Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hivi Karibuni Wote Watakuwa na Chakula Chenye Lishe!

Hivi Karibuni Wote Watakuwa na Chakula Chenye Lishe!

Hivi Karibuni Wote Watakuwa na Chakula Chenye Lishe!

UNAWEZA kuchukua hatua fulani ili ufurahie kula chakula kisichokudhuru. Hata hivyo, kuna mambo mengi ambayo huwezi kudhibiti. Kwa mfano, huwezi kukagua vyakula vyote kabla ya kuvinunua au kuvitayarisha. Huenda ukalazimika kununua vyakula ambavyo vimetengenezwa viwandani na kusafirishwa kutoka mbali. Na huenda vyakula fulani ambavyo unanunua tayari vimechafuliwa na kemikali hatari zilizo kwenye hewa, kwenye maji, au kwenye udongo.

Katika ripoti moja yenye kichwa “Kudhibiti Magonjwa Yanayosababishwa na Vyakula: Tatizo la Kimataifa,” maofisa wa Shirika la Afya Ulimwenguni wanasema kwamba matatizo fulani yanayohusiana na usalama wa chakula “hayawezi kutatuliwa na serikali moja peke yake; yanahitaji ushirikiano wa kimataifa.” Magonjwa yanayosababishwa na vyakula ni tatizo la ulimwenguni pote!

Inaeleweka kwamba wengi watajiuliza ni kwa nini tunasema kwa uhakika kwamba hivi karibuni watu wote watakuwa na chakula chenye lishe. Ni kwa sababu “Yehova, Bwana wa dunia yote,” anaahidi kwamba atatatua matatizo ya chakula yanayowakumba wanadamu. (Yoshua 3:13) Huenda watu fulani wakadai kwamba kuwepo kwa chakula kinachodhuru kunathibitisha kwamba Mungu hawezi kutumainika. Lakini hebu fikiria hili: Ikiwa mhudumu hotelini ataacha chakula kizuri kiharibike, je, ingefaa kumlaumu mpishi? La hasha.

Vivyo hivyo, ni wanadamu—na si Muumba—ambao wanapaswa kulaumiwa kwa kuharibu chakula kizuri kinachozalishwa na dunia. Kuwepo kwa chakula kinachodhuru ni tatizo lililotokezwa na wanadamu. Mungu anaahidi kwamba ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—Ufunuo 11:18.

Ukweli ni kwamba tayari Mungu amethibitisha kwamba anajali kuhusu ubora wa chakula tunachokula. Yeye ndiye aliyeifanyiza dunia na kuumba miti ‘yenye kutamanika kwa macho ya mtu’ na pia inayofaa “kwa ajili ya chakula.” (Mwanzo 2:9) Hata baada ya wanadamu kuanza kuwa wagonjwa, Yehova Mungu aliwapa watu wake miongozo hususa ambayo ingelinda chakula chao na miili yao.—Ona sanduku “Mfumo wa Sheria Kuhusu Afya.”

Mungu anataka tufurahie chakula cha aina gani? Biblia inatuambia hivi: “Anafanya majani mabichi yachipuke kwa ajili ya wanyama, na mimea ili itumikie wanadamu, ili chakula kitokezwe duniani, na divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie, kuufanya uso ung’ae kwa mafuta, na mkate unaotegemeza moyo wa mwanadamu anayeweza kufa.” (Zaburi 104:14, 15) Biblia pia inasema kwamba “kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula.”—Mwanzo 9:3.

Neno lake linaahidi hivi kuhusu wakati wetu ujao: “Naye hakika ataleta mvua kwa ajili ya mbegu yako unayoipanda katika udongo, na mkate kuwa mazao ya udongo, ambao utakuwa mnono na wenye mafuta. Mifugo yako italisha katika siku hiyo katika malisho mapana.” (Isaya 30:23) Naam, hivi karibuni badala ya kuwa na vichwa vya habari vyenye kuhuzunisha kutakuwa na tangazo hili: “Watu wote wana chakula chenye lishe!”

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Muumba wetu anatuahidi wakati ujao ulio na chakula kingi kizuri

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

“MFUMO WA SHERIA KUHUSU AFYA”

Miaka 3,500 hivi iliyopita Waisraeli walipewa Sheria ya Musa. Sheria hiyo iliwalinda Waisraeli kutokana na magonjwa mengi yanayosababishwa na vyakula. Fikiria maagizo yafuatayo:

● Epukeni vyombo vyovyote ambavyo vimegusa mnyama aliyekufa: “Chombo chochote ambacho hutumiwa kwa njia fulani kitatiwa katika maji, nacho kitakuwa kisicho safi mpaka jioni halafu kitakuwa safi.”—Mambo ya Walawi 11:31-34.

● Msile mnyama aliyekufa mwenyewe: “Msile mwili wowote uliokufa tayari.” —Kumbukumbu la Torati 14:21.

● Chakula kilichobaki kinapaswa kuliwa baada ya muda mfupi: “Kesho yake kilichobaki kinaweza kuliwa. Lakini nyama inayobaki ya dhabihu katika siku ya tatu, itateketezwa kwa moto.”—Mambo ya Walawi 7:16-18.

Dakt. A. Rendle Short, anashangaa kwamba Sheria ya Musa—ikilinganishwa na sheria za mataifa mengine jirani—ilikuwa na “mfumo wa sheria kuhusu afya uliokuwa wenye hekima na rahisi kufuata.”