Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Familia Za Kambo Zilizofanikiwa

Familia Za Kambo Zilizofanikiwa

Familia Za Kambo Zilizofanikiwa

HATUISHI TU KATIKA NYUMBA MOJA

Binti ya Philip, Elise, mwenye umri wa miaka 20 aliyekuwa akiishi na baba yake alikuwa amejichukulia jukumu la kutunza nyumba yao. Baada ya Philip kumwoa Louise, je, mama huyo wa kambo na binti wa kambo wangekuwa na uhusiano mzuri?

Louise: Mwanzoni mambo yalikuwa magumu sana. Mimi hupenda kukaa nyumbani na kufanya kazi za nyumba na nilitaka kutimiza madaraka yangu nikiwa mke.

Elise: Louise alipanga upya kila kitu na kutupa baadhi ya vitu vyetu. Wakati mmoja, nilikuwa nikipanga nyumba na kwa makosa nikaweka vitu fulani mahali pasipofaa kwa kuwa mpangilio ulikuwa umebadilika. Jambo hilo lilimkasirisha Louise, na tukatupiana maneno makali, na sikuzungumza naye kwa juma moja.

Louise: Pindi moja nilimwambia Elise, “Sijui itakuwaje, lakini siwezi kuvumilia uhasama tulio nao.” Jioni hiyo alinijia na kuniomba msamaha. Nilimkumbatia na sote tukalia.

Elise: Louise aliacha baadhi ya picha zangu ukutani, na Baba hakuondoa taa nilizokuwa nimeweka sebuleni. Huenda jambo hilo likaonekana kuwa dogo, lakini hilo lilinisaidia kuhisi kwamba nyumba yetu haijabadilika kabisa. Ninathamini jinsi ambavyo Louise humtunza ndugu yangu mdogo anapokuja kututembelea. Miaka miwili imepita, na sasa nimeanza kumwona Louise kuwa sehemu ya familia yetu.

Louise: Ninahisi kwamba sisi si watu wanaoishi tu katika nyumba moja, mimi na Elise tumekuwa marafiki wa karibu.

‘UMOJA NI MUHIMU ZAIDI’

Anton na Marelize walikuwa na watoto watatu kila mmoja walipooana miaka sita iliyopita.

Anton: Sisi hufanya mambo tukiwa familia kama vile kwenda kuishi katika hema wakati wa likizo, nasi hutenga wakati wa kuwa pamoja na kila mtoto akiwa peke yake. Ilituchukua miaka kadhaa kuhisi kwamba sisi ni familia, lakini kufikia sasa tumetatua matatizo mengi ya familia.

Marelize: Ni muhimu kwetu kuwaona watoto wote kuwa “wetu” si “wako” au “wangu.” Nakumbuka siku moja nilikasirika kwa kuwa nilihisi Anton alimtia nidhamu mmoja wa wana wangu isivyofaa na akamruhusu binti yake aketi kwenye kiti cha mbele katika gari. Nilijifunza kwamba umoja wa familia ni muhimu zaidi kuliko mambo mengine kama vile, kuketi katika kiti cha mbele. Sisi hujaribu kuwatendea wote kwa usawa ingawa hatuwezi kumtendea kila mtu kwa njia ileile.

Pia mimi huepuka kuzungumzia pindi zenye furaha tulizokuwa nazo katika familia yetu ya zamani kwa kuwa wale ambao hawakuwepo wakati huo watahisi kwamba tunaipenda zaidi familia ya zamani. Badala yake, mimi hushukuru kwa familia yetu ya sasa.

‘TOA PONGEZI KWANZA’

Francis na Cecelia walifunga ndoa miaka minne iliyopita. Familia yao inatia ndani watoto watatu wa Cecelia ambao ni watu wazima na kijana wa Francis.

Francis: Mimi hujaribu kuwa mwenye kufikika nami huepuka kukasirika upesi. Sisi hula milo pamoja kwa ukawaida, nasi hutumia fursa hiyo kuzungumza tukiwa familia. Pia, mimi huwatia moyo watoto wote washiriki kufanya kazi za nyumbani, kwa kuwa hilo linafaidi familia nzima.

Cecelia: Mimi hutenga wakati wa kuwa na kila mtoto na kusikiliza mahangaiko yao na mambo yanayowakasirisha. Tunapokuwa na mkutano wa familia, sisi hujaribu kutoa pongezi kwanza na kisha kuwatia moyo warekebishe mambo fulani. Na ninapokosea, mimi hukubali kosa langu na kuomba msamaha kutoka moyoni.

NILILELEWA NA WAZAZI WAWILI WA KAMBO

Yuki, mwenye umri wa miaka 20, hajamwona baba yake tangu alipokuwa na umri wa miaka mitano. Baadaye, mama yake aliolewa tena na Tomonori. Lakini Yuki alipokuwa na umri wa miaka kumi, mama yake alikufa. Miaka mitano baadaye, Yuki alijipata akiishi na wazazi wawili wa kambo, wakati ambapo Tomonori alimwoa Mihoko.

Yuki: Baba yangu wa kambo alipoamua kuoa tena, nilijiambia, “Singependa kuwa na mama wa kambo. Tayari kumekuwa na mabadiliko mengi maishani mwangu.” Hali hiyo haikunifurahisha hata kidogo, nami nilimtendea mama wa kambo kwa ubaridi.

Mihoko: Hata ingawa mume wangu hakunishinikiza nimpende mwana wake wa kambo kama alivyompenda, niliazimia kujaribu kuwa na uhusiano mzuri na Yuki. Tulijitahidi sana kufanya mambo aliyozoea kama vile kushiriki katika utendaji wa kiroho, tafrija, na kula mlo wa jioni pamoja halafu kuwa na mazungumzo baadaye. Nilielewa hisia zake vizuri zaidi tulipozungumza kuhusu kifo cha mama yake.

Nilipopata mimba, tulikuwa na wasiwasi kuhusu Yuki na tulitaka ahisi kwamba bado yeye ni sehemu ya familia yetu. Tulimruhusu Yuki amlishe na kumwosha mtoto na pia kumbadili nepi, na tulimpongeza mbele ya watu kwa msaada wake. Mtoto huyo anayeitwa Itsuki anampenda sana Yuki. Hata kabla ya kujifunza maneno “baba” na “mama,” alijifunza kusema niinii, yaani, kaka.

Yuki: Ukiwa mtoto wa kambo, ni kawaida kujihisi mpweke na kuwa wewe si sehemu ya familia. Unapojaribu kuwaeleza wengine hisia zako, hawaelewi. Hata hivyo, ninafurahi kusema kwamba Wakristo wenzangu wamenitegemeza kikweli. Wasiwasi niliokuwa nao kumwelekea mama yangu wa kambo umekwisha. Yeye hunipa mashauri mazuri, na ninaweza kumwambia yaliyo moyoni.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Uwe na subira! Familia za kambo zinaweza kufanikiwa na kuwa na furaha