Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anawajali Wanyama?

Je, Mungu Anawajali Wanyama?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Anawajali Wanyama?

WANYAMA wamo hatarini. Wanasayansi wengi wanasema kwamba wanyama mbalimbali wanatoweka kwa kasi sana. Wanyama wanateseka kwa sababu wanadamu wanazidi kuvamia makao yao. Kutokezwa kwa chakula viwandani, michezo ya wanyama wakipigana, na kuwaacha wanyama-vipenzi bila kujali inaonyesha hali hiyo yenye kusikitisha.

Hata hivyo, watu fulani wanahisi kwamba hali hiyo yenye kusikitisha imesababishwa na kuongezeka kwa idadi ya watu. Lakini je, hivyo ndivyo Mungu alivyokusudia? Je, amewaacha wanyama aliowaumba wateseke mikononi wanadamu? Tunajuaje kwamba Mungu anawajali wanyama?

Aliwajali Tangu Mwanzo

Baada ya Mungu kuumba samaki, ndege, na wanyama, alifurahia kazi yake. Biblia inasema kwamba aliona kuwa uumbaji huo ulikuwa wenye kupendeza. (Mwanzo 1:21, 25) Viumbe hao wote, kuanzia yule mdogo hadi yule mkubwa, walitunzwa kwa upendo na Muumba. Mungu aliwaumba wakiwa na “hekima ya kisilika” na pia akawaandalia chakula ili wasitawi katika mazingira yao ya asili. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: “Wote hao—wanaendelea kukungojea wewe ili uwape chakula chao wakati wa majira yake. Wao huokota kile unachowapa. Unaufungua mkono wako—wanashiba vitu vyema.”—Methali 30:24; Zaburi 104:24, 25, 27, 28.

Ni kweli kwamba Mungu aliwaumba wanyama wajitiishe kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kufikiri au wakiwa na hali ya kiroho. (2 Petro 2:12; Yuda 19) Tofauti na hao, Adamu alikuwa kiumbe wa hali ya juu, aliyeumbwa “kwa mfano wa Mungu.” Angeweza kuiga sifa za Muumba wake, Yehova. (Mwanzo 1:27; Zaburi 83:18) Lakini hilo halikuwapa wanadamu haki ya kuwatendea wanyama kinyume na mapenzi ya Muumba wao.

Kwa mfano, Adamu alianza kuwapa wanyama majina kwa sababu Yehova alimpa pendeleo hilo. Isitoshe, Yehova alimsaidia Adamu kwa “kumletea huyo mtu [wanyama wote] ili aone atawaitaje kila mmoja wao.” (Mwanzo 2:19) Mwanadamu angefanikiwa kuwatunza wanyama iwapo tu angefuata mwelekezo wa Muumba.

Kweli Mungu Anajali!

Kwa kusikitisha, Adamu alimwasi Muumba wake. Uasi wake ulileta matokeo mabaya kwa jamii ya kibinadamu na viumbe wote duniani. Hata hivyo, Muumba alionyesha waziwazi jinsi ambavyo wanyama walipaswa kutendewa. Ingawa hatimaye mwanadamu aliruhusiwa aue wanyama kwa ajili ya chakula na sababu nyingine zinazofaa, Mungu hakuruhusu kamwe kwamba watendewe kikatili. Biblia inasema hivi: “Mwadilifu anatunza nafsi ya mnyama wake wa kufugwa, lakini rehema za waovu ni ukatili.”—Methali 12:10.

Mungu hata alilipa taifa la kale la Israeli sheria kuhusu kuwatunza wanyama. Ule mpango wa kuwa na Sabato, yaani, siku moja ya kupumzika kabisa kila juma, uliwafaidi wanyama wa Waisraeli kwa kuwa wao pia wangepumzika. (Kutoka 23:12) Inapendeza kwamba ingawa hakuna kazi yoyote iliyoruhusiwa kufanywa siku hiyo takatifu, watu walipaswa kusaidia mnyama aliyekuwa taabani. (Luka 14:5) Pia Mungu aliamuru kwamba ng’ombe hawakupaswa kunyimwa chakula walipokuwa wakifanya kazi, na wanyama hawakupaswa kubebeshwa mizigo mizito sana. (Kutoka 23:5; Kumbukumbu la Torati 25:4) Sheria ilikataza kwamba ng’ombe-dume asifungwe nira pamoja na punda ili wasiumizane. (Kumbukumbu la Torati 22:10) Ni wazi kwamba Biblia inafundisha kuwa wanyama wanapaswa kutendewa inavyofaa, kwa heshima, na huruma!

Ingawa watu wengi wanahangaikia mahitaji yao tu na kupuuza jinsi wanyama wanavyoathiriwa, Mungu anawajali kwa huruma. Nabii Yona alipotenda kwa njia isiyo ya rehema wakati wakazi wa Ninawi walipotubu na hivyo kuokoka hukumu ya Mungu, Yehova alimwambia hivi: “Mimi, kwa upande wangu, je, sipaswi kusikitikia Ninawi lile jiji kubwa, ambalo lina wanadamu zaidi ya 120,000 wasiojua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto, na tena wanyama wengi wa kufugwa?” (Yona 4:11) Naam, Muumba aliwahurumia hata wanyama!

Utunzaji wa Wakati Ujao Waahidiwa

Ni wazi kwamba Mungu anajali jinsi wanyama wanavyotendewa. Hata Mwana wake mpendwa Yesu alisema kwamba hakuna shomoro anayeanguka chini bila Baba yake kujua. (Mathayo 10:29) Tofauti na hilo, licha ya jitihada zao za kulinda mazingira, wanadamu hawaelewi kikamili jinsi matendo yao yanavyoathiri mazingira. Ili waweze kuwajali wanyama wa mwituni, wanadamu wanahitaji kubadili jinsi wanavyofikiri.

Jambo la kufurahisha ni kwamba Biblia inaeleza kuhusu wakati ambapo, chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, “dunia hakika itajawa na kumjua Yehova.” (Isaya 11:9) Ujuzi huo utawaelimisha na kuwazoeza wanadamu watiifu ili waitunze dunia vizuri. Muumba atahakikisha kwamba kutakuwa na upatano kati ya mwanadamu na mnyama, na hivyo kurudisha duniani hali ambazo Mungu alikuwa amekusudia hapo awali.

Biblia inaeleza mabadiliko yatakayotukia wakati huo, inaposema: “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao. Na ng’ombe na dubu watakula pamoja; watoto wao watalala pamoja. Na hata simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anayenyonya hakika atacheza juu ya shimo la nyoka; na mtoto aliyeachishwa kunyonya atatia mkono wake juu ya tundu la kupitishia nuru la nyoka mwenye sumu.” Inapendeza kama nini kutafakari juu ya mambo hayo yatakayotukia wakati ujao!—Isaya 11:6-8.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, Mungu anajali jinsi ambavyo wanyama wanatendewa?—Methali 12:10; Mathayo 10:29.

● Je, inawezekana wanadamu na wanyama kuwa na upatano kamili?—Isaya 11:6-9.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Ili kuwajali wanyama wa mwituni, wanadamu wanahitaji kubadili jinsi wanavyofikiri

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]

La Voz de Galicia/Fotógrafo: Víctor Mejuto