Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Yashambuliwa

Biblia Yashambuliwa

Biblia Yashambuliwa

MAANDISHI yote yanayojulikana kama Biblia, au Maandiko Matakatifu, yaliandikwa katika kipindi cha zaidi ya miaka 1,600. Sehemu ya zamani zaidi ya maandishi hayo iliandikwa na Musa; sehemu ya mwisho iliandikwa na mwanafunzi wa Yesu Kristo aliyekuwa na umri wa karibu miaka 100.

Jitihada za kuwazuia watu wasisome Maandiko zimefanywa kwa muda mrefu sana hata kabla ya Wakati wetu wa Kawaida, katika Enzi za Kati, au hata katika nyakati za kisasa. Rekodi moja ya kale inayoonyesha majaribio hayo ni ile iliyoandikwa na nabii wa Mungu Yeremia, aliyeishi zaidi ya miaka 600 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo.

Ujumbe Usiopendwa na Wengi Washambuliwa

Nabii Yeremia aliongozwa na Mungu kuandika katika kitabu cha kukunjwa ujumbe ulioshutumu wakaaji wa Yuda la kale waliotenda dhambi na kuwaonya kwamba mji wao mkuu, Yerusalemu, ungeharibiwa ikiwa hawangebadili njia zao. Mwandishi wa Yeremia, Baruku, alisoma ujumbe huo kwa sauti, hadharani katika hekalu la Yerusalemu. Aliusoma mara ya pili mbele ya wakuu wa Yuda, nao wakampelekea Mfalme Yehoyakimu kitabu hicho cha kukunjwa. Mfalme alipoyasikia maneno ya Mungu, alikasirika sana. Kwa hiyo, akakikata kile kitabu cha kukunjwa vipande-vipande na kukiteketeza.—Yeremia 36:1-23.

Kisha Mungu akamwamuru Yeremia: “Chukua tena kitabu cha kukunjwa, kingine, nawe uandike juu yake yale maneno yote ya kwanza yaliyokuwa juu ya kile kitabu cha kwanza, ambacho Yehoyakimu mfalme wa Yuda aliteketeza.” (Yeremia 36:28) Miaka 17 hivi baadaye, kama tu Mungu alivyokuwa ametabiri kupitia Yeremia, Yerusalemu liliharibiwa, watawala wake wengi wakauawa, na wakaaji wake wakapelekwa uhamishoni huko Babiloni. Ujumbe uliokuwa ndani ya kitabu hicho cha kukunjwa—pamoja na habari kuhusu kushambuliwa kwa kitabu chenyewe—umeokoka hadi leo katika kitabu cha Biblia cha Yeremia.

Biblia Yaendelea Kuteketezwa

Si Yehoyakimu peke yake aliyejaribu kuliteketeza Neno la Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo. Baada ya kuvunjika kwa Milki ya Ugiriki, Israeli ikawa chini ya utawala wa ukoo wa Seleuko. Antioko Epifane, aliyekuwa Mfalme wa Ukoo wa Seleuko, ambaye alitawala kuanzia 175 hadi 164 K.W.K., alitaka kuunganisha milki yake kwa kutumia utamaduni wa Kigiriki. Ili afanye hivyo, alijaribu kuwalazimisha Wayahudi wakubali maisha, desturi, na dini ya Kigiriki.

Mnamo 168 K.W.K., Antioko alivamia hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Juu ya madhabahu iliyokuwapo, alijenga madhabahu nyingine ili kumtukuza mungu Zeu wa Wagiriki. Pia Antioko aliwakataza Wayahudi wasishike Sabato na akawaamuru wasiwatahiri wana wao. Adhabu ya kutotii ilikuwa kifo.

Njia moja ambayo Antioko alitumia ili kuwafanya Wayahudi wabadili dini ilikuwa kuharibu vitabu vyote vya kukunjwa vilivyokuwa na Sheria. Ingawa Antioko alijaribu kufanya mabadiliko hayo katika Israeli yote, alishindwa kuharibu nakala zote za Maandiko ya Kiebrania. Vitabu fulani vya kukunjwa vilivyofichwa vizuri na Wayahudi waliokuwa Israeli havikuteketezwa, na nakala nyingine za Maandiko Matakatifu zilihifadhiwa na Wayahudi waliokuwa wakiishi katika maeneo mengine.

Amri ya Diokletiani

Mtawala mwingine maarufu aliyejaribu kuharibu Maandiko alikuwa Maliki Mroma Diokletiani. Mnamo 303 W.K., Diokletiani alitoa amri kadhaa zilizosema kwamba Wakristo wateswe vikali. Hilo lilitokeza kile ambacho wanahistoria fulani wamekiita “Yale Mateso Makubwa.” Amri yake ya kwanza iliagiza kwamba nakala zote za Maandiko ziteketezwe na mahali ambapo Wakristo walikutania pabomolewe. Harry Y. Gamble, profesa wa masomo ya dini katika Chuo Kikuu cha Virginia, aliandika hivi: “Diokletiani alijiambia kwamba Wakristo wote, popote walipo, lazima wawe na vitabu kadhaa na alijua kwamba vitabu hivyo ni muhimu ili Wakristo waendelee kuwapo kama jamii.” Mwanahistoria Eusebio wa Kaisaria, huko Palestina, aliyeishi katika kipindi hicho, alisema hivi: “Tulijionea kwa macho yetu wenyewe nyumba za sala zikibomolewa kabisa, na Maandiko yaliyopuliziwa na matakatifu yakiteketezwa sokoni.”

Inasemekana kwamba miezi mitatu baada ya Diokletiani kutoa amri yake, meya wa jiji la Cirta, lililokuwa Afrika Kaskazini na ambalo sasa linaitwa Constantine, aliwaamuru Wakristo wamkabidhi ‘maandishi yao yote ya sheria’ na “nakala za maandiko.” Masimulizi ya kipindi hicho yanaonyesha kwamba kulikuwa na Wakristo walioona ni afadhali kuteswa na kuuawa badala ya kutoa nakala zao za Biblia ziharibiwe.

Kusudi la Mashambulio Hayo

Yehoyakimu, Antioko, na Diokletiani walikuwa na kusudi moja: kuliangamiza Neno la Mungu. Hata hivyo, Biblia iliokoka majaribio yote ya kuliangamiza. Watawala wa Roma baada ya Diokletiani walianza kudai kwamba wao ni Wakristo. Lakini bado mashambulizi dhidi ya Biblia yaliendelea. Kwa nini?

Watawala hao pamoja na viongozi wa kanisa walidai kwamba kusudi la kuiteketeza Biblia halikuwa kuiangamiza. Badala yake wanaume hao walikuwa tu wakijaribu kuwazuia watu wa kawaida wasiipate Biblia. Lakini kwa nini viongozi wa kidini walifanya hivyo? Na kanisa lilifanya jitihada zipi ili kujaribu kuwazuia watu wasiisome Biblia? Acheni tuone.