Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafsiri ya King James—Jinsi Ilivyokuja Kuwa Maarufu

Tafsiri ya King James—Jinsi Ilivyokuja Kuwa Maarufu

Tafsiri ya King James​—Jinsi Ilivyokuja Kuwa Maarufu

SHEREHE nyingi zilifanywa nchini Uingereza mwaka huu ili kuadhimisha miaka 400 tangu kutolewa kwa tafsiri ya Biblia ya King James, ambayo pia inaitwa Authorized Version. Vipindi vya pekee vya televisheni na redio, na pia mikutano, hotuba, na semina zilifanywa ili kuadhimisha miaka hiyo.

Prince Charles alikuwa mstari wa mbele kusherehekea hazina hii ya kitaifa ambayo iliitwa kwa jina la Mfalme James wa Kwanza wa Uingereza. Lakini, tafsiri hiyo ya King James, iliyochapishwa mnamo Mei 1611, ilikujaje kupendwa na watu wanaozungumza Kiingereza?

Kazi ya Kutafsiri Yapamba Moto

Kufikia katikati ya karne ya 16, watu barani Ulaya walianza kutamani kuelewa mafundisho ya Biblia. Karne mbili hivi mapema, katika mwaka wa 1382, John Wycliffe alikuwa amechochea hamu ya watu ya kusoma Biblia katika lugha yao wenyewe alipotafsiri Biblia katika Kiingereza kutoka Kilatini. Karne mbili zilizofuata, wafuasi wake walioitwa Lollards walisambaza nchini kote maandiko ya Biblia yaliyoandikwa kwa mkono.

Hatua nyingine kubwa ilikuwa kutokezwa kwa tafsiri ya New Testament ya msomi wa Biblia, William Tyndale. Ilitafsiriwa katika Kiingereza kutoka Kigiriki cha awali kufikia mwaka wa 1525. Muda mfupi baadaye, katika mwaka wa 1535, Miles Coverdale alitokeza Biblia nzima katika Kiingereza. Mwaka mmoja kabla ya hapo, Mfalme Henry wa Nane alijitenga na Kanisa Katoliki na akachukua hatua muhimu. Ili kuimarisha cheo chake akiwa kiongozi wa Kanisa la Anglikana, Henry wa Nane aliamuru Biblia itafsiriwe katika Kiingereza. Biblia hiyo ikaja kuitwa Great Bible (Biblia Kuu). Biblia hiyo iliyochapishwa mwaka wa 1539 ilikuwa buku kubwa lililoandikwa kwa herufi nzito za Kigothi.

Wapuriti na Waprotestanti wengine waliokuwa wakimbizi kutoka Ulaya walihamia Geneva, Uswisi. Katika mwaka wa 1560, Geneva Bible (Biblia ya Geneva), Biblia ya kwanza katika Kiingereza iliyokuwa na maandishi rahisi kusoma na ambayo sura zake zilikuwa zimegawanywa katika mistari ilitolewa. Ilitumwa Uingereza kutoka bara Ulaya na ikawa maarufu haraka sana. Hatimaye, mnamo 1576, Geneva Bible ilichapishwa pia nchini Uingereza. Ramani na maelezo ya pambizoni yalimsaidia mtu kuelewa Maandiko. Lakini maelezo hayo yaliwaudhi baadhi ya wasomaji kwa sababu yalimpinga Papa.

Kushinda Magumu

Kwa kuwa Great Bible haikupendwa na watu wengi na Geneva Bible ilikuwa na maelezo ya pambizoni yaliyotokeza ubishi, iliamuliwa kwamba Biblia iliyosahihishwa itokezwe. Tafsiri ya Great Bible ilichaguliwa iwe msingi wa kutafsiri Biblia hiyo. Kazi hiyo ilipewa maaskofu wa Kanisa la Anglikana, na katika mwaka wa 1568 tafsiri ya Bishops’ Bible (Biblia ya Maaskofu) ilichapishwa. Ilikuwa buku kubwa lililojaa picha nyingi. Lakini wafuasi wa Calvin waliochukizwa na majina ya kidini ya cheo hawakupenda matumizi ya neno “bishops” (maaskofu). Kwa sababu hiyo tafsiri ya Bishops’ Bible haikupendwa sana na watu nchini Uingereza.

Baada ya Mfalme James wa Kwanza kutawazwa kuwa mfalme wa Uingereza mwaka wa 1603, * aliidhinisha kwamba Biblia nyingine itafsiriwe. Alisema kwamba ili Biblia hiyo isiwaudhi watu, watafsiri walipaswa kuondoa maelezo yoyote yenye kuudhi.

Mfalme James aliutegemeza mradi huo. Mwishowe, wasomi 47 katika vikundi sita vilivyokuwa sehemu mbalimbali nchini humo walitayarisha baadhi ya maandishi yake. Wakitumia tafsiri ya Tyndale na Coverdale, wasomi hao wa Biblia walisahihisha tafsiri ya Bishops’ Bible. Hata hivyo, walitumia pia tafsiri ya Geneva Bible na tafsiri ya Kikatoliki ya Rheims New Testament ya mwaka wa 1582.

James mwenyewe alikuwa msomi wa Biblia aliyeheshimiwa, na kwa sababu ya mchango wake, tafsiri hiyo ilisemekana kuwa imetolewa kwa heshima ya “James, mkuu aliye na cheo cha juu zaidi na mwenye nguvu.” Akiwa kiongozi wa Kanisa la Anglikana, James alionwa kuwa anatumia mamlaka yake ili kuliunganisha taifa.

Tafsiri Bora Zaidi

Viongozi wa kidini walifurahi kupokea kutoka kwa mfalme wao, Biblia “ambayo iliwekwa rasmi isomwe Makanisani.” Hata hivyo, swali lililobaki ni, Je, taifa hilo litaikubali tafsiri hiyo mpya ya Biblia?

Kwenye dibaji yao ndefu ya awali, watafsiri wa Biblia hiyo waliandika kuhusu wasiwasi wao ikiwa tafsiri hiyo mpya ingekubaliwa. Hata hivyo, Biblia ya King James Version ilikubaliwa na wengi, hata ingawa ilichukua miaka 30 hivi ili watu waanze kupendelea kuisoma badala ya kusoma Geneva Bible.

Kulingana na kitabu The Bible and the Anglo-Saxon People, Biblia ya King James Version ilikuja kuonwa kuwa ndiyo Tafsiri Rasmi (Authorized Version), na ikaja kukubaliwa kwa sababu ya ubora wake. Kitabu The Cambridge History of the Bible kilifikia mkataa huu: “Maandishi yake yalionwa kuwa matakatifu kana kwamba yanatoka kwa Mungu moja kwa moja; kwa Wakristo wengi wanaozungumza Kiingereza, ilionekana kwamba kuchambua maandishi ya King James Version ni sawa na kukufuru.”

Mpaka Miisho ya Dunia

Watu wa kwanza kuhamia Amerika Kaskazini kutoka Uingereza walibeba Geneva Bible. Hata hivyo, baadaye Biblia ya King James Version ilianza kupendwa na wengi huko Amerika. Milki ya Uingereza ilipopanuka na kuenea kote ulimwenguni, wamishonari Waprotestanti walieneza utumizi wa tafsiri hiyo. Kwa kuwa watu wengi waliotafsiri Biblia katika lugha za kienyeji hawakufahamu Kiebrania na Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia, walitafsiri kwa kutumia King James Version katika Kiingereza.

Leo, kulingana na Maktaba ya Uingereza, “Tafsiri ya King James, au Authorised, ndiyo tafsiri iliyochapishwa kwa wingi katika Kiingereza.” Wengine wanakadiria kwamba nakala zaidi ya bilioni moja zimechapishwa ulimwenguni pote!

Wakati wa Mabadiliko

Kwa karne nyingi, wengi wameamini kwamba tafsiri ya King James ndiyo Biblia pekee iliyo ya “kweli.” Katika mwaka wa 1870, kazi ya kusahihisha Biblia hiyo ilianza nchini Uingereza. Baadaye, Biblia iliyotokezwa inayoitwa English Revised Version ilipofanyiwa masahihisho machache nchini Marekani, ilichapishwa ikiwa na jina American Standard Version. * Katika masahihisho yaliyofanywa hivi karibuni, mnamo 1982, dibaji ya Revised Authorised Version inasema kwamba jitihada zilifanywa “ili kudumisha mpangilio mzuri wa kishairi ambao ulipendwa sana katika Authorised Version” ya 1611.

Ingawa Biblia bado ndicho kitabu kinachouzwa kwa wingi ulimwenguni—na tafsiri ya King James ndiyo inayopendwa zaidi—Profesa Richard G. Moulton alisema hivi: “Tumefanya kila kitu tunachoweza kufanya na maandishi haya ya Kiebrania na Kigiriki. . . . Tumeyatafsiri [na] kusahihisha tafsiri hizo . . . Bado kuna jambo moja tunalopaswa kufanya na Biblia: tuisome.”

Pasipo shaka, King James Version ni tafsiri bora sana, ambayo inathaminiwa na kupendwa kwa sababu ya maneno yake yenye kupendeza. Lakini namna gani kuhusu umuhimu wa ujumbe wake? Maandishi ya Biblia yaliyoandikwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu yanafunua suluhisho la kudumu kwa matatizo tunayokabiliana nayo katika siku hizi zenye hatari. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza Biblia haidhuru unapendelea kusoma tafsiri ipi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 James alizaliwa mwaka wa 1566 na katika mwaka wa 1567 akatawazwa kuwa Mfalme James wa Sita wa Scotland. Alipotawazwa kuwa Mfalme James wa Kwanza wa Uingereza katika mwaka wa 1603, akawa mtawala wa nchi zote mbili. Katika mwaka wa 1604, akaanza kutumia jina la cheo “Mfalme wa Uingereza.”

^ fu. 21 Ona sanduku “Biblia ya American Standard Version.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

BIBLIA YA AMERICAN STANDARD VERSION

Biblia ya American Standard Version ilichapishwa katika mwaka wa 1901. Biblia hiyo ilitegemea maandishi ya King James Version. Inasema hivi katika dibaji yake: “Tunaelewa kwamba watu walipendezwa na Authorized [King James] Version kwa sababu ya maneno yake yenye kupendeza. Na hatupuuzi jambo hilo.” Hata hivyo, American Standard Version ilifanya rekebisho fulani muhimu.

Dibaji yake inaeleza hivi: “Baada ya kufanya uchunguzi kwa uangalifu, wasahihishaji wa American Standard Version, walifikia kauli moja kwamba ushirikina wa Wayahudi wa kwamba jina la Mungu ni takatifu sana lisiweze kutamkwa, haupaswi kuathiri tafsiri za Agano la Kale katika Kiingereza au lugha nyingine, kama vile haukuathiri tafsiri kadhaa za wamishonari wa kisasa.”

Si kwamba jina la Mungu, Yehova, halipatikani kabisa katika tafsiri ya King James. Linapatikana katika mistari minne, yaani, Kutoka 6:3; Zaburi 83:18; Isaya 12:2; na Isaya 26:4. Ingawa hivyo, American Standard Version ya 1901 ilirudisha jina hilo katika sehemu 7,000 hivi ambapo linastahili kuwepo.

[Picha]

1901

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

KUSHUGHULIKIA UHITAJI WA PEKEE

Katika mwaka wa 1907, Chapa ya Wanafunzi wa Biblia ya King James Version ilichapishwa nchini Marekani kwa ajili ya Watch Tower Bible and Tract Society. Ilitia ndani nyongeza ndefu iliyoitwa “Kitabu cha Walimu wa Biblia Waberoya.” Baadaye, Mashahidi wa Yehova walichapisha tafsiri ya King James katika matbaa zao wenyewe. Kufikia mwaka wa 1992, Mashahidi walikuwa wamechapisha nakala 1,858,368 za Biblia hiyo.

[Picha]

1907

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

TAFSIRI MUHIMU YA KISASA

Katika muda wa miaka 50 iliyopita, tafsiri nyingi za Biblia zimetolewa (nyingine zimechapishwa katika lugha kadhaa). Watu wengi wanaona Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kuwa tafsiri yenye thamani sana. Nakala zaidi ya milioni 170 za Biblia hiyo zimesambazwa, zikiwa nzima au sehemu, katika lugha 100. Ramani, fahirisi ya maneno yanayofuatana kialfabeti, na nyongeza zimewasaidia wasomaji kuelewa vizuri zaidi ujumbe wa Biblia kwa ajili ya siku zetu.

[Picha]

1961

[Picha katika ukurasa wa 22]

1611

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

Art Resource, NY