Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Mwenye Haki Zaidi

Jinsi ya Kuwa Mwenye Haki Zaidi

Jinsi ya Kuwa Mwenye Haki Zaidi

MUUMBA wetu anataka tuwe na furaha, tuwe na amani ya moyoni, na tuwasaidie wengine kuwa na furaha. Hivyo anatuomba ‘tutende haki na kupenda fadhili.’ (Mika 6:8) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Tunahitaji kusitawisha sifa ambazo zitatuzuia kutenda kwa ukosefu wa haki. Hebu tuchunguze jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia kufanya hivyo.

KUSHINDA PUPA. Njia bora zaidi ya kushinda pupa ni upendo—si upendo wa kijuujuu tu au wa kimahaba—bali ni upendo wa kujidhabihu kwa ajili ya wengine. Upendo wa aina hiyo ni “wenye fadhili,” na “hautafuti faida zake wenyewe,” inasema 1 Wakorintho 13:4, 5. Isitoshe, upendo huo hauonyeshwi tu kwa watu wa familia na marafiki. Yesu aliuliza hivi: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, mna thawabu gani?” Kisha akaongezea kusema kwamba hata watu wasiomjua Mungu huwapenda wale wanaowapenda wao.—Mathayo 5:46.

KUSHINDA UBAGUZI. Andiko la Matendo 10:34, 35 linasema: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” Mungu hawahukumu watu kwa kutegemea rangi yao, hali yao ya kiuchumi, au jinsia yao. Machoni pake, “hakuna Myahudi wala Mgiriki, hakuna mtumwa wala mtu huru, hakuna mwanamume wala mwanamke.” (Wagalatia 3:28) Tunapomwiga Mungu, tunashinda ubaguzi. Fikiria mfano wa Dorothy, aliyekuwa akiishi Marekani.

Dorothy alikasirishwa sana na ubaguzi wa rangi hivi kwamba alitaka kujiunga na kikundi cha uasi chenye kutumia silaha ili kuwakomboa watu weusi waliokuwa wakikandamizwa. Hata hivyo, alihudhuria mkutano wa Kikristo wa Mashahidi wa Yehova na akakaribishwa kwa uchangamfu sana na watu weusi na pia wazungu. Muda si muda, alitambua kwamba ni Mungu peke yake anayeweza kubadili nyutu za watu. Alipoonyeshwa upendo wa kweli na Mashahidi wazungu—watu ambao alisema kwamba “hangesita kuwaua ili kuendeleza jitihada za waasi”—moyo wake “uliguswa sana” hivi kwamba alilia sana.

KUSHINDA MIELEKEO YA UHASAMA DHIDI YA JAMII. Kabla ya kuwa Wakristo, baadhi ya wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza walikuwa walevi, wenye kupenda raha, wanyang’anyi, na watukanaji. Lakini, kwa msaada wa Mungu, waliacha tabia hizo mbaya na kusitawisha upendo, fadhili, na wema. (1 Wakorintho 5:11; 6:9-11; Wagalatia 5:22) Vivyo hivyo leo, mamilioni ya watu wamefanya mabadiliko makubwa maishani mwao ili wamwabudu Mungu. Mfano mmoja ni Firuddin, anayeishi Azerbaijan.

Firuddin alilelewa katika makao ya watoto yatima, na mara nyingi alipigana na wavulana wengine. Alipokuwa mtu mzima akawa mwalimu wa mbinu ya kupigana kwa mikono kama vile tae kwon do. Anasema: “Nilikuwa mfidhuli, mkatili, na mwenye jeuri. Ikiwa wakati wa chakula mke wangu, Zahra angesahau chochote—hata kijiti cha kuchokolea meno—ningempiga. Na ikiwa mtu yeyote angemtazama tulipokuwa tukitembea barabarani, ningempiga mtu huyo!”

Siku moja, moyo wa Firuddin uliguswa sana alipojifunza kwamba Yesu alimwomba Mungu awasamehe askari-jeshi waliomtundika mtini. (Luka 23:34) ‘Ni Mwana wa Mungu peke yake anayeweza kutenda kwa njia hiyo,’ akajiambia. Kwa sababu hiyo, Firuddin alitaka kujifunza mengi kumhusu Mungu. Mashahidi wa Yehova walipojitolea kumsaidia, alikubali mara moja kujifunza Biblia pamoja nao bila malipo. Punde si punde, utu wake ukaanza kubadilika. Kwa kweli, alikuwa na fadhili sana kumwelekea Zahra hivi kwamba yeye pia akachochewa kujifunza Biblia. Leo, wote wawili wameungana kwa amani katika ibada ya kweli.

Bila shaka, mabadiliko ambayo sisi binafsi tunafanya hayawezi kukomesha ukosefu wa haki ulimwenguni pote! Hata hivyo, namna gani ikiwa Mungu anakusudia kuleta ulimwengu mpya wenye haki ya kweli? Kwa kweli, yeye ana uwezo wa kufanya hivyo! Pia fikiria hili: Kwenye 2 Timotheo 3:1-4, andiko ambalo lilinukuliwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia, tuliona kwamba Biblia ilitabiri waziwazi tabia ya watu kwa ujumla katika siku zetu. Kama tu ilivyo kuhusu unabii mwingine mwingi katika Biblia, kila jambo katika unabii huo limetimia kikamili. Kwa hiyo, si jambo la kipumbavu kuweka tumaini letu katika ahadi ya Mungu ya kukomesha ukosefu wote wa haki. Kwa kweli, Mungu atatimiza kusudi hilo. Jinsi gani?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

JITIHADA ZA HEIDE ZA KUTAFUTA HAKI

“Nilikasirishwa sana na ubaguzi wa rangi, vita, umaskini, na ukosefu mwingine wa haki, na nilikuwa nikitafuta suluhisho,” anasema Heide, anayeishi Marekani. “Nilijaribu kushirikiana na harakati za kutetea haki za raia na mwishowe nilijiunga na chama cha kisiasa, lakini hazikuweza kuondoa ukosefu wa haki.

“Nilihisi kwamba mabadiliko makubwa yalihitajika, na niliona kwamba harakati za watu walioishi maisha ya kihuni zingeweza kufaulu. Lakini harakati hizo pia zilinikatisha tamaa. Niligundua kwamba wengi kati ya watu hao walipendezwa tu na ngono, dawa za kulevya, na muziki wa rock and roll badala ya kuleta mabadiliko, na hilo lilinifanya nishuke moyo sana. Kisha nikakutana na Shahidi wa Yehova. Alinionyesha kutoka katika Biblia mabadiliko ambayo Mungu anakusudia kuleta. Kwa mfano, alinionyesha maandiko kama vile Ufunuo 21:3, 4 linalosema kwamba Mungu atafuta machozi kutoka katika nyuso zote na kuondoa maombolezo, kilio, na maumivu—mambo ambayo mara nyingi husababishwa na ukosefu wa haki. Nilijiuliza, ‘Kweli ahadi hizi zitatimia?’

“Nilisadikishwa kwamba zitatimia niliposoma katika Maandiko kuhusu nguvu na upendo wa Mungu na nilipojionea mwenyewe upendo kati ya Mashahidi wa Yehova. Sasa ninatazamia kwa hamu kutimizwa kwa ahadi za Mungu.”

[Picha katika ukurasa wa 6]

Tunashinda ubaguzi tunapoiga upendo wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Firuddin akiwa na mke wake, Zahra