Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sisi Ni marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 1

Je, Sisi Ni marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 1

Vijana Huuliza

Je, Sisi Ni marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 1

JE, ULIMFIKIRIA MTU HUSUSA ULIPOSOMA SWALI LILILO HAPO JUU?

NDIYO → SOMA MAKALA HII MARA MOJA. HUENDA UTAHITAJI HABARI HII KULIKO UNAVYODHANIA.

HAPANA → HATA HIVYO UNAHITAJI. KUSOMA MAKALA HII. ITAKUSAIDIA KUHAKIKISHA KWAMBA URAFIKI JINSIA TOFAUTI HAUPITI MIPAKA HAUKULETEI MATATIZO.

Tia alama kuonyesha ikiwa sentensi ifuatayo ni kweli au si kweli:

Sipaswi kuwa na marafiki wa jinsia tofauti hadi niwe tayari kwa ajili ya uhusiano ambao hatimaye utaongoza kwenye ndoa.

․․․․․ KWELI ․․․․․ SI KWELI

Fikiria hili: Ingawa hakuwa na mpango wa kuoa, Yesu alikuwa na marafiki wa jinsia tofauti. (Mathayo 12:46-50; Luka 8:1-3) Bila shaka ilikuwa vivyo hivyo kwa mwanamume mseja Timotheo, kwa sababu mtume Paulo alimwambia awatendee “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:1, 2.

Lazima Paulo awe alijua kwamba kwa kuwa Timotheo angetumika katika makutaniko tofauti-tofauti, angekutana na wanawake wengi vijana. (Marko 10:29, 30) Je, lingekuwa kosa kwa Timotheo kuchangamana nao? La hasha. Lakini kwa sababu hakuwa na mpango wa kuoa wakati huo, Timotheo angehitaji kujiwekea mipaka ili asivutiwe kimahaba, na pia asichezee hisia za wanawake hao vijana na hivyo kuwaumiza.—Luka 6:31.

Namna gani wewe? Je, uko tayari kuoa au kuolewa?

Kama jibu lako ni NDIYO ⇨ Urafiki pamoja na watu wa jinsia tofauti unaweza kukusaidia kumpata mwenzi wa ndoa.—Methali 18:22; 31:10.

Kama jibu lako ni LA ⇨ Unahitaji kuweka mipaka. (Yeremia 17:9) Bila shaka, si rahisi kufanya hivyo, sivyo? “Si rahisi kuwa rafiki ya mtu wa jinsia tofauti bila kuvutiwa naye kimahaba,” anasema Nia, mwenye umri wa miaka 18. * “Si rahisi kujua ni mipaka gani utakayoweka.”

Kwa nini hasa unahitaji kuweka mipaka? Kwa sababu usipofanya hivyo, bila shaka utaumia au kuumiza hisia za wengine. Fikiria sababu zifuatazo.

UKWELI WA MAMBO: Unapoanza kuvutiwa na mtu kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa, mmoja wenu ataumia hisia. “Nimepatwa na hali kama hiyo mara mbili hivi,” anasema Kelli, mwenye umri wa miaka 19. “Wakati mmoja, nilianza kuvutiwa na mvulana fulani, na mara ya pili mvulana mwingine alivutiwa na mimi. Mara zote mbili mtu fulani aliumia kihisia, na visa hivyo vimeniacha na makovu moyoni.”

Jambo la kufikiria:

Ni chini ya hali gani ingefaa uchangamane na watu wa jinsia tofauti? Ni chini ya hali gani haingefaa kufanya hivyo?

Kwa nini si jambo la hekima kuzoea kuwa pamoja na mtu yuleyule kila wakati? Mtu huyo atakuwa na wazo gani akilini? Wewe utakuwa na wazo gani akilini?

“Wakati mwingine, nimejidanganya kwa kusema, ‘Ah, sisi ni marafiki tu. Yeye ni kama ndugu yangu.’ Lakini ninapomwona akianza kuvutiwa na msichana mwingine, ninaumia hisia—ni kama alipaswa kuwa na mimi tu.”—Denise.

Biblia inasema hivi: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.”—Methali 22:3, Biblia Habari Njema.

UKWELI WA MAMBO: Unapoanza kuvutiwa na mtu kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa, unaweza kupoteza rafiki mzuri. “Mimi na mvulana fulani tulikuwa tukitumiana ujumbe kupitia simu,” anasema Kati, mwenye umri wa miaka 16, “lakini punde si punde akaanza kunichezea kimahaba na tulitumiana ujumbe karibu kila siku. Halafu siku moja akaniambia kwamba ananipenda na alitaka tuwe na urafiki wa kimahaba. Tatizo ni kwamba sikuwa na hisia zozote za kimahaba kumwelekea. Baada ya kumweleza jambo hilo, tulizungumza mara chache tu, na urafiki wetu ukakoma.”

Jambo la kufikiria:

Katika kisa cha Kati, ni nani aliyeumia hisia, na kwa nini? Je, Kati au mvulana huyo wangeweza kuzuia tatizo hilo lisitokee? Wangezuiaje jambo hilo?

Unapotuma ujumbe mfupi, ni katika njia gani unaweza kuonyesha bila kukusudia kwamba unataka kuwa na urafiki wa kimahaba?

“Nyakati nyingine ninahitaji kujizuia nisitumie muda mrefu pamoja na mvulana. Wavulana wanaweza kuwa marafiki wazuri, lakini sikutaka kuharibu urafiki wetu kwa kuvuka mipaka ya urafiki.”—Laura.

Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Jambo kuu: Si vibaya kuchangamana na watu wa jinsia tofauti. Lakini ikiwa bado hujawa tayari kwa ajili ya uhusiano ambao hatimaye utaongoza kwenye ndoa, unahitaji kuweka mipaka.

KATIKA MAKALA INAYOFUATA YA “VIJANA HUULIZA” . . .

Soma jinsi unavyoweza kujiharibia sifa ikiwa utaanza kuvutiwa na mtu kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa.

Unaweza kupata makala zaidi za “Vijana Huuliza” katika Tovuti ya www.watchtower.org/ype

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

WEWE UNGEFANYA NINI?

SIMULIZI HALISI: “Nilimtumia rafiki yangu anayeishi umbali wa zaidi ya kilomita 1,500 ujumbe mfupi wa simu. Tuliwasiliana kwa njia hiyo angalau mara moja hivi kila juma. Sikuwa nimevutiwa naye kimahaba, na sikudhani kama alivutiwa nami kwa njia hiyo. Kisha, siku moja alinitumia ujumbe mfupi uliosema hivi: ‘Vipi mrembo! Nimekukosa sana. Unaendeleaje?’ Nilishtuka! Nikamwambia kwamba uhusiano wetu ulikuwa wa kirafiki tu na sikuwa ninavutiwa naye kimahaba. Alinijibu, ‘Sawa.’ Baada ya hapo, hakunitumia tena ujumbe.”—Janette.

● Ikiwa kwa sasa huwezi kuanzisha uhusiano wa karibu au hutaki kuwa na uhusiano wa aina hiyo na mtu wa jinsia tofauti, ungefanyaje kama ungepokea ujumbe kama ule ambao Janette alipokea?

● Ikiwa wewe ni mvulana, unafikiri ujumbe ambao Janette alitumiwa ulifaa? Kwa nini unasema hivyo?

● Kwa maoni yako, je, unafikiri ni rahisi zaidi kuanza kuvutiwa na mtu mwingine mnapotumiana ujumbe mfupi kuliko mnapoongea uso kwa uso? Kwa nini unasema hivyo?

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Waulize wazazi wako maoni yao kuhusu maswali yaliyoonyeshwa kwa nukta kubwa katika makala hii. Je, maoni yao yanatofautiana na yako? Ikiwa ndivyo, yanatofautianaje? Unaona maoni yao yanaweza kukufaidi jinsi gani? —Methali 11:14.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 17]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

Joshua—Kadiri unavyotumia wakati mwingi pamoja na mtu yuleyule, ndivyo unavyozidi kuvutiwa naye kimahaba.

Natasha—Ikiwa nia yako ni muwe marafiki tu, lakini unakuwa pamoja na mtu yuleyule kila wakati, hilo linaweza kuchochea hisia za kimahaba kati yenu.

Kelsey—Hata kama mwanzoni ninyi ni marafiki tu, hisia zenu zinaweza kubadilika kwa urahisi ikiwa mtatumia wakati mwingi pamoja. Si kwamba haiwezekani kuwa marafiki tu, lakini ili mfaulu lazima muwe wakomavu na wenye utambuzi.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kuonyesha hisia za kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa kutatokeza matatizo