Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Jicho kwa Hekima

Tumia Jicho kwa Hekima

Tumia Jicho kwa Hekima

● Jicho la mwanadamu ni kiungo maridadi sana. Lakini si maridadi tu. Lina nguvu pia. Kitabu Visual Impact, Visual Teaching kinasema kwamba “asilimia 40 ya nyuzi zote za neva zinazoelekea kwenye ubongo zimeunganishwa kwenye retina,” tishu nyembamba iliyo tata katika tabaka la ndani la jicho.

Kwa kufaa, Yesu Kristo alisema kuwa jicho ni “taa ya mwili.” Akieleza alichomaanisha, alisema: “Ikiwa jicho lako ni rahisi [nyoofu, linalokazia mambo mema], mwili wako wote utakuwa mwangavu; lakini ikiwa jicho lako ni bovu, mwili wako wote utakuwa wenye giza.” (Mathayo 6:22, 23) Kwa maneno hayo, Yesu alikuwa akitukumbusha jinsi ambavyo jicho letu linaweza kuchochea mawazo, hisia, na matendo yetu. Mawazo mazuri huangaza maisha ya mtu; mawazo mabaya huyatia giza.

Kwa mfano, hebu fikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:28, 29: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake. Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe [kwa njia ya mfano].” Alimaanisha nini? Jicho linalotangatanga linaweza kuchochea tamaa mbaya hivi kwamba, mtu akipata fursa, anaweza kujihusisha katika ukosefu wa maadili na kupoteza kibali cha Mungu.​—Yakobo 1:14, 15.

Ni jambo bora kama nini kujizuia, hata ikiwa kufanya hivyo ni vigumu kama tu inavyoweza kuwa vigumu kwa mtu kuling’oa jicho lake! Je, kweli kuna faida yeyote kwa mtu kupoteza uzima wa milele ili tu atosheleze tamaa za mwili ambazo ni za muda mfupi?

Mambo tunayotazama kwa macho yetu yanaweza kuchochea pupa. Kwa sababu hiyo, Biblia inatuonya kwamba ‘tamaa ya kichoyo ya macho haitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.’​—1 Yohana 2:16, 17.

Je, Biblia ina vizuizi vingi kupita kiasi? La, hasha! Mtu akipuuza viwango vya Biblia atapatwa na matatizo na kukosa furaha. (Wagalatia 6:7, 8) Tukitii Neno la Mungu, kutia ndani mwelekezo wake wenye hekima kuhusu mambo tunayotazama, tutavuna furaha. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika.” (Luka 11:28) Isitoshe, wana tumaini la kuishi milele duniani, ilhali wale walio na jicho linalokazia mambo yasiyo ya adili au pupa watakosa furaha na uhai.