Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”—Jinsi Gani?

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”—Jinsi Gani?

Maoni ya Biblia

“Kweli Itawaweka Ninyi Huru”—Jinsi Gani?

MAMILIONI ya watu wadhani kwamba wako huru, lakini sivyo. Kwa mfano, wengi ni watumwa wa ushirikina. Wengine huwahofu wafu na wanatumia pesa nyingi kutoa dhabihu ili kuwatuliza. Nao wengine, kwa kuwa hawajui kinachompata mtu anapokufa, wana woga usiofaa wa kifo. Je, watu hao wanaweza kuwekwa huru kutokana na mambo hayo yanayowalemea kiakili, kihisia, na hata kifedha? Ndiyo! Kama maneno ya Yesu Kristo yaliyonukuliwa hapo juu yanavyoonyesha, kweli tu ndiyo inayoweza kuwaweka huru. Lakini kweli ni nini? Je, ni kweli tu kwa ujumla au ni kweli fulani hususa?

Yesu alitoa jibu la wazi. Alisema: “Mkikaa katika neno langu, . . . mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:31, 32) “Neno” la Yesu ni mafundisho yake yanayopatikana katika Biblia.

Yesu aliposema kwamba “kweli itawaweka ninyi huru,” alimaanisha hasa kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo. Hata hivyo, kujua kweli inayopatikana katika Neno la Mungu pia hutuweka huru kutokana na mambo kama vile ushirikina, kuhofu wafu, na woga usiofaa wa kufa. Jinsi gani?

1. Kuwekwa huru kutokana na ushirikina. Watu wengi huamini kwamba vitu au nambari fulani huleta bahati mbaya. Wengine huepuka kufanya maamuzi muhimu hadi kwanza wachunguze ikiwa kuna dalili ya kupata bahati njema au watafute mashauri kutoka kwa mnajimu au mtu anayewasiliana na pepo.

Jinsi kweli ya Biblia inavyotuweka huru: Katika nyakati za Biblia, baadhi ya watu wa Mungu walikuwa washirikina sana hivi kwamba hata walianza kuabudu “mungu wa Bahati Njema” na “mungu wa Majaliwa”! Yehova Mungu alionaje jambo hilo? Alisema: “Mliendelea kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pangu.” (Isaya 65:11, 12) Mungu alihisi vivyo hivyo kuelekea wale wanaotafuta mwongozo kutoka kwa watu wanaowasiliana na pepo: “Yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo . . . ni chukizo kwa Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 18:11, 12.

Ushirikina na wale wanaowasiliana na pepo ni hatari kwa sababu wanatumia “hila za Ibilisi,” ambaye Yesu alimwita “baba ya uwongo.” (Waefeso 6:11; Yohana 8:44) Ikiwa ungetaka mwongozo kuhusu jambo fulani muhimu, je, ungetafuta mashauri kutoka kwa mtu mwongo? Bila shaka la! Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuepuka kitu chochote kinachohusiana na “baba ya uwongo.”

Siri ya kufanya maamuzi mazuri maishani ni kutumia hekima inayotegemea ujuzi sahihi wa kanuni za Biblia na kusudi la Mungu kwa wanadamu. Methali 2:6 inasema: “Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.”

2. Kuwekwa huru kutokana na hofu ya wafu. Watu wengi wanaamini kwamba “roho” za mababu waliokufa zinaweza kuwadhuru au kuwasaidia walio hai. Wanasema kwamba “roho” hizo lazima zitulizwe kwa kutoa dhabihu mbalimbali ili zisikasirike. Kwa sababu hiyo, watu fulani hukopa pesa nyingi ili kulipia dhabihu na sherehe kubwa.

Jinsi kweli ya Biblia inavyotuweka huru: Biblia hutuambia ukweli kuhusu hali ya wafu. Kwa mfano, Yesu alisema kwamba wafu wako “usingizini.” (Yohana 11:11, 14) Alimaanisha nini? Jibu linapatikana kwenye Mhubiri 9:5: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” Ni kana kwamba wafu wako katika usingizi mzito, hawana fahamu kabisa. Kwa kweli, hawapo tena, kwa hiyo hawawezi kututendea mema au kutudhuru.

Ingawa hivyo, watu fulani hudai kwamba wamewahi kuwasiliana na wafu. Hilo linawezekanaje? Biblia inajibu. Inatuambia kwamba mapema katika historia ya mwanadamu, malaika kadhaa walimwasi Mungu. (2 Petro 2:4) Roho hao waovu hujaribu kuwadanganya wanadamu. (1 Timotheo 4:1) Njia moja wanayotumia ni kujifanya kuwa wao ni watu waliokufa, na hivyo kuendeleza uwongo wa kwamba wafu huendelea kuishi katika umbo lingine au ulimwengu mwingine.

3. Kuwekwa huru kutokana na woga usiofaa wa kifo. Kifo kwa kweli ni adui kama Biblia inavyosema. (1 Wakorintho 15:26) Kwa hiyo, tuna sababu nzuri ya kuogopa kifo na kujaribu kukiepuka. Hata hivyo, hatupaswi kuwa na woga usiofaa wa kifo.

Jinsi kweli ya Biblia inavyotuweka huru: Mbali na kufunua ukweli kuhusu hali ya wafu, Biblia pia inaonyesha kwamba Mungu anakusudia kuwafanya wafu wawe hai tena kwa kuwafufua. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Kristo] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

‘Watatoka’ wakiwa na umbo gani? Yesu alitoa jibu alipowafufua watu kadhaa. Katika kila kisa, mtu alirudi katika umbo la kibinadamu—jinsi alivyokuwa kabla ya kufa. (Marko 5:35-42; Luka 7:11-17; Yohana 11:43, 44) Hilo linapatana na neno “ufufuo,” ambalo linamaanisha “kusimama.” Alipokuwa akizungumza na mtumishi wake Danieli aliyekuwa amezeeka, Mungu alisema: “Utapumzika [au kulala usingizi katika kifo], lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:13) Lazima maneno hayo yawe yalimfariji Danieli na kumwezesha kukabiliana na kifo bila woga!

Utume wa Yesu ulitia ndani “kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka”—wale ambao ni watumwa wa mafundisho ya uwongo. (Luka 4:18) Kwa kuwa mafundisho yake yanapatikana katika Biblia, yanaendelea kuwaweka watu huru kila siku. Tunatumaini kwamba kweli ya Biblia itakuweka huru kabisa.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

Kweli ya Biblia hutuwekaje huru kutokana na

● ushirikina?—Isaya 8:19, 20; 65:11, 12.

● hofu ya wafu?—Mhubiri 9:5; Yohana 11:11, 14.

● kuogopa kifo?—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Kweli ya Biblia huwaweka watu huru kutokana na ushirikina, hofu ya wafu, na woga usiofaa wa kufa