Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unyoofu Huleta Mafanikio ya Kweli

Unyoofu Huleta Mafanikio ya Kweli

Unyoofu Huleta Mafanikio ya Kweli

“Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”​—Luka 12:15.

KUTAFUTA riziki ni sehemu muhimu ya maisha. Tuna wajibu mbele za Mungu wa kuandaa mahitaji yetu na ya familia zetu.​—1 Timotheo 5:8.

Lakini namna gani ikiwa badala ya kutafuta riziki tu unaanza kukazia fikira kutafuta pesa na vitu unavyoweza kununua? Vipi ikiwa hilo ndilo kusudi lako kuu maishani? Wale ambao lengo lao kuu ni kutajirika huona kuwa ni rahisi kutumia njia zisizo za unyoofu kupata pesa. Huenda wasitambue kwamba kukosa unyoofu kunawafanya wasifanikiwe kikweli mpaka inapokuwa kuchelewa mno. Isitoshe, kama vile Biblia inavyosema, kupenda pesa husababisha maumivu mengi.​—1 Timotheo 6:9, 10.

Fikiria mifano minne ifuatayo ya watu ambao wanasema kwamba kufanikiwa hakumaanishi kujirundikia mali.

Kujiheshimu

“Miaka kadhaa iliyopita, nilimhoji mteja aliyetaka kununua bima ya maisha ambayo ingemgharimu dola milioni moja. Ningelipwa maelfu ya dola kwa kukamilisha mkataba huo. Aliniambia kwamba ili awe mteja wangu, ingebidi nimpe nusu ya pesa nilizopata. Ombi lake lilikuwa kinyume cha maadili na pia tungekuwa tukivunja sheria, nami nilimwambia hivyo waziwazi.

“Nilijaribu kuzungumza naye na kumwuliza ikiwa angetaka mtu asiye mnyoofu ajue habari zake za kibinafsi na za kifedha ambazo ni siri. Nilimweleza tena msimamo wangu na kumwambia awasiliane nami ikiwa bado angetaka nimwakilishe. Hakuwahi kuwasiliana nami tena.

“Kama ningekubali ombi lake, ningeacha kuwa mwaminifu na ningeacha kujiheshimu kama Mkristo. Ningekuwa mtumwa wa mwanadamu ambaye alitaka kunishinikiza nijiunge naye katika ukosefu wa unyoofu.”​—Don, Marekani.

Amani ya Akili

Kama ilivyotajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu, mmiliki wa kiwanda fulani alitaka kumpa Danny rushwa kubwa ili adanganye kwamba kiwanda hicho kinaweza kutokeza bidhaa zinazofaa. Danny alifanya nini?

“Nilimshukuru meneja huyo kwa kunikaribisha kwenye mlo kisha nikamrudishia bahasha hiyo iliyokuwa na pesa. Alinishinikiza kwa kusema kwamba ikiwa kiwanda chake kingepita ukaguzi wetu, angeniongezea pesa zaidi. Nilikataa.

“Kama ningekubali rushwa hiyo, ningekuwa na wasiwasi daima kwamba nitagunduliwa. Baadaye, mwajiri wangu alipata habari kuhusu kisa hicho. Nilifurahi sana kwamba sikuwa nimefanya jambo lolote lenye ukosefu wa unyoofu. Nilikumbuka andiko la Methali 15:27: ‘Mtu anayepata faida isiyo ya haki anailetea nyumba yake mwenyewe taabu, lakini anayechukia zawadi [au rushwa] ndiye atakayeendelea kuishi.’”​—Danny, Hong Kong.

Furaha ya Familia

“Nina biashara yangu ya ujenzi. Mimi hupata fursa nyingi za kuwadanganya wateja wangu au kukwepa kulipa kodi. Lakini mimi na familia yangu tumefaidika kutokana na jitihada zangu za kuendelea kuwa mnyoofu.

“Mtu anapaswa kuwa mnyoofu katika kila sehemu ya maisha yake, si kazini au katika biashara tu. Kujua kwamba mume au mke wako hatavunja kanuni za Mungu za unyoofu kunafanya washiriki wa familia waaminiane. Mwenzi wako anajihisi akiwa salama kwa sababu anajua kwamba unyoofu wako si kama vazi unalovaa na kuvua inapohitajika.

“Unaweza kuwa mmiliki wa kampuni kubwa zaidi ulimwenguni lakini huwezi kununua suluhisho la matatizo ya familia yako. Nikiwa Shahidi wa Yehova, nimegundua kwamba kufuata kanuni za Biblia hufanya niwe na usawaziko. Nina wakati wa kuwa pamoja na familia yangu bila kufuata tu ulimwengu huu unaoongozwa na pupa na pesa.”​—Durwin, Marekani.

Uhusiano Mzuri na Mungu

“Kazi yangu inahusisha kununua bidhaa kwa ajili ya kampuni yetu. Nyakati nyingine wauzaji huniambia kwamba badala ya kuipunguzia kampuni bei, watanipa kiasi fulani cha faida wanayopata kutoka kwa kampuni yetu. Lakini kufanya hivyo kungekuwa kuiba pesa za kampuni.

“Mimi hupata mshahara wa chini, na pesa hizo za ziada zingenisaidia sana. Lakini hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na dhamiri safi na kupata kibali machoni pa Yehova Mungu. Kwa hiyo, ninaponunua bidhaa yoyote, mimi hufuata kanuni ya Biblia kwenye Waebrania 13:18: ‘Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.’”​—Raquel, Filipino.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kanuni Kuhusu Kufanya Biashara kwa Unyoofu

Kanuni za maadili za biashara hutofautiana katika sehemu mbalimbali. Hata hivyo, kanuni za Biblia zinaweza kutumiwa kuwa msingi wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili. Zifuatazo ni kanuni sita za kufanya biashara kwa unyoofu:

Kusema Kweli

Kanuni: “Msiwe mkiambiana uwongo.”​—Wakolosai 3:9.

Kutegemeka

Kanuni: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”​—Mathayo 5:37.

Kuaminika

Kanuni: “Usifunue mazungumzo ya siri ya mwingine.”​—Methali 25:9.

Unyoofu

Kanuni: “Usikubali rushwa, kwa maana rushwa hupofusha watu wanaoona.”​—Kutoka 23:8.

Tenda kwa Haki

Kanuni: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”​—Mathayo 7:12.

Fuata Sheria

Kanuni: “Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi.”​—Waroma 13:7.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 9]

Jinsi ya Kuwa Mnyoofu Katika Biashara

Amua Mambo Utakayotanguliza. Kwa mfano, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwako—kupata utajiri au kudumisha msimamo mzuri mbele za Mungu?

Amua Mapema. Fikiria hali ambazo zinaweza kufanya iwe vigumu kuwa mnyoofu, na uamue jinsi utakavyokabiliana nazo.

Tangaza Msimamo Wako Waziwazi. Unapoanza kufanya biashara na wengine, waeleze kwa busara kuhusu viwango vyako.

Waombe Wengine Mashauri. Unapokabili kishawishi, mwombe mashauri mtu ambaye anafuata viwango kama vyako.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ukiwa mnyoofu, utakuwa na amani ya akili