Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maendeleo Makubwa Nchini Malawi—Majumba 1,000 ya Ufalme!

Maendeleo Makubwa Nchini Malawi—Majumba 1,000 ya Ufalme!

Maendeleo Makubwa Nchini Malawi​—Majumba 1,000 ya Ufalme!

“SIKUDHANI jambo hilo litawezekana nchini Malawi,” akasema Augustine. Alikuwa akizungumzia ujenzi wa Majumba mengi ya Ufalme, jina ambalo Mashahidi wa Yehova huita mahali wanapofanyia ibada. Katika mwaka wa 1993, Mashahidi huko Malawi hawakuwa na mahali panapofaa kwa ajili ya ibada na kujifunza Biblia. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi 30,000 katika nchi hiyo ndogo iliyoko kusini-mashariki mwa Afrika.

Hata hivyo, sasa mambo yamebadilika kabisa. Mnamo Septemba 2010, Mashahidi huko Blantyre, nchini Malawi, walikamilisha ujenzi wa Jumba la Ufalme la 1,000! * Kwa nini Mashahidi hao walifikia idadi ya 30,000 kabla ya kuanza kujenga mahali pa ibada? Na waliwezaje kujenga majumba 1,000 kwa muda mfupi hivyo katika nchi isiyo na uwezo mkubwa wa kifedha? Na programu hiyo ya ujenzi yenye kusisimua imekuwa na matokeo gani kwa Mashahidi na jirani zao?

Nyakati Zenye Majaribu

Mapema katika miaka ya 1900, Mashahidi wa Yehova, ambao wakati huo walijulikana kama Wanafunzi wa Biblia, walianza kufundisha kweli za Biblia nchini Malawi. Kufikia mwaka wa 1967, idadi ya Mashahidi ilikuwa imefika 17,000 hivi. Kama tu Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi hao walijulikana kuwa watu wanaotii sheria na kuheshimu maofisa wa serikali. Vilevile kama Wakristo wa karne ya kwanza, walidumisha msimamo thabiti wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa.—Yohana 18:36; Matendo 5:29.

Kwa kusikitisha, kufikia katikati ya miaka ya 1960, msimamo wao unaotegemea Biblia ulifanya wahitilafiane na serikali, na katika mwaka wa 1967, walipigwa marufuku. Baada ya hapo, wengi wao walifutwa kazi bila sababu, na vikundi fulani vya wapinzani vilipora au kuharibu mali zao. Kwa sababu ya kuteswa sana na pia kwa sababu ya kuhofu kwamba wangeuawa, maelfu ya Mashahidi walitorokea nchi jirani za Msumbiji na Zambia.

Hata hivyo, baadaye mateso ya Mashahidi wa Yehova nchini Malawi yalipungua, na wengi waliruhusiwa kurudi kwao mwanzoni mwa miaka ya 1990. Agosti 12, 1993 walifurahi kama nini kwamba baada ya miaka 26, marufuku juu ya kazi yao iliondolewa! Hata hivyo, tatizo jipya lilizuka. Wakiwa Mashahidi zaidi ya 30,000 katika makutaniko 583, hawakuwa na mahali panapofaa pa kukutania ili kuabudu! Wangefanya nini?

Upendo Waonyeshwa kwa Matendo!

Miaka sita ya kwanza baada ya marufuku kuondolewa, Mashahidi wenyeji walifanya kazi nzuri sana ya kujenga Majumba ya Ufalme kwa kutumia uwezo wao mdogo wa kifedha. Lakini hilo halikuwa jambo rahisi kwa sababu kila mwaka, Mashahidi waliongezeka kwa kiwango ambacho kilizidi idadi ya Majumba ya Ufalme. Tatizo hilo lingeshughulikiwaje? Kanuni ya Biblia iliyo kwenye 2 Wakorintho 8:14 ilitumiwa. “Kupitia usawazisho,” fedha za ziada katika nchi nyingine ‘zilijazia upungufu’ wa nchi kama ya Malawi. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1999 Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilianzisha mpango maalumu wa kusaidia ujenzi wa majengo ya ibada katika nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha. Kupitia msaada huo wenye upendo, Mashahidi nchini Malawi walijenga Majumba mengi ya Ufalme kwa haraka sana. *

Hapo awali, makutaniko nchini Malawi yalifanya mikutano yao katika madarasa ya shule, katika vibanda, au hata chini ya miti. Kwa sasa, makutaniko 1,230 yanaweza kukutana kwa ajili ya ibada na kujifunza Biblia katika majengo mazuri yaliyowekwa wakfu ili kuendeleza ibada ya kweli. Kama unavyoweza kuwazia, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 75,000 nchini Malawi wanathamini sana utegemezo wanaopata kutoka kwa ndugu na dada zao wa kiroho ulimwenguni pote.

Jambo lingine lililowasaidia Mashahidi hao kujenga majumba mengi ya ibada kwa muda mfupi hivyo ni hamu yao ya kuwa na Majumba sahili, yanayofaa. Hawakutaka majumba ya kifahari. Badala yake, walitaka kuwa na majumba sahili, yaliyojengwa vizuri ambayo yanamletea Yehova heshima na yenye mazingira mazuri kwa ajili ya kuzungumzia na kujifunza Biblia.

Majirani Wafaidika

Zamani, nchini Malawi Mashahidi wa Yehova walidhihakiwa kuwa ni dini ambayo haikuwa na majengo ya ibada. Kwa sababu hiyo, baadhi ya Mashahidi waliaibika kuwaalika wenye kupendezwa mikutanoni. Kwa hiyo, wazia jinsi walivyohisi walipopata Majumba yao maridadi ya Ufalme. Sasa walifurahia kuwaalika majirani na watu waliopendezwa kwenye mikutano ya Kikristo. Katika eneo moja, kutaniko lilisisimuka kuona watu 698 kwenye mkutano katika Jumba lao jipya la Ufalme!

Mashahidi wengi na majirani wao walisema kwamba hawakuwa wamewazia wangeweza kuwa na jumba maridadi na lililo thabiti katika eneo lao. Augustine, aliyetajwa hapo mwanzoni, anaweza kukumbuka kutaniko moja ambalo lilifanya mikutano chini ya mti. “Ilipendeza sana wakati wa kiangazi,” anasema Augustine. “Lakini katika msimu wa mvua ilikuwa balaa tupu!” Kama umewahi kunyeshewa na mvua ya maeneo ya tropiki, huenda unaelewa Augustine anamaanisha nini.

Augustine anakumbuka wakati mmoja alipotembelea Kutaniko la Chimwanje. “Tulifanya mikutano katika kibanda kidogo kilichojengwa kwa miti na kuezekwa kwa nyasi,” anaeleza. “Jambo ambalo hatukujua ni kwamba paa hilo la nyasi lilikuwa nyumba ya buibui mkubwa mwenye sumu kali. Ghafula, nilipokuwa nikitoa hotuba, mdudu huyo alianguka kando ya mguu wangu! Nilimsikia mmoja wa wasikilizaji aliyeshtuka akipiga kelele, ‘Mkanyage, Augustine, Mkanyage!’ Bila shaka, nilimkanyaga. La sivyo, nisingalikuwa hai sasa.” Kwa kuwa sasa kutaniko hilo lina Jumba jipya la Ufalme, hawakengeushwi tena na mambo kama hayo.

“Kito Katika Jamii”

Mradi huo wenye kusisimua wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme umefanya watu katika jamii na machifu wawapende na kuwathamini Mashahidi wa Yehova, kama maelezo yafuatayo yanavyoonyesha:

✔ “Ujenzi wa jengo jipya la ibada, pamoja na upendo na umoja wa Mashahidi wa Yehova, ni kama kito katika jamii, mfano mzuri wa kuigwa na makanisa mengine.”—Chifu wa kijiji cha Chabwenzi.

✔ “Jambo linalonivutia zaidi kuhusu Mashahidi wa Yehova ni umoja wao. Tulianza kujenga kanisa letu miaka kumi iliyopita, lakini bado ujenzi unaendelea—na haionekani kama utakwisha hivi karibuni. Ningependa kuwashukuru kwa kujenga jumba maridadi kama hili katika eneo letu.”—Mzee wa kijiji cha Chigwenembe.

✔ “Inasisimua kuona jinsi mnavyofanya kazi. Mnajenga haraka na kwa utaratibu mzuri! Lazima muwe mna umoja kwelikweli.”—Chifu wa kijiji cha Chiuzira.

Programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme ni ya pekee sana hivi kwamba imetambuliwa na waandishi wa kamusi inayotafsiri maneno ya Chichewa na Chinyanja katika Kiingereza (Chichewa/Chinyanja—English Dictionary) kwani inasema hivi kuhusu Mashahidi: “Mashahidi wa Yehova wamejenga [Majumba ya Ufalme] mengi.”

“Jumba Hili la Ufalme Ni Muujiza”

Januari 30, 2011, Kutaniko la Manyowe katika jiji la Blantyre, lililotajwa awali, liliweka wakfu Jumba lao jipya la Ufalme—jumba la 1,000 kujengwa nchini Malawi. “Kuwa na Jumba hili la Ufalme ni muujiza,” akasema mshiriki mmoja wa kutaniko hilo. “Ni kama ndoto iliyotimia.”

“Sikukosa hata siku moja wakati wa ujenzi huo,” anasema msichana mmoja wa Kutaniko la Manyowe. “Ninafurahi sana kwamba niliweza kushiriki katika ujenzi wa mahali panapofaa kwa ajili ya ibada katika eneo letu.”

“Tulisumbuka kupata kibali kutoka kwa wenye mamlaka ili kujenga Jumba letu Ufalme,” alieleza mmoja wa wazee wa kutaniko hilo. “Mara kadhaa, maofisa wa jiji walikataa kutia sahihi stakabadhi tulizohitaji. Hata hivyo, Bi. Liness Chikaoneka ambaye ni mzee wa kijiji, alijitahidi sana kuwashawishi maofisa ili watie sahihi stakabadhi hizo.”

Siku moja, Bi. Chikaoneka aliandamana na mzee mmoja wa kutaniko alipokuwa akipeleka stakabadhi ili zitiwe sahihi. “Ninataka Mashahidi wajenge Jumba la Ufalme katika kijiji changu,” akamwambia ofisa. “Wao ni watu wazuri. Sijawahi kushughulikia shtaka lolote kuwahusu katika mahakama yangu ya kijiji.” Ofisa huyo alitia sahihi stakabadhi hizo.

Bi. Chikaoneka alifurahi sana wakati Jumba hilo la Ufalme lilipowekwa wakfu. Alisema hivi: “Nina furaha na ninajivunia kuwa na jengo hili maridadi katika kijiji changu!”

Kotekote nchini Malawi, Mashahidi wa Yehova na majirani wao wanaendelea kuonyesha uthamini kwa programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Kwa sababu ya roho yao nzuri ya kujitolea na kufanya kazi kwa bidii, katika nchi hiyo Mashahidi wa Yehova hawana tena uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme kama ilivyokuwa katika mwaka wa 1993. Ni kweli kwamba bado wataendelea kuwa na uhitaji wa Majumba zaidi ya Ufalme kadiri watu wengi wanavyoitikia vizuri “habari njema ya ufalme wa [Mungu]” na kadiri makutaniko mapya yanavyoanzishwa. (Mathayo 24:14) Hivyo basi, Mashahidi wanathamini sana utegemezo wenye fadhili na michango inayotolewa kwa ukarimu na Mashahidi wenzao ulimwenguni pote. *

Zaidi ya yote, Mashahidi wanamshukuru Mungu wao, Yehova. Maneno yao yanafanana na ya mtunga-zaburi, aliyesema hivi: “Mataifa yote ambayo umeyafanya, yatakuja yenyewe, nayo yatainama mbele zako, Ee Yehova, na kulipa utukufu jina lako. Kwa maana wewe ni mkuu na unafanya mambo ya ajabu.”—Zaburi 86:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Idadi ya Majumba ya Ufalme sasa imepita 1,030.

^ fu. 9 Tangu mwaka wa 1999, ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamejenga Majumba ya Ufalme 23,786 katika nchi 151 ambazo hazina uwezo mkubwa wa kifedha.

^ fu. 28 Ulimwenguni pote, kazi ya Mashahidi wa Yehova hutegemezwa kwa michango ya hiari.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kabla ya programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme kuanza, watu walikutana kwa ajili ya ibada katika vibanda vilivyoezekwa kwa nyasi

[Picha katika ukurasa wa 24]

Sasa makutaniko hukutana katika Majumba ya Ufalme kama hili