha kwamba mtoto anaelewa mapema matokeo ya kutotii. Watoto watakubali nidhamu kwa urahisi iwapo wanajua sheria na wanajua kitakachotukia wakivunja sheria hizo na ikiwa wana sababu ya kuamini kwamba adhabu haiwezi kubadilishwa.

Bila shaka, ili nidhamu iwe na matokeo, inapaswa kutolewa bila hasira. Biblia inasema: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Nidhamu haipaswi kutolewa kwa ukatili na haipaswi kuwa yenye kudhuru—kimwili au kihisia.

Lakini unaweza kuzuia hasira yako jinsi gani mtoto wako anapokukasirisha kabisa? “Si rahisi kufanya hivyo nyakati zote,” anasema Peter, baba mmoja nchini New Zealand, “lakini watoto wanahitaji kujifunza kwamba nidhamu hutolewa kwa sababu ya tendo walilofanya na si kwa sababu mzazi ameshindwa kujizuia.”

Peter na mke wake hujaribu kuwasaidia watoto wao waone faida ya muda mrefu ya nidhamu wanayopewa. “Hata watoto wanapofanya jambo lenye kuchukiza sana,” anasema, “sisi hujaribu kuwaonyesha tungependa wawe watu wa aina gani badala ya kukazia kosa walilofanya.”

“Usawaziko Wenu na Ujulikane”

Mungu alisema hivi kuhusu nidhamu ambayo angewapa watu wake: “Nitakutia adabu kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 46:28) Utafanikiwa zaidi ukitoa nidhamu kwa haki na inayolingana na makosa yaliyofanywa. Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane.”—Wafilipi 4:5.

Sehemu moja ya kuwa na usawaziko ni kutoa nidhamu kwa njia ambayo haitawavunjia watoto wako heshima. Santi, baba mmoja nchini Italia, anasema: “Sijawahi kumshushia heshima mwanangu au binti yangu. Badala yake mimi hujaribu kutambua sababu iliyomfanya atende jambo fulani na kushughulikia jambo hilo. Ikiwezekana, siwatii nidhamu watoto wangu mbele ya watu wengine, au hata mbele ya wenzao. Nami sifanyi ucheshi kuhusu udhaifu wao iwe ni mbele ya watu au faraghani.”

Richard, aliyenukuliwa awali, anatambua hekima ya kuwa na usawaziko. “Hupaswi kukusanya makosa kadhaa kisha kutoa nidhamu kwa makosa hayo yote mara moja,” anasema. “Baada ya kutoa nidhamu, ni muhimu kwamba usiendelee kuzungumza kuhusu jambo hilo na kumkumbusha mtoto kuhusu makosa yake.”

Kulea watoto ni kazi ngumu inayohitaji mtu ajidhabihu lakini inaleta thawabu nyingi. Hivyo ndivyo Yelena, mama mmoja nchini Urusi alivyogundua. Anasema: “Nimeamua kufanya kazi kwa saa chache kila juma ili niwe na wakati mwingi wa kuwa pamoja na mwana wangu. Hilo linahitaji jitihada na nimepata hasara ya kifedha, lakini ninapomwona mwanangu akiwa na shangwe nyingi na uhusiano wetu ukiimarika, ninatambua kwamba nilijidhabihu kwa njia inayofaa.”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Watoto wanaweza kujifunza kuwafikiria wengine

[Picha katika ukurasa wa 12]

Watie watoto wako nidhamu kwa njia ambayo haitawavunjia heshima