Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu

Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu

Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu

KADIRI wakati ulivyopita, jitihada zilifanywa ili kuitafsiri Biblia katika lugha ambazo watu walizungumza kwa ukawaida. Ni wachache tu ambao wangeweza kusoma Biblia katika lugha zake za awali za Kiebrania au Kigiriki. Ingekuwa vigumu kwa wengi wetu kuelewa Neno la Mungu ikiwa leo lingepatikana katika lugha hizo za kale tu.

Karibu miaka 300 kabla ya Yesu kuishi duniani, kazi ilianza ya kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki. Tafsiri hiyo inajulikana kama Septuajinti ya Kigiriki. Miaka 700 hivi baadaye, Jerome alitokeza tafsiri maarufu inayojulikana kama Vulgate. Hiyo ilikuwa tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania na Kigiriki katika Kilatini, lugha iliyokuwa ikitumiwa kwa ukawaida katika Milki ya Roma wakati huo.

Baadaye, Kilatini kiliacha kuwa lugha ya kawaida. Ni watu wenye elimu tu walioendelea kutumia Kilatini, na Kanisa Katoliki lilipinga mbinu za kutafsiri Biblia katika lugha nyingine. Viongozi wa kidini walisisitiza kwamba Biblia ilifaa tu kuwa katika lugha ya Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini. *

Migawanyiko Katika Kanisa na Kutafsiriwa kwa Biblia

Katika karne ya tisa W.K., Methodius na Cyril, wamishonari Wathesalonike waliokuwa wametumwa na Kanisa la Mashariki huko Byzantium, walipendekeza kwamba Kislavonia kitumiwe katika kanisa. Kusudi lao lilikuwa kuwawezesha watu wa Slavonia wa Ulaya Mashariki kujifunza kumhusu Mungu katika lugha yao wenyewe kwa kuwa hawakuelewa Kigiriki au Kilatini.

Hata hivyo, wamishonari hao walikabili upinzani mkali kutoka kwa makasisi Wajerumani, ambao walijaribu kulazimisha kwamba Kilatini kitumiwe ili kuzuia Ukristo wa Byzantium usienee. Kwa wazi, siasa zilikuwa muhimu kwao kuliko watu kupata elimu ya kidini. Mizozo kati ya sehemu ya Magharibi na ya Mashariki ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ulifanya Kanisa Katoliki na Kanisa la Othodoksi la Mashariki zigawanyike katika mwaka wa 1054.

Kuzuia Biblia Isitafsiriwe

Mwishowe, Kanisa Katoliki likaanza kuona Kilatini kuwa lugha takatifu. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1079 Vratislaus, dyuki wa Bohemia, alipoandika barua akiomba ruhusa ya kutumia Kislavonia katika ibada kanisani, Papa Gregory wa Saba alimjibu hivi: “Hatuwezi kwa njia yoyote kukubali ombi hili.” Kwa nini?

“Kwa wale wanaochunguza jambo hili kwa uangalifu,” akasema Gregory, “ni wazi kwamba ilimpendeza Mungu kufanya sehemu fulani ya Maandiko Matakatifu isieleweke kabisa kwa sababu, ikiwa kila mtu angeelewa kila kitu, basi [Maandiko] yangefanywa kuwa ya kawaida tu na kuvunjiwa heshima au watu wasio na akili nyingi wangeyaelewa vibaya na hivyo waasi.”

Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, na ilipaswa kuwa hivyo. Msimamo huo uliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu ya watu wa kawaida. Hawakutaka watu wa kawaida wachunguze mambo ambayo waliona kuwa ni ya makasisi tu.

Mnamo 1199, Papa Innocent wa Tatu aliandika kuhusu watu walioonwa kuwa wazushi ambao walitafsiri Biblia katika Kifaransa na wakaamua kuwa na mazungumzo kati yao kuihusu. Innocent alitumia maneno haya ya Yesu kuwahusu: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” (Mathayo 7:6) Kwa nini alikuwa na maoni hayo? “Ili mtu wa kawaida na ambaye hana elimu asiwe na kimbelembele cha kujifunza Maandiko matakatifu yaliyotukuka, au kuwahubiria watu kuyahusu.” Mara nyingi, wale waliopinga amri ya papa walipelekwa kwa watesaji ambao waliwalazimisha waungame kwamba wao ni wazushi. Wale waliokataa kukana msimamo wao waliteketezwa wakiwa hai.

Wakati wa kile kipindi kirefu cha kuwazuia watu wasiipate na kuisoma Biblia, barua ya Papa Innocent ilitumiwa mara nyingi ili kutetea wazo la kwamba Biblia haipaswi kutumiwa wala kutafsiriwa katika lugha nyingine. Punde tu baada ya amri yake kutolewa, Biblia katika lugha nyingine zikaanza kuteketezwa, na pia watu fulani waliomiliki Biblia waliteketezwa. Katika karne zilizofuata, maaskofu na watawala wa nchi za Ulaya zilizokuwa chini ya udhibiti wa Kanisa Katoliki walitumia njia yoyote waliyoweza ili kuhakikisha kwamba marufuku yaliyowekwa na Papa Innocent wa Tatu yalifuatwa.

Viongozi wa Kanisa Katoliki walijua kwamba mafundisho mengi ya dini hiyo hayakutegemea Biblia bali yalitegemea mapokeo ya kanisa. Bila shaka, hiyo ilikuwa sababu moja iliyowafanya wawazuie waumini wao wasiipate Biblia. Iwapo wangeisoma basi wangetambua kwamba mafundisho ya kanisa yalipingana na Maandiko.

Matokeo ya Yale Mabadiliko Makubwa ya Kidini

Uprotestanti ulibadili hali ya kidini barani Ulaya. Majaribio ya Martin Luther ya kuleta mabadiliko katika Kanisa Katoliki na kujitenga kwake katika mwaka wa 1521 kulitegemea hasa uelewaji wake wa Maandiko. Kwa hiyo, utengano huo ulipokamilika, Luther, aliyekuwa mtafsiri mwenye kipawa, alijitahidi kuifanya Biblia ipatikane kwa watu wote.

Tafsiri ya Luther ya Kijerumani na usambazaji wake ulivuta fikira za Kanisa Katoliki, ambalo liliona kwamba umaarufu wa Biblia ya Luther ulipaswa kufunikwa kwa kutokeza Biblia nyingine iliyokubaliwa na kanisa. Tafsiri mbili za aina hiyo katika Kijerumani zilitokezwa upesi baada ya hapo. Lakini, mnamo 1546, baada ya miaka isiyozidi 25, Baraza la Trent la Kanisa Katoliki, liliamua kwamba kuchapishwa kwa vichapo vyovyote, kutia ndani tafsiri za Biblia, hakupaswi kufanywa bila idhini ya kanisa.

Baraza la Trent liliagiza kwamba “kuanzia sasa Maandiko matakatifu . . . yatachapishwa kwa njia sahihi iwezekanayo; na kwamba itakuwa kinyume cha sheria kwa yeyote kuchapisha, au kumlipa mtu achapishe, vitabu vyovyote kuhusu mambo matakatifu bila jina la mwandishi kuonyeshwa; au kuviuza wakati ujao, au kuvimiliki, isipokuwa kwanza viwe vimechunguzwa na kuidhinishwa [na askofu wa eneo hilo].”

Mnamo 1559, Papa Paul wa Nne alichapisha orodha ya kwanza ya vitabu vilivyopigwa marufuku na Kanisa Katoliki. Orodha hiyo ilikataza mtu kuwa na tafsiri za Biblia za Kifaransa, Kihispania, Kiholanzi, Kiingereza, Kiitaliano, na Kijerumani, kutia ndani tafsiri fulani za Kilatini. Watu wowote waliotaka kusoma Biblia waliambiwa wapate idhini iliyoandikwa kutoka kwa maaskofu au watesaji—jambo ambalo hakuna mtu angetaka kufanya kwani angeshukiwa kuwa mzushi.

Watu waliojaribu kumiliki au kugawa Biblia katika lugha za kawaida katika eneo lao walilazimika kukabiliana na hasira ya Kanisa Katoliki. Wengi walikamatwa, wakateketezwa kwenye mti ulio wima au juu ya mti uliolazwa, wakahukumiwa kifungo cha maisha, au wakapelekwa kwenye meli wakafanye kazi ngumu ya kupiga makasia. Biblia zilizokusanywa ziliteketezwa. Makasisi Wakatoliki waliendelea kukusanya na kuteketeza Biblia hadi kufikia karne ya 20.

Hilo halimaanishi kwamba Waprotestanti wamekuwa na mtazamo tofauti au wameitetea Biblia. Katika karne ya 18 na 19, baadhi ya wanatheolojia Waprotestanti walianza kutumia mbinu ya kujifunza Biblia ambayo baadaye ilikuja kuitwa uchambuzi wa Biblia. Kadiri muda ulivyopita, watu wengi walikubali nadharia za Darwin kwamba uhai haukuumbwa bali ulijitokeza wenyewe kwa njia fulani na kupitia mageuzi ukawa bora bila msaada wa Muumba.

Wanatheolojia, na hata makasisi wengi, walifundisha kwamba Biblia ilitegemea hasa hekaya. Kwa sababu hiyo, si ajabu leo kuwasikia makasisi Waprotestanti, kutia ndani wengi wa wafuasi wao, wakisema kwamba Biblia si sahihi kihistoria.

Huenda umesikia watu wakisema kwamba Biblia si sahihi, na huenda umeshangazwa na majaribio yaliyofanywa ili kuiangamiza katika karne zilizopita. Hata hivyo, majaribio hayo yalishindwa. Biblia iliokoka!

Kwa Nini Imeokoka?

Ni kweli kwamba watu wengi wameonyesha kuwa wanaipenda Biblia na wamekuwa tayari kufa ili kuitetea. Hata hivyo, kuokoka kwake kunategemea nguvu kubwa zaidi kuliko upendo wa wanadamu. Biblia imeokoka kwa sababu wote ambao waliandika Biblia waliongozwa na roho ya Mungu.—Isaya 40:8; 1 Petro 1:25.

Kusoma na kufuata kile ambacho Biblia inasema kutatusaidia kuboresha maisha, afya, na familia zetu. Mungu anataka Biblia iokoke na itafsiriwe katika lugha nyingi kadiri inavyowezekana ili wote wapate nafasi ya kujifunza jinsi wanavyoweza kumpenda, kumtumikia, na hatimaye kufurahia baraka zake za milele. Bila shaka, sisi sote tunatamani mambo hayo!

Yesu alisema hivi katika sala kwa Baba yake wa mbinguni: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Biblia—yale Maandiko ambayo Yesu alisoma na kufundisha—ndiyo njia ya Mungu ya kujibu maswali ambayo watu wanyoofu huuliza.

Unatiwa moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu ujumbe wa Mungu kwa wanadamu unaopatikana katika Biblia. Mashahidi wa Yehova, wanaotokeza gazeti hili, watafurahi kukusaidia kufanya hivyo. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Inaonekana kwamba wazo hilo lilitokana na maandishi ya askofu Mhispania, Isidore wa Seville (560-636 W.K.), aliyesema hivi: “Kuna lugha tatu takatifu, Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini, na hizo ndizo lugha kuu ulimwenguni pote. Sababu ni kwamba shtaka dhidi ya Bwana lililoandikwa juu ya msalaba na Pilato lilikuwa katika lugha hizo tatu.” Bila shaka, uamuzi wa kuandika shtaka hilo katika lugha hizo tatu ulifanywa na Waroma wapagani. Uamuzi huo haukutoka kwa Mungu.

^ fu. 28 Unaweza kuwasiliana nao bila masharti, kwa kutumia anwani moja kati ya zile zilizoonyeshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili au kupitia Tovuti ya www.watchtower.org.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, jambo ambalo liliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu yao

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Watu waliojaribu kumiliki au kugawa Biblia walipokamatwa, waliteketezwa kwenye mti au wakahukumiwa kifungo cha maisha

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

MAJIBU YA BIBLIA

Muumba anataka tupate majibu ya maswali haya ya msingi:

● Kwa nini tuko hapa?

● Kwa nini watu wanateseka sana?

● Wafu wako wapi?

● Wanadamu wanaelekea wapi?

Biblia inajibu maswali haya na kutoa mashauri ya jinsi tunavyoweza kupata furaha ya kweli.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 6]

PINDI AMBAPO BIBLIA ILISHAMBULIWA

m. 636 W.K.

Isidore wa Seville anadai kwamba Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini ni lugha “takatifu” kwa hiyo ndizo lugha ambazo Biblia Takatifu inapaswa kutafsiriwa

1079

Papa Gregory wa Saba anakataa katakata ombi la Vratislaus la kutumia Kislavonia kanisani, akisema kwamba watu “wasio na akili nyingi” hawapaswi kuwa na Maandiko

1199

Papa Innocent wa Tatu anasema kwamba wote wanaojaribu kutafsiri au kuwa na mazungumzo kuhusu Biblia ni wazushi. Wale wanaopinga amri ya papa wanateswa na kuuawa

1546

Kwa amri ya Baraza la Trent, uchapishaji wowote wa tafsiri za Biblia unapaswa kwanza kuidhinishwa na Kanisa Katoliki

1559

Papa Paul wa Nne anawazuia watu wasiwe na Biblia katika lugha za kawaida. Tafsiri za lugha za kienyeji zinakusanywa na kuteketezwa, na mara nyingi watu waliteketezwa pamoja na Biblia walizomiliki

[Hisani ya Picha]

Pope Gregory VII: © Scala/White Images/Art Resource, NY; Pope Innocent III: © Scala/Art Resource, NY; Council of Trent: © Scala/White Images/Art Resource, NY; Pope Paul IV: © The Print Collector, Great Britain/HIP/Art Resource, NY

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

From Foxe’s Book of Martyrs