Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Manne Unayopaswa Kujiuliza Kuhusu Vituo vya Mawasiliano

Maswali Manne Unayopaswa Kujiuliza Kuhusu Vituo vya Mawasiliano

Maswali Manne Unayopaswa Kujiuliza Kuhusu Vituo vya Mawasiliano

Kama tu ilivyo kuhusu matumizi mengine ya Intaneti, kuna hatari ya kutumia vituo vya mawasiliano. * Ukiwa na hilo akilini, fikiria maswali yafuatayo.

1 Vituo vya Mawasiliano Vinaathirije Faragha Yangu?

“Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa, lakini anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.”​—Methali 10:19.

Unachopaswa kujua. Usipokuwa mwangalifu, habari zako za kibinafsi, picha, ujumbe mfupi unaopachika kwenye ukurasa wako, na maelezo unayoandika kwenye ukurasa wa wengine, yanaweza kufunua mambo mengi sana. Kwa mfano, yanaweza kufunua mambo kama vile mahali unapoishi, wakati ambapo upo nyumbani (ama ikiwa umetoka), mahali unapofanyia kazi, au mahali unapoenda shule. Habari kuhusu mahali unapoishi pamoja na ujumbe kama vile, “Kesho tunaenda likizo!” unatosha kumwambia mwizi mahali na wakati wa kushambulia.

Kufichua habari nyingine, kama vile anwani ya barua-pepe, tarehe ya kuzaliwa, au namba yako ya simu, kunaweza kufanya udhulimiwe, uonewe, au kumfanya mtu aibe utambulisho wako. Ingawa hivyo, watu wengi hutoa habari hizo kwa urahisi kwenye ukurasa wao katika kituo cha mawasiliano.

Watu husahau kwamba mara tu wanapopachika kitu kwenye Intaneti, kinaweza kupatikana na kila mtu. Hata mtu anapofunga ukurasa wake utumiwe tu na “Marafiki pekee,” hawezi kudhibiti jinsi marafiki hao watakavyotumia habari hizo. Kwa kweli, chochote ambacho mtu anapachika kwenye kituo cha mawasiliano kinapaswa kuonwa kuwa habari ya umma au habari inayoweza kupatikana kwa urahisi na umma.

Jambo unaloweza kufanya. Hakikisha unafahamiana vizuri na mbinu za kuweka siri za kituo cha mawasiliano unachotumia na uzitumie. Funga ukurasa wako ili ujumbe wako na picha zako zionekane tu na watu unaowajua na kuwaamini.

Hata unapofanya hivyo, tambua kwamba kile unachopachika kinaweza kuonekana na watu wengi kuliko ulivyokusudia. Chunguza ukurasa wako mara kwa mara, na ujiulize ikiwa chochote ambacho umefunua kinaweza kutumiwa na wahalifu ili kukupata au kuiba utambulisho wako. Hata unaposhughulika na rafiki zako, usipachike habari inayoweza kufichua mambo yako ya siri au ya mtu mwingine. (Methali 11:13) Ikiwa una habari nyeti unayotaka kupitisha, tumia njia nyingine ya mawasiliano. Msichana anayeitwa Cameron anasema, “Kuzungumza kwenye simu ni njia ya kuwasiliana moja kwa moja na kwa faragha zaidi.”

Jambo kuu. Mwanamke anayeitwa Kim alisema hivi: “Ukiwa mwangalifu kuhusu jambo unalofanya, unaweza kudumisha kiasi fulani cha faragha unapotumia kituo cha mawasiliano. Unapokuwa mwangalifu hutapatwa na madhara.”

2 Vituo vya Mawasiliano Vinaathirije Wakati Wangu?

“Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”​—Wafilipi 1:10.

Unachopaswa kujua. Kutumia vituo vya mawasiliano kunaweza kukuibia wakati mwingi sana na kukukengeusha kutokana na utendaji mwingine muhimu zaidi. Mwanamke anayeitwa Kay anasema kwamba “ukiwa na marafiki wengi, ndivyo utakavyotumia wakati mwingi zaidi kwenye kituo cha mawasiliano na ni rahisi zaidi kuwa mraibu.” Fikiria maelezo ya watu fulani wanaosema kwamba walinaswa na mtego huo.

“Ni vigumu kuacha kutumia kituo cha mawasiliano, hata wakati ambapo hutaki kuendelea kukitumia. Ni kama uraibu.”​—Elise.

“Kuna vitu vingi sana unavyoweza kufanya humo—michezo, mitihani, kurasa kwa ajili ya watu wanaopenda wanamuziki fulani—bila kutaja kuhusu kurasa za marafiki wako.”uraibu.”​—Blaine.

“Ni uraibu unaokunasa kabisa, hutambui kwamba umenaswa hadi mama yako anaporudi nyumbani na kukuuliza kwa nini hujaosha vyombo.”​—Analise.

“Nilijikuta nikitamani kufika nyumbani upesi kutoka shuleni ili nione ikiwa kuna yeyote ambaye ameandika maelezo yake kwenye ukurasa wangu. Kisha nilihitaji kuwajibu watu wote hao na kuangalia picha zote mpya walizokuwa wamepachika. Ilikuwa rahisi sana kwangu kuudhika nilipokuwa nikitumia Intaneti, na nilichukizwa sana mtu aliponikatiza. Watu fulani ninaowafahamu hutumia kituo hicho kila wakati—hata wanapokuwa wamealikwa kwenye nyumba za watu wengine na hata usiku sana!”​—Megan.

Jambo unaloweza kufanya. Wakati ni kitu ambacho hupaswi kupoteza. Kwa hiyo, mbona usipange jinsi utakavyoutumia, kama tu unavyopanga jinsi utakavyotumia pesa? Kwanza, andika kiasi cha wakati unachohisi kwamba kinafaa kutumiwa kwenye kituo cha mawasiliano. Kisha jichunguze kwa mwezi mzima na uone ikiwa ulitumia wakati vizuri kama ulivyopangia. Fanya mabadiliko yanayohitajika.

Ikiwa wewe ni mzazi na vijana wako wanatumia wakati mwingi kwenye vituo vya mawasiliano, jaribu kuchunguza ikiwa kuna mambo yoyote yanayochochea tatizo hilo. Kwa mfano, katika kitabu chake Cyber-Safe Kids, Cyber-Savvy Teens, Nancy E. Willard anasema kwamba kutumia kituo cha mawasiliano kupita kiasi kunaweza kuhusianishwa na wasiwasi, mfadhaiko, na kutojiheshimu. “Vijana wengi huwa na wasiwasi kuhusu ikiwa wanapendwa na wengine,” anaandika. “Ikiwa vijana wanapima kama wanapendwa kwa kutegemea wanawasiliana na marafiki wao kwa kadiri gani kupitia vifaa vya kielektroniki, hilo linaweza kuchochea uraibu.”

Usiache vituo vya mawasiliano—au utendaji wowote wa Intaneti—uathiri uhusiano unaopaswa kuwa ukikuza ndani ya nyumba yako mwenyewe. Don Tapscott anaandika hivi katika kitabu chake Grown Up Digital: “Jambo moja lenye kushangaza kuhusu Intaneti ni kwamba ingawa inafanya kuwasiliana kuwe rahisi zaidi wakati ambapo watu wa familia wako mbali, matumizi ya Intaneti yanaweza kuwafanya watengane wanapokuwa nyumbani.”

Jambo kuu. Msichana anayeitwa Emily anasema hivi: “Nafikiri vituo vya mawasiliano ni njia nzuri sana ya kuwasiliana na watu. Lakini, kama tu kitu kingine chochote, unapaswa kujua wakati wa kuacha kukitumia.”

3 Vituo vya Mawasiliano Vinaathirije Sifa Yangu?

“Afadhali kuwa na sifa nzuri kuliko mali nyingi.”—Methali 22:1, “Biblia Habari Njema.”

Unachopaswa kujua. Mambo unayopachika kwenye kituo cha mawasiliano yanakufanya uwe na sifa ambayo si rahisi kubadili. (Methali 20:11; Mathayo 7:17) Ni kana kwamba watu wengi hawaoni hatari iliyopo. “Inaonekana kwamba watu wanapoanza kutumia kituo cha mawasiliano, wanapoteza uwezo wao wa kufikiri,” anasema msichana anayeitwa Raquel. “Wanasema mambo ambayo kwa kawaida hawangesema. Wengine hawatambui kwamba kupachika tu kitu kimoja kisichofaa kutaharibu sifa yao kabisa.”

Kuharibu jina lako kwenye kituo cha mawasiliano kunaweza kutokeza madhara ya muda mrefu. Kitabu Grown Up Digital kinasema: “Kuna visa vingi sana vya watu ambao wamepoteza kazi au wakakosa kuajiriwa kwa sababu ya mambo ambayo walipachika kwenye vituo vya mawasiliano.”

Jambo unaloweza kufanya. Chunguza ukurasa wako kwenye kituo cha mawasiliano na ujaribu kufikiria wengine watakapouona watakuwa na maoni gani. Jiulize maswali haya: ‘Je, ningependa watu wanitambue kuwa mtu wa aina hii? Ikiwa mtu angetazama picha nilizopachika na afafanue utu wangu kutokana na kile alichoona, angetumia maneno ya aina gani kunihusu? “Anapenda kuwachezea wengine kimapenzi”? “Anachochea hamu ya ngono”? “Mpenda-anasa”? Ikiwa ndivyo, je, hayo ndiyo maoni ambayo ningependa wengine wawe nayo kunihusu, kwa mfano, ninapotoa ombi kwa ajili ya kazi ningependa mwajiri afikiri hivyo kunihusu anapotazama ukurasa wangu? Je, picha hizo zinaonyesha viwango ninavyofuata?’

Ikiwa wewe ni kijana, jiulize: ‘Namna gani ikiwa mzazi, mwalimu, au mtu mzima ninayeheshimu angetazama ukurasa wangu? Je, ningeaibikia mambo ambayo angeona na kusoma?’

Jambo kuu. Sifa yako inapohusika, kumbuka maneno ya mtume Paulo: “Alichopanda mtu ndicho atakachovuna.”​—Wagalatia 6:7, BHN.

4 Vituo vya Mawasiliano Vinaathirije Urafiki Wangu?

“Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Unachopaswa kujua. Marafiki wako huathiri jinsi unavyofikiri na kutenda. (1 Wakorintho 15:33) Kwa hiyo, inafaa kwamba uwe mteuzi unapoamua kukubali watu wawe marafiki wako kwenye kituo cha mawasiliano. Watu wengine hukubali maombi ya mamia ya watu wanaotaka kuwa marafiki ingawa hawawajui watu hao vizuri—au hata hawawajui kabisa. Wengine hugundua kwamba si watu wote walio kwenye orodha yao ya marafiki ambao ni mashirika wazuri. Fikiria kile ambacho watu fulani wamesema.

“Ikiwa mtu anakubali maombi ya mtu yeyote tu anayetaka kuwa rafiki, atajiingiza katika shida.”​—Analise.

“Watu wengi ninaojua hukubali maombi ya watu ambao hawakutaka wawe marafiki wao, eti kwa sababu hawataki tu kuumiza hisia za mtu huyo kwa kupuuza ombi lake.”​—Lianne.

“Ni kama tu kushirikiana na watu hao uso kwa uso. Lazima uwe mwangalifu unakubali nani awe rafiki yako.”​—Alexis.

Jambo unaloweza kufanya. Jiwekee ‘masharti ya kukubali marafiki.’ Kwa mfano, wengine wamejiwekea mipaka kuhusu urafiki: *

“Mimi hukubali tu mtu awe rafiki yangu ikiwa ninamfahamu—si kwa sababu tu ninamtambua—lakini kwa sababu ninamjua vizuri.”​—Jean.

“Mimi hukubali tu maombi ya watu ambao nimewafahamu kwa muda mrefu. Sikubali kamwe maombi ya watu nisiowafahamu.”​—Monique.

“Mimi hupenda kukubali maombi ya watu ambao ninawajua vizuri na ambao ninajua wana viwango kama vyangu.”​—Rae.

“Ninapopata ombi kutoka kwa mtu nisiyemfahamu, mimi hupuuza ombi hilo. Hakuna mchezo. Marafiki wangu wote ni watu ninaowafahamu na tayari wao ni marafiki wangu kihalisi, si kwenye Intaneti tu.”​—Marie.

“Rafiki yangu anapoanza kupachika picha au ujumbe ninaoona kuwa wenye kutiliwa shaka, sioni ubaya wa kumwondoa kwenye orodha yangu. Hata ukitazama vitu wanavyopachika tayari wao ni mashirika mabaya.”​—Kim.

“Nilipokuwa na akaunti kwenye kituo cha mawasiliano, niliweka masharti makali ya faragha. Sikuruhusu marafiki wa marafiki wangu waone ujumbe au picha zangu—niliruhusu tu marafiki wangu. Nilifanya hivyo kwa sababu sikujua ikiwa marafiki wa marafiki wangu walikuwa watu ambao mimi ningependa kushirikiana nao. Sikuwafahamu—wala sikufahamu walikuwa na sifa gani.”​—Heather.

Jambo kuu. Dakt. Gwenn Schurgin O’Keeffe anaandika hivi katika kitabu chake CyberSafe: “Jambo bora zaidi unaloweza kufanya ni kukubali tu marafiki unaowafahamu na ambao mna uhusiano nje ya Intaneti.” *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Amkeni! haipendekezi wala haishutumu tovuti yoyote ya mawasiliano. Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matumizi yao ya Intaneti hayavunji kanuni za Biblia.​—1 Timotheo 1:5, 19.

^ fu. 35 Katika makala hii, tunazungumza kuhusu urafiki wa kawaida, si mahusiano ya kibiashara.

^ fu. 42 Kwa habari zaidi kuhusu vituo vya mawasiliano, ona matoleo ya Amkeni! ya Julai 2011, ukurasa wa 24-27, na Agosti 2011, ukurasa wa 10-13.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

KUMBUKA KUTOKA!

Ukiacha akaunti yako ikiwa wazi unapoondoka, huenda wengine wakapachika vitu kwenye ukurasa wako. Kulingana na wakili Robert Wilson, hiyo ni “sawa na kuacha kibeti au simu yako ya mkononi mahali pa umma. Mtu yeyote anaweza kupachika vitu kwenye Ukuta wako.” Anapendekeza nini? “Hakikisha kwamba unatoka.”

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

UNAJITAKIA MATATIZO?

Uchunguzi uliofanywa na jarida Consumer Reports unafunua kwamba watu wengi wanaotumia vituo vya mawasiliano “hupachika mambo yanayoweza kufanya nyumba zao zivunjwe, waibiwe utambulisho wao, na hata waandamwe na wahalifu. Asilimia 15 ya watu walikuwa wameonyesha mahali walipokuwa au mipango yao ya kusafiri, asilimia 34 walionyesha tarehe kamili ya kuzaliwa, na asilimia 21 ya watu waliokuwa na watoto nyumbani walipachika majina na picha za watoto hao.”