Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mashini Yenye Uwezo Mkubwa Zaidi Ulimwenguni”

“Mashini Yenye Uwezo Mkubwa Zaidi Ulimwenguni”

“Mashini Yenye Uwezo Mkubwa Zaidi Ulimwenguni”

UBONGO wa mtoto mchanga umesemwa kuwa ndiyo “mashini yenye uwezo mkubwa zaidi ulimwenguni,” na kwa sababu nzuri. Mtoto anazaliwa akiwa tayari kufyonza kila kitu anachoona, kusikia, na kugusa.

Zaidi ya yote, mtoto huvutiwa na wanadamu wengine, yaani, anavutiwa watu wanapomgusa, anavutiwa na nyuso na sauti zao. Kitabu Babyhood, kilichoandikwa na Penelope Leach, kinasema hivi: “Uchunguzi mwingi umefanywa kuhusu mambo yanayovutia zaidi macho ya mtoto, sauti zinazovuta fikira zake, na vitu anavyopenda kugusa mara nyingi. Yote hayo hutimizwa kwa urahisi na mtu mzima anayemtunza.” Haishangazi kwamba wazazi wanatimiza fungu muhimu katika ukuzi wa mtoto!

‘Nilisema Kama Kitoto’

Wazazi na vilevile madaktari wa watoto wanashangazwa sana na uwezo wa mtoto wa kujifunza lugha kwa kuisikia tu. Watafiti wamegundua kwamba siku chache tu baada ya kuzaliwa, mtoto anajua sauti ya mama yake na anaipenda kuliko sauti ya mtu asiyemfahamu; majuma machache tu baadaye, anaweza kutofautisha kati ya sauti za lugha ya wazazi wake na za lugha nyingine; na miezi michache baadaye, anajua tofauti kati ya maneno na hivyo anaweza kutofautisha usemi wa kawaida na sauti zisizoweza kueleweka.

Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto mchanga nilisema kitoto.” (1 Wakorintho 13:11, Biblia Habari Njema) Mtoto mchanga husema kwa njia gani? Kwa kawaida anabubujika kwa mambo yasiyoeleweka. Je, hizo ni kelele tu zisizo na maana? La! Katika kitabu chake What’s Going On in There?—How the Brain and Mind Develop in the First Five Years of Life, Dakt. Lise Eliot anatukumbusha kwamba kusema kunahusisha “ustadi wa ajabu wa ubongo wa kutendesha misuli inayodhibiti midomo, ulimi, kaakaa, na zoloto na kuifanyisha kazi kwa haraka na upatano.” Anaongezea hivi: “Ingawa huenda ikaonekana kwamba kusudi la sauti zisizoeleweka za watoto wachanga ni kuvuta fikira za watu tu, sauti hizo hutimiza jambo muhimu katika kuzoeza misuli kusonga kwa upatano wakati atakapoanza kuongea.”

Wazazi wanapoongea kwa msisimuko mwingi pamoja na mtoto wao mchanga anapopiga kelele zisizoeleweka, hilo hutimiza kusudi fulani. Msisimuko huo humchochea mtoto aendelee kutokeza sauti hizo. Mazungumzo hayo kati ya mtoto na wazazi humfundisha mtoto mchanga mambo yanayohusika katika mazungumzo—ustadi ambao atautumia katika maisha yake yote.

Majukumu Yanabadilika

Wazazi wa mtoto mchanga huwa na shughuli nyingi za kumtimizia mtoto wao mahitaji yake ya kila siku. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumlisha. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumbadilisha nepi. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumbeba. Utunzaji huo unafaa na unahitajika. Hiyo ndiyo njia kuu ambayo wazazi wanatimiza jukumu lao wakiwa watunzaji.1 Wathesalonike 2:7.

Ukizingatia mambo yaliyozungumziwa hapa juu, ni jambo la asili kwa mtoto kuhisi kwamba yeye ndiye mtu muhimu zaidi na kwamba watu wazima, hasa wazazi wake, wapo ili tu kumtimizia mahitaji yake yote. Maoni hayo yana kasoro lakini inaeleweka ni kwa nini anahisi hivyo. Kumbuka kwamba kwa zaidi ya mwaka mmoja, hivyo ndivyo mtoto amezoea kutendewa. Kwa maoni yake, yeye ni mfalme wa milki fulani iliyo na watu wakubwa ambao wamewekwa hapo ili tu wamtumikie. John Rosemond, mshauri wa mambo ya familia anaandika hivi: “Kwa muda usiozidi miaka miwili, mtoto amefundishwa kuwa na maoni hayo; inachukua miaka kumi na sita hivi kuyarekebisha! Na jambo la kushangaza ni kwamba wazazi ndio walio na jukumu la kufanya hivyo: wao ndio humfanya mtoto awe na maoni hayo, kisha kwa upole wanamfundisha kwamba maoni hayo hayafai.”

Anapofikia umri wa miaka miwili hivi, mtoto anaanza kutambua kwamba maoni yake hayafai mzazi anapoacha kuwa mtunzaji na kuanza kuwa mfundishaji. Sasa mtoto anatambua kwamba wazazi wake hawatii amri yake; badala yake yeye ndiye anayetarajiwa kutii amri yao. Serikali yake imepinduliwa, na huenda asifurahie mabadiliko hayo. Akiwa amekasirika, anajaribu kushikilia mamlaka yake juu ya wazazi. Jinsi gani?

Kukabiliana na Milipuko ya Hasira

Wanapofikia umri wa miaka miwili hivi, tabia za watoto wengi hubadilika sana, hilo likitia ndani kuwa na milipuko ya hasira. Hicho huwa kipindi kigumu sana kwa wazazi. Kwa ghafula, mtoto wako anatumia sana maneno “Hapana!” au “Sitaki!” Huenda akawa na hasira kujielekea au kuwaelekea wazazi wake huku akipambana na hisia zake zinazobadilika-badilika. Anataka kukaa mbali nawe, na wakati huohuo, anataka kuwa karibu nawe. Wazazi waliochanganyikiwa hawajui la kufanya, hawana suluhisho. Tatizo ni nini?

Hebu fikiria mabadiliko makubwa ambayo yametukia katika maisha ya mtoto. Hadi hivi karibuni, alihitaji tu kutoa kilio, na watu wazima walimtimizia mahitaji yake mara moja. Sasa anaanza kutambua kwamba “utawala” wake ulikuwa wa muda tu na sasa itabidi ajifanyie mambo fulani. Pole kwa pole, anaanza kutambua kwamba anapaswa kujitiisha kama Biblia inavyosema: “Watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo.”—Wakolosai 3:20.

Wakati wa kipindi hicho kigumu, wazazi wanapaswa kushikilia mamlaka yao. Wakifanya hivyo kwa uthabiti lakini kwa upendo, mtoto atazoea jukumu lake jipya. Na mambo atakayojifunza yatamsaidia kadiri anavyokua.

Kusitawisha Utu Wake

Wanyama, na hata mashini, zinaweza kutambua maneno na kuiga usemi. Lakini ni mwanadamu peke yake anayeweza kutua na kujichunguza. Kwa hiyo, mtoto anapokuwa na umri wa miaka miwili au mitatu hivi, anakuwa na hisia za kujitutumua, kuaibika, kuhisi hatia, na kadhalika. Hizo ni hatua za kwanza za kuwa mtu mzima mwenye sifa za kiadili—mtu anayeweza kusimama imara na kutetea lililo sawa, hata wengine wanapofanya jambo baya.

Kufikia hatua hiyo, wazazi wanafurahia jambo lingine. Mtoto wao anaanza kujali hisia za wengine. Alipokuwa na umri wa miaka miwili, alikuwa akicheza kando ya wenzake, lakini sasa anacheza pamoja nao. Pia anatambua wakati ambapo wazazi wake wanafurahia jambo fulani, na huenda akataka kuwafurahisha. Kwa hiyo, inaelekea kwamba ataweza kufundishwa kwa urahisi.

Mtoto anapotimia umri wa miaka mitatu anaanza kujifunza yaliyo sawa na yasiyo sawa, mema na mabaya. Ni wazi kwamba huo ndio wakati wa wazazi kuwafundisha watoto wao kuwa watu wazima wanaotegemeka.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Siku chache tu baada ya kuzaliwa, mtoto anajua sauti ya mama yake na anaipenda kuliko sauti ya mtu asiyemfahamu

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Mtoto anapotimia umri wa miaka mitatu anaanza kujifunza yaliyo sawa na yasiyo sawa, mema na mabaya

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

SABABU INAYOMFANYA MTOTO AENDELEE KULIPUKA KWA HASIRA

“Wazazi fulani hudhani kwamba mtoto analipuka kwa hasira kwa sababu hawakumtimizia mahitaji yake,” anaandika John Rosemond, katika kitabu New Parent Power. “Kwa hiyo, wazazi hudhani kwamba ikiwa wao ndio wamesababisha mtoto alipuke kwa hasira, basi lazima warekebishe kosa hilo haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, ikiwa walikuwa wamekataa jambo fulani wanabadili nia mara moja na kulikubali. Au baada ya kumchapa mtoto, wanampa zaidi ya alichotaka, ili wasihisi hatia. Mbinu hiyo hufanikiwa. Mtoto huacha kulipuka kwa hasira, mzazi anatulia, na mtoto anajua kwamba akilipuka kwa hasira atapewa anachotaka, kwa hiyo anatumia mbinu hiyo tena na tena.”