Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kufanya Amani?

Unawezaje Kufanya Amani?

Maoni ya Biblia

Unawezaje Kufanya Amani?

BIBLIA inasema hivi kuhusu wanadamu: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa sababu wanadamu zaidi ya bilioni saba waliopo duniani si wakamilifu, tofauti za nyutu haziwezi kuepukika. Tunawezaje kufanya amani chini ya hali hizo?

Biblia inatoa mashauri mazuri. Inaeleza kwamba Muumba wetu ambaye jina lake ni Yehova, ni “Mungu wa amani.” (Waebrania 13:20; Zaburi 83:18) Yehova anataka watoto wake wanaoishi duniani wawe na mahusiano yenye amani. Naye anatuwekea mfano mzuri katika jambo hilo. Wanadamu wa kwanza wawili walipofanya dhambi na hivyo kuvunja uhusiano wenye amani kati yao na Mungu, alichukua hatua mara moja ya kupatanisha uhusiano wake pamoja na wanadamu. (2 Wakorintho 5:19) Fikiria mambo matatu unayoweza kufanya ili ufanye amani na wengine.

Samehe kwa Hiari

Biblia inasema nini? “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Wakolosai 3:13.

Kwa nini ni vigumu? Huenda una “sababu ya kulalamika” na unaona ni haki kuvunja uhusiano wako na aliyekukosea. Pia, huenda ukawa na maoni ya kwamba aliyekukosea anapaswa kuomba msamaha kwanza. Lakini ikiwa mtu hajui kwamba amekukosea, au anaamini kwamba wewe ndiye mwenye makosa, mzozo huo utaendelea bila kutatuliwa.

Unaweza kufanya nini? Fuata shauri la Biblia na usamehe kwa hiari, hasa ikiwa ni kosa dogo. Kumbuka kwamba ikiwa Mungu angehesabu makosa yetu, hatungeweza kusimama mbele zake. (Zaburi 130:3) Biblia inasema kwamba “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:8, 14.

Fikiria pia methali hii ya Biblia: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” (Methali 19:11) Ufahamu hutusaidia kuchanganua jambo kwa undani zaidi, kutambua sababu iliyomfanya mtu aseme au kutenda kwa njia fulani. Kwa hiyo jiulize, ‘Je, mtu aliyenikosea alikuwa amechoka, alikuwa mgonjwa, au alikuwa chini ya mkazo fulani?’ Kutambua nia, hisia, na hali za wengine kunaweza kupunguza hasira yako na kukusaidia kutozingazitia makosa yao.

Zungumzieni Jambo Hilo

Biblia inasema nini? “Ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.”—Mathayo 18:15.

Kwa nini ni vigumu? Hisia zisizofaa kama vile woga, hasira, na aibu zinaweza kukuzuia kumfikia yule mtu mwingine ili kutatua tatizo hilo. Pia huenda ukataka wengine wakuunge mkono kwa kuwaambia kuhusu tatizo hilo, na hivyo kufanya hali iwe mbaya hata zaidi.

Unaweza kufanya nini? Ikiwa ni tatizo zito na unaona kwamba huwezi kulipuuza, mfikie mtu huyo na mlizungumzie. Jaribu kushughulika na tatizo hilo katika njia zifuatazo:

(1) Haraka: Usiahirishe. Ukiahirisha huenda tatizo likawa kubwa. Jaribu kufuata shauri hili la Yesu: “Ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.”—Mathayo 5:23, 24.

(2) Faraghani: Epuka kuzungumza na wengine kuhusu jambo hilo. “Jitetee kwa mwenzako, wala usifunue mazungumzo ya siri ya mwingine.”—Methali 25:9.

(3) Kwa amani: Epuka mwelekeo wa kuchanganua ni nani aliye na makosa. Lengo lako ni kufanya amani, si kushinda ugomvi. Jaribu kutumia neno “mimi” badala ya “wewe.” Unaweza kupata matokeo mazuri zaidi ukimwambia, “Ninahisi uchungu kwa sababu . . . ” badala ya kusema: “Uliniumiza!” Biblia inasema: “Tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.”—Waroma 14:19.

Uwe Mstahimilivu

Biblia inasema nini? “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Lakini, ‘ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe.’”—Waroma 12:17, 20.

Kwa nini ni vigumu? Ikiwa mwanzoni mtu yule mwingine anakataa jitihada zako za kufanya amani, huenda ukahisi kana kwamba utakata tamaa.

Unaweza kufanya nini? Uwe na subira. Watu wanatofautiana katika utu na ukomavu. Huenda watu fulani wakachukua muda kupunguza hasira; wengine bado wanajifunza kuonyesha sifa za Kikristo. Endelea kuwatendea kwa fadhili na upendo. Biblia inasema: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.”—Waroma 12:21.

Ili tufanye amani pamoja na wengine, tunahitaji kuonyesha unyenyekevu, ufahamu, subira, na upendo. Lakini kuna faida nyingi za kuwa na mahusiano yenye amani!

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Ni nini kitakachokusaidia usamehe kwa hiari?—Wakolosai 3:13.

● Ni nini kitakachokusaidia umfikie mtu na kuzungumzia tatizo?—Mathayo 5:23, 24.

● Unaweza kufanya nini ikiwa jitihada zako za kufanya amani zinakataliwa?—Waroma 12:17-21.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.”—METHALI 19:11