Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Lengo la Mzazi Ni Nini?

Lengo la Mzazi Ni Nini?

Maoni ya Biblia

Lengo la Mzazi Ni Nini?

UNGEPENDA kijana wako awe mtu wa aina gani?

A. Awe kama wewe.

B. Awe mwasi ambaye lengo lake ni kutenda kinyume cha jinsi unavyotenda.

C. Awe mtu mzima anayefanya maamuzi ya hekima.

Ingawa wazazi fulani wangependa kijana wao awe mtu anayetajwa mwisho (C) huenda wakajaribu kumfanya awe mtu anayetajwa mwanzoni (A). Wao hujaribu kumlazimisha kijana wao afuate viwango vyao, kama vile kwa kumchagulia kazi atakayofanya. Matokeo yanakuwa nini? Mara tu anapoanza kujitegemea, kijana hutenda kinyume kabisa na jinsi wazazi walivyotaka. Vijana wengi ambao wazazi wao wangependa kuwaona wakiwa kama mtu anayetajwa kwenye alama A, huwa kama mtu anayetajwa kwenye alama ya B.

Huwezi Kuwadhibiti Vijana Kabisa

Unataka kijana wako awe mtu mzima anayefanya maamuzi ya hekima. Lakini unaweza kufikia lengo hilo jinsi gani? Jambo moja ni hakika: Kujaribu kumdhibiti kabisa si suluhisho. Fikiria sababu mbili zifuatazo.

1. Kujaribu kumdhibiti kabisa hakupatani na maandiko. Yehova Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. Anawaruhusu watu wachague njia watakayofuata maishani, iwe nzuri au mbaya. Kwa mfano, Kaini alipokuwa na hasira na kutaka kumuua ndugu yake Abeli, Yehova alimwambia hivi: “Ukigeuka utende mema, je, hutainuliwa? Lakini usipogeuka utende mema, kuna dhambi inayovizia katika mwingilio, nayo inakutamani wewe. Je, wewe utaishinda?”—Mwanzo 4:7.

Ona kwamba ingawa Yehova alimpa Kaini shauri la wazi, hakumlazimisha alifuate. Kaini alipaswa kuchagua ikiwa angeshinda hasira yake au la. Tunajifunza nini? Ikiwa Yehova hajaribu kudhibiti kabisa viumbe wake ili wamtii, basi wewe hupaswi kujaribu kuwadhibiti kabisa vijana wako. *

2. Unapojaribu kumdhibiti kabisa atatenda kinyume na unachotaka. Hebu wazia kwamba mwuzaji fulani anajaribu kukulazimisha ununue bidhaa fulani. Kadiri anavyosisitiza, ndivyo unavyokataa katakata. Hata ikiwa unahitaji bidhaa hiyo, huenda usipende jinsi anavyojaribu kukushinikiza uinunue. Unataka kumwepuka kabisa mwuzaji huyo.

Hali inaweza kuwa hivyo ukijaribu kumlazimisha kijana wako afuate viwango, imani, na miradi yako. Je, atakubali? La! Kwa kweli, huenda kufanya hivyo kukamfanya kijana wako achukie viwango vyako. Mara nyingi, wazazi wanapojaribu kuwadhibiti kabisa watoto wao, watoto huasi. Basi unaweza kufanya nini?

Badala ya kujaribu kudhibiti kabisa maisha ya kijana wako, kwa kumlazimisha afuate viwango vyako kama ulivyofanya alipokuwa mchanga, msaidie aone hekima ya kufanya lililo sawa. Kwa mfano, ikiwa wewe ni Mkristo, mwonyeshe kwamba kufuata kanuni za Mungu kutamletea uradhi katika maisha yake yote.—Isaya 48:17, 18.

Unapofanya hivyo, mwekee mfano mzuri. Sitawisha sifa ambazo unataka kijana wako awe nazo. (1 Wakorintho 11:1) Onyesha wazi viwango ambavyo umechagua kufuata. (Methali 4:11) Kijana wako anapompenda Mungu na viwango vyake, basi atafanya maamuzi ya hekima, hata wakati haupo.—Zaburi 119:97; Wafilipi 2:12.

Mfundishe Stadi Zitakazomfaidi

Kama ilivyotajwa kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili, siku moja—ambayo huenda kwa maoni yako ikaja haraka sana—mtoto wako ambaye amekuwa mtu mzima “atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ukiwa mzazi, unataka kuhakikisha kwamba amepata stadi zitakazomsaidia kujitegemea akiwa mtu mzima. Fikiria kuhusu stadi unazoweza kumfundisha sasa akiwa bado nyumbani.

Kazi za Nyumbani. Je, kijana wako anaweza kupika chakula? kuosha na kupiga pasi nguo zake? kusafisha chumba chake na kuhakikisha kwamba ni nadhifu? kufanya marekebisho madogo ya gari? Kuwa na ustadi wa kufanya mambo kama hayo kutamsaidia mwana au binti yako kusimamia nyumba yake siku moja. Mtume Paulo alisema hivi: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo.”—Wafilipi 4:11.

Kushirikiana na Wengine. (Yakobo 3:17) Je, kijana wako ana uhusiano mzuri na watu wengine? Je, anaweza kusuluhisha ugomvi kwa utulivu na fadhili? Je, umemzoeza kuwaheshimu wengine na kusuluhisha mizozo kwa amani? (Waefeso 4:29, 31, 32) Biblia inasema: “Waheshimuni watu wa namna zote.”—1 Petro 2:17.

Kupangia Matumizi ya Pesa. (Luka 14:28) Je, unaweza kumsaidia kijana wako ajifunze ufundi fulani, kupanga na kufuata bajeti, na kuepuka madeni? Je, umemfundisha kuweka pesa akiba ili anunue vitu anavyohitaji na kuepuka kununua vitu ambavyo hakupangia na kuridhika na mahitaji ya lazima? (Methali 22:7) Paulo aliandika hivi: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika.”—1 Timotheo 6:8.

Vijana ambao wamejifunza kufuata viwango vya maadili na wamejifunza stadi fulani wanazoweza kutumia wako tayari kuishi kama watu wazima. Wazazi wamefikia lengo lao!—Methali 23:24.

[Maelezo ya Chini]

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Lengo lako ni nini ukiwa mzazi?—Waebrania 5:14.

● Kijana wako atakabili uamuzi gani atakapokuwa mtu mzima? —Yoshua 24:15.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ungependa kijana wako awe mtu wa aina gani?

Awe kama wewe . . .

Awe mwasi . . .

Awe mtu mzima mwenye kutegemeka