Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Sababu Zinazotetea Ushoga?

Je, Kuna Sababu Zinazotetea Ushoga?

Maoni ya Biblia

Je, Kuna Sababu Zinazotetea Ushoga?

USHOGA unaendelea kukubaliwa katika nchi nyingi. Kikundi fulani katika kanisa moja nchini Marekani kinasema kwamba maoni ya Biblia kuhusu ushoga yanapaswa kufafanuliwa upya yapatane na “uelewaji wa kisasa.” Kasisi mmoja huko Brazili ambaye hivi majuzi alimwoa mwanamume mwenzake alisema kwamba “Biblia inapaswa kuchunguzwa upya,” ili iruhusu maoni ya kisasa ya kanisa lake.

Kwa upande mwingine, watu ambao hawakubaliani na ushoga wanaonwa kuwa watu wanaowachukia mashoga au wenye ubaguzi. Biblia inasema nini hasa kuhusu ushoga?

Biblia Inasema Nini?

Biblia haikubaliani na watu wanaowabagua watu wengine. Hata hivyo, inaeleza waziwazi maoni yake kuhusu matendo ya ushoga.

“Usilale na mwanamume kama vile unavyolala na mwanamke. Ni jambo lenye kuchukiza.”​Mambo ya Walawi 18:22.

Sheria hiyo ambayo ni sehemu ya Sheria ya Musa ilikuwa mojawapo ya sheria kuhusu maadili ambazo zilipewa hasa taifa la Israeli. Hata hivyo, amri hiyo inaeleza maoni ya Mungu kuhusu matendo ya ushoga, iwe yanafanywa na Wayahudi au watu wasio Wayahudi, inaposema hivi: “Ni jambo lenye kuchukiza.” Mataifa yaliyozunguka Waisraeli yalikuwa na mazoea ya ushoga, ngono kati ya watu wa familia, uzinzi, na matendo mengine yaliyokatazwa na Sheria. Kwa sababu hiyo, Mungu aliyaona mataifa hayo kuwa si safi. (Mambo ya Walawi 18:24, 25) Je, maoni ya Biblia yalibadilika wakati wa Ukristo? Hebu ona andiko lifuatalo:

“Mungu aliwaacha katika hamu za ngono yenye kufedhehesha, kwa maana wanawake wao walibadili matumizi yao wenyewe ya asili kuwa yale yaliyo kinyume cha asili; na vivyo hivyo pia hata wanaume waliacha matumizi ya asili ya mwanamke na kuwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekeana wao wenyewe, wanaume kwa wanaume, wakitenda mambo machafu.”Waroma 1:26, 27.

Kwa nini Biblia inasema kwamba ushoga ni kinyume cha asili na ni uchafu? Kwa sababu ushoga unahusisha matendo ya ngono ambayo Muumba wetu hakukusudia. Ushoga hautokezi watoto. Biblia inalinganisha ushoga na matendo ya kingono ambayo malaika waasi, ambao walikuja kuwa roho waovu, walifanya na wanawake kabla ya Gharika ya siku za Noa. (Mwanzo 6:4; 19:4, 5; Yuda 6, 7) Kwa maoni ya Mungu, matendo yote mawili ni kinyume na asili.

Je, Kuna Sababu Zinazotetea Ushoga?

Huenda watu fulani wakauliza, ‘Je, chembe za urithi, mazingira, au mambo yaliyompata mtu maishani, kama vile kutendewa vibaya kingono, yanaweza kutumiwa kutetea ushoga?’ La, hayawezi. Fikiria mfano huu: Huenda mtu akarithi kile ambacho wanasayansi wanasema ni mwelekeo wa kutumia kileo vibaya, au huenda alilelewa katika familia ambayo ilikuwa kawaida kwa watu kutumia kileo vibaya. Kwa kweli, watu wengi wangemhurumia mtu aliye katika hali hiyo. Lakini hawangemtia moyo aendelee kutumia kileo vibaya au aache kujitahidi kupambana na zoea hilo eti kwa sababu tu alizaliwa akiwa na mwelekeo huo au alilelewa katika mazingira hayo.

Vivyo hivyo, ingawa Biblia haishutumu watu wanaopambana na tamaa za ushoga, haiungi mkono kabisa wale wanaojihusisha katika ushoga, iwe ni kwa sababu ya chembe za urithi au sababu nyingine. (Waroma 7:21-25; 1 Wakorintho 9:27) Badala yake, Biblia inatoa msaada unaofaa na kitia-moyo ili kuwasaidia watu washinde zoea la ushoga.

Mapenzi ya Mungu Ni Nini kwa Watu Wenye Tamaa za Ushoga?

Biblia inatuhakikishia kwamba mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Ingawa Biblia inashutumu matendo ya ushoga, haiwatii watu moyo wawachukie mashoga.

Maoni ya Mungu kuhusu ushoga hayawezi kupunguzwa uzito. Kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10, Biblia inasema waziwazi kwamba “wanaume wanaolala na wanaume” ni kati ya watu ambao “hawataurithi ufalme wa Mungu.” Lakini mstari wa 11 unaongezea wazo hili lenye kufariji: “Na bado wengine wenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.”

Ni wazi kwamba wale waliotaka kweli kumwabudu Mungu kulingana na matakwa yake walikaribishwa katika kutaniko la Kikristo la mapema. Ndivyo ilivyo hata leo kwa watu wote wenye mioyo minyofu ambao wanatafuta kibali cha Mungu​—si kwa kuifafanua upya Biblia—​bali kwa kupatanisha maisha yao na Biblia.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Biblia ina maoni gani kuhusu matendo ya ushoga?​—Waroma 1:26, 27.

● Je, Biblia inawabagua watu wenye tamaa za ushoga?​—1 Timotheo 2:4.

● Je, mtu anaweza kuepuka ushoga?​—1 Wakorintho 6:9-11.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Je, maoni ya Mungu kuhusu ushoga yanapaswa kufafanuliwa upya?