Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tsunami ya 2011 Nchini Japani—Masimulizi Kutoka kwa Waokokaji

Tsunami ya 2011 Nchini Japani—Masimulizi Kutoka kwa Waokokaji

Tsunami ya 2011 Nchini Japani​—Masimulizi Kutoka kwa Waokokaji

Soma masimulizi kutoka kwa wale waliookoka tetemeko la nchi huko Japani na tsunami iliyotokea baada ya tetemeko hilo.

IJUMAA, Machi 11, 2011, saa 8:46 alasiri, Japani ilipigwa na tetemeko la nne kwa ukubwa kuwahi kutokea duniani. Tetemeko hilo lilitokeza tsunami kubwa sana pamoja na matetemeko mengine madogo yaliyotokea baadaye ambayo yaliendelea kuwaogopesha watu katika eneo hilo kwa majuma kadhaa. Watu 20,000 hivi walikufa au hawakupatikana. Hata hivyo, maelfu ya watu waliokoka. Yafuatayo ni masimulizi ya baadhi yao.

Tadayuki na mke wake, Harumi, walikuwa nyumbani kwao huko Ishinomaki, Wilaya ya Miyagi, waliposikia mngurumo fulani na nyumba yao ikaanza kutikisika sana. “Tulikimbia nje na tukashangaa kuona ardhi ikiwa imepasuka,” akasema Tadayuki. “Tulitazama nyumba yetu ikisukwasukwa huku na kule na vumbi likitoka ukutani kama moshi.”

Kitovu cha tetemeko hilo kilikuwa umbali wa kilomita 129 kutoka kwenye pwani ya Miyagi. Tsunami hiyo ilitokeza uharibifu kwenye Pwani ya Pasifiki ya Japani katika eneo lenye upana wa kilomita 670. Katika sehemu fulani, mawimbi yenye kimo cha mita 15 yaliipiga fuo, yakivunja vifaa vilivyowekwa ili kuzuia mawimbi na kuingia umbali wa kilomita 40 ndani ya nchi kavu.

Sehemu zinazotokeza umeme, gesi, na maji safi ziliharibiwa kabisa. Maduka, viwanda, na nyumba 160,000 hivi ziliharibiwa au kufagiliwa mbali. Wakati mmoja, watu 440,000 hivi walioathiriwa walikuwa wakiishi katika makao 2,500 ya muda, kama vile shule na vituo vya kijamii. Watu wengine wengi waliishi katika nyumba za watu wa ukoo au marafiki. Makumi ya maelfu ya watu walikufa, lakini kuna maelfu ya miili ambayo haijapatikana.

Vifo na Huzuni

Tsunami iliwaua watu wengi zaidi kuliko waliokufa kutokana na tetemeko la nchi. Yoichi, aliyeishi huko Rikuzentakata, katika Wilaya ya Iwate, alitambua mara moja kwamba tetemeko hilo lingefuatiwa na tsunami, kwa hiyo aliwapeleka wazazi wake kwenye kituo fulani cha kujikinga kilichokuwa karibu. Kisha akarudi kuwatafuta majirani wake. Bado akiwahangaikia wazazi wake, Yoichi pamoja na mke wake, Tatsuko, walitaka kurudi wakawajulie hali lakini wakapata habari kwamba tsunami ilikuwa ikija.

Walikimbilia kituo kingine cha kujikinga lakini hawangeweza kuingia kwa kuwa mlango ulikuwa umezuiwa na vitu vilivyoporomoka. Kisha wakaona jengo jeusi ambalo lilikuwa kiwanda cha kupasulia mbao cha eneo hilo likisukumwa na maji kuwaelekea. “Kimbia!” Tatsuko akasema kwa sauti kubwa.

Mwishowe walifika kwenye uwanja fulani wa shule iliyokuwa katika eneo lililoinuka. Kutoka hapo waliona tsunami ikilifunika eneo lao lote. “Nyumba yangu ndiyo ile inabebwa,” akasema mtu fulani. Karibu robo tatu ya eneo la Rikuzentakata iliharibiwa, na wazazi wa Yoichi wakasombwa na maji hayo. Mwili wa baba yake haukuwahi kupatikana; mwili wa mama yake ulipatikana baadaye.

Toru alikuwa akifanya kazi katika kiwanda fulani karibu na pwani ya Ishinomaki. Tetemeko dogo la kwanza lilipokwisha, alikimbia kwenye gari lake ili aondoke. Aliwaambia wengine kwa sauti kubwa waondoke kwa kuwa alifikiri kwamba huenda tsunami ikafuatilia.

“Kwanza nilitaka kwenda nyumbani kwani nyumba yangu iko katika eneo lililoinuka, lakini nikazuiwa na msongamano wa magari,” Toru akaeleza. “Nilisikia kwenye redio ya gari langu kwamba tayari tsunami ilikuwa imelipiga jiji fulani la karibu. Nilifungua dirisha la gari langu ili niweze kuponyoka iwapo ingefika katika eneo nilimokuwa. Punde si punde, ukuta wa maji ulioinuka kwa mita 2 ukaja mbio kuelekea nilipokuwa. Magari yaliyokuwa mbele yangu yalirushwa na kugonga gari langu, nasi tukabebwa ndani sana kuelekea nchi kavu.

“Nilifaulu tu kutoka kupitia dirisha la gari, lakini nikabebwa na maji mengi yaliyokuwa yamejaa mafuta na yaliyojaa uvundo. Nilibebwa hadi ndani ya duka fulani la kurekebisha magari ambapo nilijishikilia kwenye ngazi fulani na kupanda hadi kwenye orofa ya pili. Kwa jitihada nyingi sana, nilifaulu kuwaokoa watu wengine watatu kutoka majini. Ni watu wachache tu walioweza kuokoka maji hayo yaliyokuwa yakipanda na usiku uliokuwa na baridi na theluji. Lakini tulishindwa kuwaokoa watu wengine waliokuwa wakililia msaada.”

Kabla ya tetemeko hilo, Midori huko Kamaishi, Iwate, alikuwa ametoka tu kuwatembelea babu na nyanya (bibi) yake. Alikuwa tu amehitimu kutoka shule ya sekondari na alikuwa ameenda kumwonyesha babu yake diploma kwa sababu babu alikuwa hajiwezi kwa muda fulani. Alisoma diploma hiyo kwa sauti na kumpongeza Midori kwa bidii yake. Siku tano tu baada ya pindi hiyo yenye kufurahisha, tetemeko la nchi likatokea.

Midori na mama yake, Yuko, waliwasihi babu na nyanya watafute mahali pa kukimbilia, kwa kuwa waliamini kwamba tsunami ingefuatia. Lakini babu yake akasema: “Hapana, mimi siondoki. Tsunami zilizotokea zamani hazikuingia katika nchi kavu kufikia mahali tulipo.” Walijaribu kumtoa nje ya nyumba lakini hawangeweza kumbeba, kwa hiyo wakaenda kutafuta msaada. Hata hivyo, kufikia wakati huo tsunami ilikuwa imefika ufuoni. “Harakisheni! Kimbieni!” wakasema wanaume fulani waliokuwa kwenye mlima hapo karibu. Tsunami ilikuwa ikiipiga nyumba moja baada ya nyingine. Midori alipiga mayowe, “Babu! Nyanya!” Mwili wa babu yake ulipatikana baadaye, lakini nyanya yake hakuwahi kupatikana.

Jitihada za Kutoa Msaada

Mara moja, serikali ya Japani iliwatuma wazima-moto, polisi, na wanajeshi kutoka sehemu zote za Japani. Katika muda mfupi tu, zaidi ya watu 130,000 walikuwa wakifanya kazi ya kutoa msaada. Baada ya muda, msaada ulifika kutoka nchi nyingine na kutoka kwa mashirika ya kimataifa. Vikundi vya kuokoa uhai na madaktari walifika upesi. Waliwatafuta waokokaji, wakawapa matibabu, na wakaondoa vitu vilivyoporomoka.

Mashirika kadhaa yaliwasaidia watu wao. Mashahidi wa Yehova walifanya hivyo pia. Punde baada ya tetemeko la nchi na tsunami kutokea Ijumaa alasiri, Mashahidi walianza kuwatafuta wale ambao wanakutana pamoja nao kwa ajili ya ibada. Hata hivyo, katika sehemu nyingi barabara hazingeweza kupitika, na huduma za umeme na za simu zilikuwa zimekatwa. Ilikuwa vigumu sana kuwapata watu katika eneo hilo kubwa lililoathiriwa.

Takayuki, mmoja wa wazee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova huko Soma, Wilaya ya Fukushima, angeweza kuwasiliana na familia chache tu alasiri hiyo ya Ijumaa. “Niliamua kuwatafuta wengine siku iliyofuata,” akasema. “Alfajiri, nilienda kwa gari kisha nikaenda kwa miguu ili kuwatafuta na nikaendelea hadi jioni. Nilienda kwenye maeneo 20, kutia ndani vituo mbalimbali, ili kuwatafuta washiriki wa kutaniko. Nilipowapata, nilisoma maandiko na kusali pamoja nao.”

Shunji, huko Ishinomaki, anaeleza: “Tulianzisha vikundi mbalimbali vya kuwatafuta waumini wenzetu. Tulipofika kwenye eneo lililokumbwa na msiba tulibaki mdomo wazi. Magari yalikuwa yakining’inia juu ya milingoti ya umeme, nyumba zilikuwa zimelaliana, na marundo ya maporomoko yalikuwa makubwa kuliko nyumba zenyewe. Juu ya gari moja, tuliona mwili wa mtu, ambaye huenda alishindwa kustahimili baridi ya usiku. Gari lingine lilikuwa likining’inia juu chini katikati ya nyumba mbili. Kulikuwa na mwili wa mtu ndani yake.”

Shunji alifurahi kuwapata waumini wenzake katika vituo mbalimbali. “Nilipowaona,” anasema, “nilitambua jinsi ninavyowapenda sana.”

“Mmekuja Haraka Sana!”

Wasichana wawili Mashahidi, Yui na Mizuki, walikuwa majirani huko Minamisanriku, Miyagi. Tetemeko la kwanza lilipokwisha, walikimbia nje na wakakutana. Walikimbilia eneo lililoinuka. Hazikupita dakika kumi walipoona mji wote, kutia ndani nyumba zao, ukifagiliwa na wimbi moja baada ya lingine.

Yui na Mizuki waliwapata marafiki ambao ni Mashahidi katika kituo fulani na wakasali pamoja. Siku iliyofuata, washiriki wa kutaniko lao na wengine wa kutaniko jirani walisafiri kuvuka mlima ili kuwaletea chakula na vitu vingine. Yui na Mizuki wakasema, “Tulijua mtakuja, lakini mmekuja haraka sana!”

Hideharu, mmoja wa waangalizi wa Mashahidi katika Kutaniko la Tome alitembelea kituo hicho. Anaeleza hivi: “Usiku mzima nilijaribu kuwatafuta ndugu zetu wanaoishi ufuoni. Mwishowe, saa 10 usiku nikapata habari kuhusu shule fulani ambako watu walikuwa wamekimbilia. Saa moja asubuhi, tukiwa kikundi cha watu kumi tulikutana ili kupika wali na mimi pamoja na wengine wawili tuliondoka kwa gari ili kupeleka chakula hicho. Barabara nyingi hazingeweza kupitika. Baada ya jitihada nyingi, tulifika kwenye shule hiyo. Hata wale waliokuwa wamepoteza nyumba zao waliungana nasi kuwasaidia wengine.”

Kutosheleza Uhitaji wa Kiroho

Mashahidi wa Yehova hukutana kwa ukawaida ili kujifunza Biblia, na makutaniko mengine hukutana Ijumaa usiku ili kufanya hivyo. Huko Rikuzentakata wao hukutana jioni hiyo; hata hivyo, Jumba la Ufalme—jengo ambalo Mashahidi hutumia kwa ajili ya mikutano yao—lilikuwa limefagiliwa na tsunami. “Si tufanye mkutano,” akasema Shahidi mmoja. Kwa hiyo, nyumba moja ambayo haikuwa imeharibiwa sana ikachaguliwa, na washiriki wa kutaniko wakajulishwa.

Ingawa umeme ulikuwa umekatwa, jenereta ilitumiwa kutokeza mwangaza. Watu kumi na sita walihudhuria. “Tulilia kwa shangwe,” anakumbuka kijana anayeitwa Yasuyuki, ambaye nyumba yake ilisombwa na tsunami hiyo. “Hilo ndilo lililokuwa kimbilio bora zaidi kwetu.” Hideko anasema: “Matetemeko mengine madogo yaliyotukia baadaye yalitusumbua mkutano ulipokuwa ukiendelea, lakini tulipokuwa pamoja, nilisahau hofu na wasiwasi niliokuwa nao.”

Tangu wakati huo, kutaniko hilo halijakosa kamwe kufanya hata mkutano mmoja. Siku mbili baadaye, Jumapili, kichwa cha hotuba ya watu wote iliyochaguliwa kwa ajili ya siku hiyo kilikuwa “Udugu wa Ulimwenguni Pote Waokolewa Kutoka Afa.”

Kazi ya Kutoa Msaada kwa Utaratibu

Mashirika kadhaa ya serikali yalianza kazi ya kutoa msaada, na pia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ambayo inapatikana huko Ebina, karibu na Tokyo, ilianza kufanya hivyo. Kufikia Jumamosi, siku iliyofuata tetemeko la nchi, ofisi ya tawi ilikuwa imegawanya eneo kubwa lililokumbwa na tetemeko hilo katika sehemu tatu. Jumatatu, siku tatu baada ya tetemeko hilo la nchi, wawakilishi kutoka kwenye ofisi ya tawi walitembelea maeneo hayo.

Jitihada za kutoa msaada ziliendelea kwa majuma na miezi kadhaa iliyofuata. Tani nyingi za msaada zilizotolewa na Mashahidi zimegawanywa. Wakati mmoja kulikuwa na vituo 3 vya kutoa msaada, mabohari 21 na vituo vingine vilikuwa vikitoa msaada uliohitajika. Katika miezi miwili ya kwanza, mamia ya wajitoleaji waligawa zaidi ya tani 250 za chakula, mavazi, na vitu vingine vilivyohitajika. Mashahidi wengi waliwagawia majirani wao vitu walivyopata.

Washiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Rikuzentakata na kutaniko jirani la Ofunato wanatumia Jumba lao la Ufalme lililojengwa upya ili kuwaimarisha watu kiroho. Hilo litawasaidia watu kukabiliana na magumu wanayopata wakijaribu kuanza upya maisha yao na kupona kutokana na huzuni waliyopata kutokana na tetemeko la nchi na tsunami hiyo. Kati ya Mashahidi zaidi ya 14,000 wanaoishi katika eneo lililokumbwa na msiba, 12 walikufa na 2 hawajawahi kupatikana.

Wengi kati ya Mashahidi wa Yehova walioathiriwa na msiba huo mkubwa walisema maneno kama haya yaliyosemwa na familia moja: “Tulipokimbia, kila mmoja wetu alikuwa na mfuko mmoja tu. Lakini mahitaji yetu yote yalishughulikiwa na waumini wenzetu.” Inafurahisha kama nini kwamba watumishi wa Mungu wa kweli, Yehova, wanaweza kufurahia undugu wa ulimwenguni pote ambao Yesu na mitume wake walizungumzia! Undugu huo hauwezi kuvunjwa na tsunami au msiba mwingine wowote wa asili.—Yohana 13:34, 35; Waebrania 10:24, 25; 1 Petro 5:9.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

MSIBA WA NYUKLIA ULIOFUATA

Ulimwenguni pote, watu walipata habari kuhusu kuharibika kwa vinu katika mtambo wa nguvu za nyuklia huko Fukushima Daiichi. Gesi zenye sumu na mnururisho ulienea kotekote Japani na katika nchi nyingine. Maelfu ya watu walihamishwa kwa sababu ya uwezekano wa kuathiriwa na mnururisho hatari.

“Nyumba yetu ilikuwa karibu na mtambo wa nguvu za nyuklia,” anaeleza Megumi. “Siku moja baada ya tetemeko hilo, tulisikia kuhusu uharibifu uliotukia kwenye mtambo wa nguvu za nyuklia na tukaamriwa tuondoke.” Dada yake anayeitwa Natsumi anakumbuka, “Helikopta zilikuwa zikiruka kila mahali, ving’ora vya magari ya kushughulikia hali za dharura vilikuwa vikivuma, na mtangazaji fulani alikuwa akisema kwa sauti kwamba tunapaswa kuondoka mara moja.” Katika majuma yaliyofuata, walihamia sehemu tisa tofauti. Mwishowe, wasichana hao waliruhusiwa kurudi nyumbani kwa saa mbili tu ili kuchukua vitu vichache.

Chikako, aliye na umri wa miaka 60 hivi, alikuwa huko Namie, Fukushima. “Tetemeko hilo lilipotukia, nilienda kwenye kituo cha kujikinga kilichokuwa karibu. Mimi pamoja na watoto wangu wawili tulikaa huko usiku mzima lakini hatukuweza kupata usingizi kwa sababu ya matetemeko madogo yaliyofuatia yaliyokuwa na nguvu. Siku iliyofuata saa moja asubuhi, tuliambiwa tuhamie mara moja kwenye kituo kingine kilichokuwa katika jiji lingine.

“Kulikuwa na msongamano wa magari barabarani, kwa hiyo tulifika huko mwendo wa saa tisa alasiri. Tukiwa huko, tulisikia kuhusu mlipuko wa mtambo wa nguvu za nyuklia. Nilifikiri kwamba tungerudi nyumbani baada ya muda mfupi, kwa hiyo hatukutoka na chochote.” Yeye na familia yake walihama kutoka mahali pamoja hadi pengine hadi walipopata nyumba fulani mbali na kwao.

[Hisani ya Picha]

Photo by DigitalGlobe via Getty Images

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

MAMBO AMBAYO SOTE TUNAWEZA KUJIFUNZA

Yoichi, anayeishi Rikuzentakata, aliyetajwa awali na ambaye alipoteza mali nyingi, alisema, “Nimejionea wazi kwamba vitu vya kimwili haviwezi kukulinda.” Maneno hayo yamesemwa kwa muda mrefu na watumishi wa Mungu, hasa wale ambao wamejifunza mambo ambayo Yesu alifundisha. Alieleza kwamba vitu vya kimwili havina faida kubwa kama kupata kibali na baraka za Mungu.—Mathayo 6:19, 20, 33, 34.

Jambo lingine tunalojifunza ni kwamba tunapaswa kutenda haraka maonyo yanapotolewa. Huo ni uamuzi wa kufa na kupona. Watu nchini Japani waliokimbia upesi kwenye maeneo ya juu waliookoka.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 16]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

JAPANI

TOKYO

Kamaishi

Rikuzentakata

Minamisanriku

Ishinomaki

Soma

Mtambo wa nguvu za nyuklia huko Fukushima

Ebina

Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova

[Picha]

Soma, Fukushima

Rikuzentakata, Iwate

Ishinomaki, Miyagi

Kamaishi, Iwate

Minamisanriku, Miyagi

[Picha katika ukurasa wa 14]

Harumi na Tadayuki

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yoichi na Tatsuko

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yuko na Midori

[Picha katika ukurasa wa 17]

Toru

[Picha katika ukurasa wa 17]

Gari ambalo Toru alikuwa akiendesha

[Picha katika ukurasa wa 17]

Takayuki

[Picha katika ukurasa wa 18]

Shunji

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mizuki na Yui

[Picha katika ukurasa wa 19]

Hideharu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wafanyakazi wakitoa msaada

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jumba la Ufalme la Rikuzentakata baada ya “tsunami”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kazi ya ujenzi miezi mitatu baadaye

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jumba la Ufalme lililokamilishwa

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 14]

JIJI PRESS/AFP/Getty Images