Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kusali kwa Mungu Jinsi Gani?

Tunapaswa Kusali kwa Mungu Jinsi Gani?

Maoni ya Biblia

Tunapaswa Kusali kwa Mungu Jinsi Gani?

NI PENDELEO lisilo na kifani kuzungumza na Mweza-Yote na kumweleza mawazo yetu ya ndani. Hata hivyo, watu wengi hawajui jinsi ya kusali, na wengine wanataka kuboresha sala zao. Inaonekana kwamba baadhi ya wafuasi wa kwanza wa Yesu Kristo walitaka kuboresha sala zao. Mmoja wao alimwambia hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Yesu alimjibu kwa kutoa ile sala ya kielelezo, ambayo mara nyingi huitwa Sala ya Bwana au Sala ya Baba Yetu. Sala hiyo yenye maneno yenye kupendeza na rahisi hutusaidia kujua jinsi ya kuzungumza na Mungu kwa njia inayokubalika na pia inatusaidia kujua ujumbe mkuu wa Biblia.

Sala ya Kielelezo ya Yesu

Yesu alisema: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii; na utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu. Na usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.’”​Mathayo 6:9-13.

Ona kwamba Yesu alisema: “Basi, ninyi msali hivi.” Alimaanisha nini? Yesu hakumaanisha kwamba wafuasi wake wakariri au kurudia-rudia maneno yake kama kasuku. Alikuwa ametoka tu kuwakataza wasifanye hivyo. (Mathayo 6:7) Badala yake, sala yake inatoa somo kuhusu mambo ya kutanguliza​—mambo yaliyo muhimu, machoni pa Mungu, si machoni petu tu. Ili kujua ni mambo gani tunayopaswa kutanguliza, tunahitaji kuelewa maana ya maneno ya Yesu. Acheni basi tuchunguze maneno yake, moja baada ya lingine.

Sala ya Kielelezo Yafafanuliwa

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” Kwa kufaa Yesu alimwita Mungu “Baba” kwa sababu yeye ni mwenye upendo na anawalinda watoto wake, kama vile tu baba mzuri wa kibinadamu. Pia, yeye ana jina lake la kibinafsi—Yehova—​ambalo halipaswi kuchukuliwa kuwa jina la cheo sawa na majina yake mengine ya cheo, kama vile Mweza-Yote, Mungu, na Bwana. * (Zaburi 83:18) Lakini kwa nini jina la Mungu, ambalo linahusisha sifa yake, linahitaji kutakaswa, au kufanywa kuwa takatifu? Ni kwa sababu jina hilo limeshutumiwa na kuvunjiwa heshima.

Watu fulani humlaumu Mungu kwa sababu ya majaribu yanayowapata, lakini huenda majaribu hayo yakasababishwa na wanadamu au huenda ni kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa. (Methali 19:3; Mhubiri 9:11) Wengine wamemshutumu Mungu kuwa ndiye anayesababisha misiba ya asili. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Na dini nyingi zinafundisha kwamba Mungu anawaadhibu waovu kwa kuwatesa milele katika moto wa mateso, fundisho ambalo humchukiza sana Mungu mwenye upendo. (Yeremia 19:5; 1 Yohana 4:8) Waroma 6:23 inasema kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” wala si kuteswa milele! *

“Ufalme wako na uje.” Ufalme wa Mungu ni serikali iliyo chini ya Yesu Kristo, ambaye ndiye Mfalme wake. Hivi karibuni ataitawala dunia yote. Danieli 7:14 inasema hivi: “Naye akapewa utawala na heshima na ufalme.” Ufalme wa Mungu ‘utakuja’ wakati utakapoingilia shughuli za wanadamu na kuziponda tawala zote zinazoupinga na kuchukua mamlaka duniani pote.​—Danieli 2:44.

“Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Chini ya utawala wa Ufalme, wanadamu watajitiisha kwa mapenzi ya Mungu. Kwa sababu hiyo, kutakuwa na amani ya kweli na wanadamu wote watamwabudu Mungu kupatana na mapenzi yake. Siasa na dini ya uwongo ambayo huleta migawanyiko haitakuwepo tena. Kwa njia ya mfano, “hema la Mungu” litakuwa “pamoja na wanadamu,” inasema Ufunuo 21:3, 4, “naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

“Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” Baada ya kutanguliza jina na Ufalme wa Mungu, Yesu alitaja mahitaji yetu. Maneno yake yanaonyesha kwamba tunapaswa kuepuka kufuatilia mambo ambayo yanazidi yale tunayohitaji “kwa ajili ya siku hii.” Badala yake, tunapaswa kutii shauri linalopatikana kwenye Methali 30:8: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile chakula nilichoamriwa.”

“Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” Hapa neno “madeni,” linamaanisha “dhambi.” * Sisi sote tuna deni la kumtii Mungu. Kwa hiyo tunapokosa kumtii, au tunapomtendea dhambi, ni kana kwamba tunajirundikia deni. Ingawa hivyo, Yehova yuko tayari kutusamehe deni hilo ikiwa tutawasamehe kwa fadhili wale wanaotutendea dhambi.​—Mathayo 18:21-35.

“Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” “Yule mwovu” ni Shetani Ibilisi, ambaye pia huitwa “Mjaribu.” (Mathayo 4:3) Kwa kuwa mwili wetu wenye dhambi ni dhaifu, tunahitaji msaada wa Mungu ili kumpinga Shetani na wawakilishi wake wa kibinadamu.​—Marko 14:38.

Sala ya kielelezo ya Yesu na ikusaidie kuboresha sala zako, labda kwa kubadili mambo unayotanguliza. Sala ya kielelezo ya Yesu inakaziaje ujumbe mkuu wa Biblia? Kupatana na maneno ya Yesu, kichwa kikuu cha Biblia ni kutakaswa kwa jina takatifu la Mungu, kuondolewa kwa uovu wote, na utawala wenye amani wa Ufalme wa Mungu hapa duniani. Naam, sala ya kielelezo ya Yesu ina hazina nyingi sana za kiroho!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Katika maandishi ya awali ya Biblia, hasa yale yaliyoandikwa katika Kiebrania na Kigiriki, jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi. Kwa kusikitisha, tafsiri nyingi za kisasa zinatumia majina ya Mungu ya cheo badala ya jina lake takatifu.

^ fu. 9 Wafu hawaendelei kuishi katika njia fulani, lakini wako “usingizini,” au “hawajui lolote kamwe,” hadi watakapofufuliwa wakati ujao.​—Yohana 5:28, 29; 11:11-13; Mhubiri 9:5.

^ fu. 13 Ona Luka 11:4, ambapo maneno yote mawili yanatumiwa.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Yesu alimaanisha nini aliposema: “Basi, ninyi msali hivi”?​—Mathayo 6:9.

● Ni mambo gani tunayopaswa kutanguliza katika sala zetu?​—Mathayo 6:9, 10.

● “Madeni yetu” ni nini, na kwa nini tunapaswa kuwasamehe wale wanaotutendea dhambi?​—Mathayo 6:12.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sala ya kielelezo ya Yesu inaweza kukusaidia kujua mambo ya kutanguliza ambayo ni muhimu machoni pa Mungu, si machoni pako tu