Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushinikizwa Usiwe Mnyoofu

Kushinikizwa Usiwe Mnyoofu

Kushinikizwa Usiwe Mnyoofu

“Kuwa mnyoofu katika biashara ni zoea la kale lililopitwa na wakati, na wale wanaojaribu kulifuata hawatafanikiwa.”​—Stephen, Marekani.

JE, UNAKUBALIANA na maneno hayo? Inakubalika kwamba mara nyingi watu hufaidika kwa kukosa kuwa wanyoofu​—angalau kwa muda mfupi. Kwa sababu hiyo, wale wanaojaribu kuwa wanyoofu hushinikizwa sana waache kuwa wanyoofu katika hali zifuatazo.

Kushawishiwa na Tamaa Yako Mwenyewe. Ni nani ambaye hangependa kuwa na pesa nyingi au vitu vya kifahari? Inaweza kuwa vigumu kwa mtu kupinga kishawishi cha kujipatia faida za kifedha kwa njia isiyo ya unyoofu.

● “Mimi ndiye huwapa watu kandarasi za kampuni ninayofanyia kazi. Watu hujaribu kunipa rushwa. Ni vigumu sana kukataa pesa za bure.”​—Franz, Mashariki ya Kati.

Kushinikizwa Kuongeza Faida Katika Biashara. Katika miaka ya hivi karibuni, biashara nyingi zimekuwa zikipambana na hali mbaya ya kiuchumi. Lazima zikabiliane na teknolojia inayobadilika haraka na mashindano ya makampuni katika eneo lao na ulimwenguni pote. Huenda wafanyakazi wakahisi kwamba kukosa unyoofu ndio njia pekee ya kutimiza malengo waliyowekewa na wamiliki na mameneja.

● “Tuliona kwamba hakukuwa na lingine la kufanya. . . . La sivyo kampuni ingefilisika.”​—Reinhard Siekaczek, aliyekamatwa kwa sababu ya kutoa rushwa.​—The New York Times.

Kushinikizwa na Wengine. Huenda wafanyakazi wengine au wateja wakadokeza, au hata wakakushurutisha ujiunge nao katika mbinu zao za ukosefu wa unyoofu.

● “Meneja wa mteja fulani mashuhuri alinifikia na kuniambia kwamba hangefanya mapatano ya kibiashara pamoja nami ikiwa singempa kiasi fulani cha pesa kisiri.”​—Johan, Afrika Kusini.

Utamaduni. Katika tamaduni fulani, watu wana zoea la kupeana zawadi wanapofanya mapatano ya kibiashara. Huenda isiwe wazi kama mapatano hayo yalifanywa kwa unyoofu, ikitegemea ni zawadi ya aina gani na ilitolewa chini ya hali gani. Katika nchi nyingi, maofisa wafisadi hudai wapewe pesa kabla ya kutekeleza wajibu wao, nao hukubali kulipwa ili wamhudumie mtu kwa njia ya pekee.

● “Ni vigumu sana kutofautisha kati ya bakshishi na rushwa.”​—William, Kolombia.

Mazingira. Watu ambao huishi katika nchi maskini sana au nchi ambazo zimekumbwa na mvurugo wa kijamii ndio hushinikizwa zaidi. Katika maeneo kama hayo, wale ambao hawataki kudanganya au kuiba huonwa kuwa hawajui kuandalia familia zao.

● “Ukosefu wa unyoofu huonwa kuwa jambo la kawaida, linalokubalika, na la lazima maadamu mtu hagunduliwi.”​—Tomasi, Kongo Kinshasa.

Jinsi Watu Huacha Kuwa Wanyoofu

Shinikizo la kutokuwa mnyoofu lina nguvu sana. Uchunguzi uliofanyiwa mameneja wa biashara nchini Australia ulionyesha kwamba 9 kati ya 10 waliona rushwa na ufisadi kuwa “mambo yasiyofaa lakini hayawezi kuepukika.” Wale waliohojiwa walisema kwamba wangepuuza maadili yao ili wapate kandarasi au wanufaishe kampuni zao.”

Lakini mara nyingi wale wanaojihusisha katika ukosefu wa unyoofu hujiona kuwa hawana hatia. Wanawezaje kudumisha hadhi yao wakiwa na tabia hiyo? Jarida Journal of Marketing Research linaripoti hivi: “Watu hujifanya wao ni wanyoofu kwa kufuata maadili kwa kiasi fulani lakini wakati huohuo wanatenda kwa ukosefu wa unyoofu ili wajipatie faida.” Ili dhamiri zao zisiwasumbue, watu hutoa udhuru, kupunguza uzito, au kutetea matendo yao mbalimbali ya ukosefu wa unyoofu.

Kwa mfano, huenda watu wakatumia maneno yasiyoshtua ili kuelezea vitendo vyao vya ukosefu wa unyoofu. Kudanganya au kusema uwongo kunakuwa “kutumia njia za mkato.” Huenda rushwa ikasemwa kuwa “kiinua-mgongo” au “chai.”

Wengine wanapuuza mwenendo usiofaa kwa kuzungumzia ukosefu wa unyoofu kwa njia ambayo haionyeshi uzito wake. Tom, anayefanya kazi katika shirika moja la kifedha anasema hivi: “Watu wana maoni ya kwamba unyoofu ni uwezo wa mtu kujitetea kisheria badala ya kusema ukweli.” David, aliyekuwa na cheo kikubwa katika shirika fulani la kibiashara anasema hivi: “Ingawa ukosefu wa unyoofu ni tendo ambalo huchukiwa na watu linapofunuliwa, watu wengi huona kwamba linakubalika maadamu mtu hagunduliwi. Watu ambao huepuka kukamatwa huonwa kuwa wajanja.”

Huenda hata wengi wakadai kwamba mtu hawezi kufanikiwa akiwa mnyoofu. Mtu mmoja ambaye amefanya biashara kwa muda mrefu anasema hivi: “Mara nyingi, roho ya ushindani hufanya watu waseme, ‘Unapaswa kufanya chochote kile ili upate kazi.’” Je, maoni hayo ni ya kweli? Au wale wanaojaribu kutetea ukosefu wao wa unyoofu kwa kweli ‘wanajidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli’? (Yakobo 1:22) Fikiria faida za kuwa mnyoofu zinazozungumziwa katika makala inayofuata.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Watu wana maoni ya kwamba unyoofu ni uwezo wa mtu kujitetea kisheria badala ya kusema ukweli”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wengi wanadai kwamba mtu hawezi kufanikiwa akiwa mnyoofu