Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapohisi Kwamba Hutaki Kuendelea Kuishi

Unapohisi Kwamba Hutaki Kuendelea Kuishi

Unapohisi Kwamba Hutaki Kuendelea Kuishi

KILA siku watu 3,000 hivi ulimwenguni pote hujiua. Biblia inaeleza sababu ya msingi inayowafanya watu wengi wafikie hali hiyo ya kukata tamaa. Inaeleza kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watu wanahisi kwamba kuna mkazo mwingi sana maishani. (2 Timotheo 3:1; Mhubiri 7:7) Mtu anapolemewa na mahangaiko ya maisha, anaweza kufikiria kujiua ili asiendelee kuumia. Unaweza kufanya nini ikiwa umepatwa na mawazo kama hayo?

Wengine Wanakabili Hali Kama Yako

Hata ingawa huenda hali yako ikaonekana kuwa mbaya, kumbuka kwamba si wewe peke yako unayekabili hali hiyo na kwamba kwa kusikitisha, karibu kila mtu leo anakumbwa na tatizo fulani. Biblia inasema hivi: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Ingawa huenda kwa sasa ikaonekana kwamba tatizo lako haliwezi kusuluhishwa, mara nyingi mambo hubadilika kadiri wakati unavyopita. Kwa sasa, ni nini kinachoweza kukusaidia?

Mweleze rafiki mkomavu, unayemwamini hisia zako. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Mwanamume mwadilifu Ayubu, anayetajwa katika Biblia, aliwaeleza wengine jinsi alivyohisi alipokuwa akikabili hali ngumu. Alipohisi kwamba ‘anachukizwa na uhai wake,’ alisema hivi: “Nitaonyesha hangaiko langu kujihusu mwenyewe. Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 10:1) Kuwaeleza wengine jinsi unavyohisi kunaweza kupunguza uzito wa hisia zako, na hilo linaweza kukusaidia ubadili maoni yako kuhusu matatizo unayokabili. *

Mmiminie Mungu moyo wako katika sala. Wengine hufikiri kwamba sala ni njia tu ya kutuliza hisia, lakini Biblia inaonyesha jambo tofauti. Zaburi 65:2 inasema kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala,” na 1 Petro 5:7 inasema: “Yeye anawajali ninyi.” Biblia inakazia mara nyingi umuhimu wa kumtegemea Mungu. Kwa mfano:

“Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”​METHALI 3:5, 6.

“[Yehova] atawatimizia wale wanaomwogopa tamaa yao, naye atakisikia kilio chao cha kuomba msaada, naye atawaokoa.” ​ZABURI 145:19.

“Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”​1 YOHANA 5:14.

“Yehova yuko mbali sana na waovu, lakini huisikia sala ya waadilifu.”​METHALI 15:29.

Ukimweleza Mungu matatizo unayokabili, atakupa msaada. Biblia ina sababu nzuri inapokutia moyo ‘umtegemee nyakati zote.   .Mimina moyo wako mbele zake.’​—Zaburi 62:8.

Mengi Zaidi Yanapohitajika

Uchunguzi unaonyesha kwamba watu wengi ambao hujiua wamewahi kushuka moyo kwa muda fulani. * Hilo linakazia kwamba huenda mtu akahitaji kumwona daktari. Huenda daktari akapendekeza mtu atumie dawa fulani au abadili chakula. Katika visa fulani, programu fulani ya mazoezi inaweza kumsaidia mtu anapoendelea na matibabu. Matibabu ya kitaalamu yamewasaidia watu wengi. *

Biblia ina habari nyingi zinazoweza kukutegemeza na kukupa tumaini. Kwa mfano, katika Ufunuo 21:4, Biblia inasema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Hiyo ni ahadi kutoka kwa Mungu, na kutafakari kuihusu kunaweza kukusaidia upate kitulizo.

Mashahidi wa Yehova wanawafundisha mamilioni ya watu ulimwenguni pote tumaini hilo linalotegemea Biblia. Kufanya hivyo kunawasaidia watu wengi wapate tumaini la kweli katika nyakati hizi zenye kuhuzunisha. Ili upate habari zaidi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu kwa kuwatembelea katika Jumba la Ufalme lililo karibu nawe, au uandike barua kwa kutumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili. Unaweza pia kutembelea Tovuti yetu www.watchtower.org/sw.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Wengine wamepata msaada kwa kupiga simu kwenye kituo cha kuzuia watu kujiua au kituo cha kuwatunza watu walio na matatizo ya akili.

^ fu. 13 Ili upate habari zaidi kuhusu kushuka moyo, ona toleo la Julai  2009 la Amkeni! ukurasa wa 3-9.

^ fu. 13 Amkeni! halipendekezi matibabu yoyote hususa. Kila mtu anapaswa kuchunguza matibabu mbalimbali kabla ya kufanya uamuzi wake.

[Sanduku katika ukurasa wa 16]

MSAADA KUTOKA KWA BIBLIA

● “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”​—Wafilipi 4:6, 7.

● “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.”​—Zaburi 34:4.

● “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”​—Zaburi 34:18.

● “Anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”​—Zaburi 147:3.

[Sanduku katika ukurasa wa 17 18]

IKIWA UNAFIKIRIA KUJIUA . . .

Mweleze rafiki unayemwamini hisia zako

Mmiminie Mungu moyo wako katika sala

Mwone daktari

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 18]

MARAFIKI NA WATU WA FAMILIA

Mara nyingi watu wa familia na marafiki wa karibu ndio wa kwanza kutambua kwamba mtu aliyeshuka moyo anafikiria kujiua. Kuchukua hatua kunaweza kuokoa uhai wa mtu huyo! Sikiliza kwa hisia mwenzi. Kubali kwamba matatizo anayokabili ni halisi. Biblia inasema: “Semeni kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.” (1 Wathesalonike 5:14) Msihi yule aliyeshuka moyo apate msaada, na inapohitajika fuatilia uhakikishe kwamba msaada huo umetolewa.