Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini ili Nifurahie Kujifunza Biblia?

Nifanye Nini ili Nifurahie Kujifunza Biblia?

Vijana Huuliza

Nifanye Nini ili Nifurahie Kujifunza Biblia?

Kwa nini hasa ujifunze Biblia? Fikiria mambo haya:

Biblia inaweza kukusaidia upate hazina. Kitabu hiki kilichosambazwa sana kinaweza

● Kukuonyesha jinsi ya kujitayarisha ili uwe na maisha bora baadaye

● Kukuambia mambo yanayohusu wakati ujao—na yaliyopita—ambayo usingeyajua kamwe

● Kukusaidia ujielewe vizuri na kuboresha utu wako *

KUJIFUNZA Biblia kunataka jitihada, lakini kuna faida nyingi! Je, ungependa kujua jinsi vijana fulani hujifunza Biblia? Kata na ukunje ukurasa unaofuata. Utapata kurasa nne nzima za kukuonyesha jinsi vijana wa rika lako wanavyoshinda vizuizi na kufaidika kikamili kutokana na kujifunza Biblia kibinafsi.

“Kila mtu anaweza kupata jambo fulani katika Biblia litakalomvutia na kumsaidia kibinafsi. Kuna mambo mengi sana tunayoweza kujifunza katika Biblia!”​—Valerie. *

Unaweza kupata makala zaidi za “Vijana Huuliza” katika Tovuti ya www.watchtower.org/ype

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ili ujifunze jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia kufanya mambo hayo yote, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu, andika barua ukitumia anwani ifaayo kati ya zile zilizoorodheshwa katika ukurasa wa 5, au tembelea Tovuti yetu ya www.watchtower.org/sw.

^ fu. 9 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 19, 20]

JINSI YA KUJIFUNZA BIBLIA

Tatizo: HUNA HAMU YA KUJIFUNZA

“Sipendi kuketi kwa saa nzima ili kujifunza.”​—Lena.

Unachohitaji: KICHOCHEO

Ili ufurahie kujifunza Biblia, unahitaji kujiuliza, Nitapata faida gani? Je, ungependa kuwa rafiki ya Mungu? au kufahamu vyema matukio ya ulimwengu? au kuboresha utu wako? Biblia inaweza kukusaidia kutimiza mambo hayo—na mengine mengi!

“Usiwe na wazo la kwamba ni kama kazi au kama masomo ya shule. Badala yake, ona funzo la Biblia kuwa njia ya kumkaribia Rafiki Mkuu zaidi ya wote—Yehova Mungu.”​—Bethany.

“Pindi ya kujifunza ni wakati unaotumia wewe binafsi pamoja na Yehova Mungu. Ukitumia wakati pamoja na mtu fulani pindi tu wazazi wako wapo, je, unaweza kusema kwa kweli huyo ni rafiki yako au ni rafiki ya wazazi wako? Ukijifunza kibinafsi, Yehova anaweza kuwa rafiki yako.”​—Bianca.

Kumbuka: “Maandiko yote matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa katika kufundisha ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha ya adili.” (2 Timotheo 3:16, Biblia ya Kiswahili East Africa) Biblia inaweza kukusaidia katika njia hizo pia!

“Ninajaribu kukazia fikira thawabu. Kama nina udhaifu fulani, kujifunza ni fursa nzuri ya kujua njia ya kufanyia maendeleo udhaifu huo.”​—Max.

Jambo la kufikiria:

Ni nini kinachoweza kukuchochea ujifunze?

Tatizo: KUNACHOSHA

“Baada ya kujifunza kwa dakika 10 hivi, mimi huanza kuchoka; dakika 20 zikiisha natamani tu kufanya jambo lingine; dakika 30 zikipita, nimepoteza kabisa hamu ya kusoma!”​—Allison.

Unachohitaji: UBUNIFU

Uwe mbunifu, iwe ni kuhusu habari unayotaka kujifunza, jinsi ya kujifunza, au mazingira unayochagua kufanyia funzo lako.

“Fanya utafiti kuhusu maswali uliyo nayo. Ukijifunza kuhusu jambo ambalo umekuwa ukifikiria, mwishowe unahisi umeridhika na unapata shangwe pia.”​—Richard.

“Unaposoma kuhusu tukio fulani, jiweke katika hali ya wanaohusika. Wazia kwamba wewe ndiwe mhusika mkuu au mtazamaji wa jambo linalotendeka. Jaribu kuwazia unajionea jambo hilo likitendeka.”​—Steven.

“Fanya funzo livutie. Keti nyuma ya nyumba ukiwa na glasi ya maji ya matunda. Mimi hupenda vitafunio ninapojifunza. Kila mtu hufurahia vitafunio anapojifunza.”​—Alexandra.

Kumbuka: Mara nyingi mtu huchoka kwa sababu ya kuwa na mtazamo usiofaa. Kwa hiyo badala ya kusema “kujifunza kunachosha,” sema “mimi nimechoka.” Badili mtazamo wako kuelekea kujifunza. Hilo litakusaidia uwe na nguvu za kuchukua hatua inayofaa.​—Methali 2:10, 11.

“Si lazima funzo la kibinafsi liwe lenye kuchosha. Ukitaka linaweza kuwa lenye kupendeza.”​—Vanessa.

Jambo la kufikiria:

Unaweza kufanya nini ili uwe mbunifu unapojifunza?

Tatizo: HUNA WAKATI

“Ningependa sana kujifunza Biblia zaidi, lakini kwa kuwa nina shughuli nyingi siwezi kupata wakati wa kuketi chini na kujifunza!”​—Maria.

Unachohitaji: KUJUA MAMBO YA KUTANGULIZA

Njia moja ya kuonyesha umekuwa mtu mzima ni kujifunza ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’​—Wafilipi 1:10.

“Mama yangu alinisaidia kutambua kwamba sitawahi kuwa na wakati wa ziada. Nilihitaji kununua wakati. Nilipokuza hamu ya kujifunza, nilitenga wakati kwa ajili ya jambo hilo.”​—Natanya.

“Kadiri ninavyokua, nimejifunza kwamba ni lazima nitenge wakati wa kujifunza, nami hujifunza wakati huo, haidhuru kunatokea nini.”​—Yolanda.

“Ukitanguliza funzo kabla ya tafrija, ninakuhakikishia utafurahia funzo hata zaidi—na utafurahia tafrija bila kusumbuliwa na dhamiri.”​—Diana.

Kumbuka: Usipojua mambo ya kutanguliza, utapoteza wakati na hutaweza kutimiza mambo uliyopanga kufanya. Ni afadhali utenge wakati wa kujifunza.​—Waefeso 5:15, 16.

“Kwa kuwa mimi ni mwanafunzi wa shule ya sekondari, ni rahisi sana kujipata nikijishughulisha na mambo mengine! Ingawa hivyo, mimi huhakikisha kwamba ninatia funzo la Biblia la kibinafsi katika ratiba yangu.”​—Jordan.

Jambo la kufikiria:

Unaweza kujipangia ratiba gani ya kujifunza?

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 19]

MADOKEZO KUTOKA KWA VIJANA WENZAKO

Zachary​—Usijifunze mambo ambayo wazazi wako au watu wengine wanajifunza. Linakuwa funzo la kibinafsi unapojifunza jambo ambalo wewe unataka.

Kaley​—Anza kujifunza kwa muda mfupi. Ikibidi, jifunze kwa dakika tano tu, lakini usikose hata siku moja. Kisha hatua kwa hatua unaweza kuongeza muda huo hadi dakika 10, 15 . . . Hatimaye utaanza kufurahia kujifunza!

Daniela​—Mambo madogo-madogo yanaweza kusaidia sana. Tafuta kalamu zenye rangi tofauti-tofauti na kijitabu kizuri, au tengeneza faili katika kompyuta yako yenye kichwa Funzo la Kibinafsi.

Jordan​—Ninapochagua jambo ninalofurahia kujifunza, ninaweza kujifunza kwa muda mrefu zaidi. Pia mimi hupenda mazingira matulivu. Siwezi kujifunza mahali ambapo kuna kelele nyingi.

[Mchoro katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Kata ukifuata mstari wenye nukta

Kunja