Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu cha Pekee Kisichoweza Kuangamizwa

Kitabu cha Pekee Kisichoweza Kuangamizwa

Kitabu cha Pekee Kisichoweza Kuangamizwa

“Hakuna kitabu kingine ambacho kimewahi kupingwa kiasi hicho, lakini kimeokoka mashambulizi yote kutoka kwa watu wenye mamlaka, vipawa, na ustadi wa kusema.”

KWA nini unapaswa kuichunguza Biblia? Sababu moja ni kwamba inadai kuwa ina ujumbe kutoka kwa Mungu kwa ajili ya wanadamu. (2 Timotheo 3:16) Ikiwa hilo ni kweli, yeyote ambaye haisomi anakosa jambo fulani muhimu.

Sababu nyingine ya kuichunguza Biblia ni kwamba ni moja kati ya vitabu vya zamani zaidi na ndicho kitabu ambacho kimetafsiriwa na kusambazwa zaidi kuliko vitabu vingine vyote. Hakuna kitabu kingine ambacho kimeuzwa kwa wingi zaidi ulimwenguni.

Mambo ambayo Biblia inasema, umri wake, na kusambazwa kwake kunapendeza hata zaidi unapofikiria kwamba kumekuwa na majaribio chungu nzima ya kuwazuia watu wasiisome. “Hakuna kitabu kingine ambacho kimewahi kupingwa kiasi hicho; lakini kimeokoka mashambulizi yote kutoka kwa watu wenye mamlaka, vipawa, na ustadi wa kusema,” akasema Albert Barnes, mwanatheolojia wa karne ya 19.

Mwandishi huyo alisema kwamba kwa kawaida watu huvutiwa na kitu chochote ambacho kimeokoka mashambulizi mara nyingi. “Lakini hakuna jeshi ambalo limewahi kuokoka vita vingi kama Biblia,” Barnes anasema, “hakuna ngome yoyote ambayo imewahi kustahimili mashambulizi mengi kama hayo, na kuendelea kusimama licha ya kukabiliwa na madhara ya vita na kupita kwa wakati; na hakuna mwamba ambao umewahi kupigwa na mawimbi mengi kiasi hicho, na bado ukaendelea kusimama mahali pake.”

Hati nyingi za kale zimepotea, zikaharibiwa, au zikasahauliwa, lakini licha ya mashambulizi makali, Biblia imeokoka sikuzote. Watu fulani walipambana, na hata wakahatarisha maisha yao, ili wengine waweze kuipata kwa urahisi. Kwa upande mwingine, wengine waliwanyang’anya wasomaji wenye hamu na kuiteketeza Biblia pamoja na wamiliki wake.

Kwa nini kitabu hicho kimependwa na kuchukiwa sana hivyo? Kimeokoka jitihada zipi za kukiharibu? Ni nani waliojaribu kukiharibu? Zaidi ya yote, kwa nini kimeokoka? Na kwa nini ujumbe wake unakufaa? Kurasa zinazofuata zitajibu maswali hayo.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 2, 3]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MIAKA MUHIMU KATIKA UCHAPISHAJI WA BIBLIA

1513 K.W.K. Biblia inaandikwa katika Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki

–m. 98 W.K.

100 Inaweza kubebwa kwa urahisi ikiwa kodeksi

405 Inatafsiriwa katika Kilatini na Jerome

1380 Inatafsiriwa katika Kiingereza kutoka Kilatini na Wycliffe

1455 Gutenberg anatokeza Biblia ya kwanza iliyochapishwa

1525 Tyndale anaitafsiri katika Kiingereza

1938 Inachapishwa katika lugha zaidi ya 1,000

2011 Inapatikana katika lugha zaidi ya 2,500